|
|
Wakati
Bunge likihitimisha shughuli zake; Othman Matata asema:
Wakati Bunge la Bajeti likihitimisha shughuli zake; imeelezwa kwamba Waislamu hawatokubali kusingiziwa mambo ili kuhalalisha dhulma dhidi yao. Aidha imeelezwa kwamba habari zinazowahusu Waislamu zimekuwa zikipotoshwa na hata kuwasingizia mambo Waislamu ili kupata sababu ya kuwafanyia hujuma. Akiongea na gazeti hili jana Agosti 6; Mwanaharakati mashuhuri Ustadh Othman Matata amesema kwamba Waislamu wakiwa raia sawa na raia wengine katika nchi hii hawawezi kukaa kimya huku wakidhulumiwa, bali wataendelea kuvichagiza vyombo husika kama Bunge virekebishe hali hii na ikishindikana watalazimika kulichukua jambo hili katika vyombo vya Jumuiya ya Kimataifa. Akitoa mfano Ustadh Matata alisema kwamba suala la Mwembechai ambapo baadhi ya Waislamu waliuliwa na polisi haliwezi kuisha bila ya wahusika kufikishwa mahakamani. Aidha, alisema kwamba tukio la Mwembechai limekuwa ni sehemu tu ya vielelezo vya uonevu na uvunjaji wa Haki za binadamu inaofanywa nchini hapa dhidi ya Waislamu. Ustadh Matata ambaye ni mtaalam wa sheria amesema kwamba anashangazwa na hali iliyojitokeza Bungeni ambapo taarifa zisizo sahihi zilitolewa bila ya hatua zozote kuchukuliwa. Akifafanua alisema kwamba hivi karibuni. Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Ali Ameir aliliambia Bunge kwamba mwanafunzi Chuki Athumani aliyepigwa risasi na polisi alikuwa na makaratasi ya uchochezi. Mbali ya mwanafunzi huyo kukanusha; Ustadh Matata amesema; kuwa kwamba mwanafunzi huyo hakufunguliwa kesi inayotaja kosa la kukutwa na makaratasi ya uchochezi ni ushahidi kwamba aliyoyasema Mhe. Waziri Ali Ameir si sahihi. Ustadhi ambaye wakati akiongea alikuwa na nakala za mashitaka (charge sheet) za watuhumiwa wote wa Mwembechai, alisema kitendo hiki ni cha dhulma. Alisema, Mhe. Ali Ameir kwa nafasi yake kama Waziri wa Serikali hakusema kweli Bungeni. Na ni dhulma kwa sababu amesema mambo yasiyo sahihi juu ya watu ambao hawana fursa ya kuingia Bungeni kukanusha hayo wanayosingiziwa. Kwamba kamsingizia kwa kujua kwamba hawezi kuingia Bungeni kujitetea. Lakini linaloshangaza; anasema Ustadh Matata ni jinsi suala hili lilivyopita Bungeni.Kwanza anasema Wabunge wangetakiwa wamhoji Mhe. Waziri, kipi kilitangulia. Kumpiga mtoto huyo risasi ndio akakutwa na makaratasi ya uchochezi au kakutwa kwanza na makaratasi hayo ndio akapigwa risasi. Na je hiyo ndiyo hukumu kwa mujibu wa sheria? Lingine ambalo amelitaja Ustadh Othman Matata kama mfano wa mambo yaliyoelezwaBungeni na si sahihi ni suala la kulindwa kwa msikiti wa Membechai na madai kwamba Mama Chuki amesema kwamba mwanawe hataki kurudi kusoma tena Alharamain. Kwa mujibu wa maelezo ya Ustadh Matata msikiti bado unalindwa na Mama Chuki amekanusha kutoa maelezo hayo. Ustadh Matata amesema kwamba anashangazwa na utendaji kazi wa Mhe. Waziri kwani hata katika suala la Parole alishindwa kuona kosa hata baada ya Rais kuingilia kati na kuzivunja "Parole" zake. Akihitimisha kutoa maoni yake Ustadh Matata ambaye alisema anafanya hivyo kama mwananchi na kwa kutumia haki yake ya kikatiba alisema dhulma haiwezi kuachwa iendelee. Kwahiyo akasisitiza kwamba waliohusika na mauaji pale Mwembechai wafikishwe Mahakamani. Na Tume iundwe kujua kwanini na nini chanzo cha dhulma wanayofanyiwa Waislamu; athari zake kwa Taifa letu sasa na baadae na namna ya kuliondoa tatizo hilo. Akiongea na mwandishi wa habari hizi kutokea Dodoma jana usiku, kiongozi wa upinzani bungeni Mhe. Fatma Maghimbi amesema kwamba kanuni za Bunge zinatoa adhabu kwa Mbunge kusimamishwa lau itagundulika kwamba kaongopa. Na kosa hilo huwa zito zaidi inapokuwa anayeongopa ni Waziri katika serikali, ambapo katika nchi zilizoendelea hulazimika kujiuzulu. Kwa mantiki hiyo, Mhe. Maghimbi amesema kwamba, kama alivyoadhibiwa Bw. Augustino Mrema, Mhe. Ali Ameir naye aadhibiwe kama ni kweli kaongopa. Kuacha kutolewa adhabu kwa Mhe. Ali Ameir , amesema Mhe. Fatma Maghimbi ni kujenga jamii ya ‘Animal farm’ ambapo baadhi ya watu huhesabiwa kuwa wa hadhi ya juu zaidi ya wengine. Wakati huo huo, Mama yake Chuki Athumani amedai kwamba kufuatia kauli ya Mhe. Waziri Ali Ameir Bungeni anaogopa kwenda Wizara ya Mambo ya Ndani kufuatilia masuala ya mwanawe. Alisema siku polisi walipomfungua mwanae pingu na serikali kumfutia mashitaka walimwambia akiwa na tatizo lolote kuhusu mwanawe afike Wizarani au awaarifu kwa simu kwa namba ambayo alipewa. Lakini anasema toka itoke kauli inayodai kwamb mwanawe kakutwa na makaratasi ya uchochezi anaogopa kwenda. Juhudi za kumpata Mhe. Waziri Ali Ameir kuzungumzia suala hili hazikuweza
kufanikiwa. Bw.. Mwakilembe ambaye alijitambulisha kama Msaidizi wa Mhe.
Waziri aliliambia AN-NUUR kwa njia ya simu toka Dodoma kwamba Mhe.
Waziri asingeweza kupatikana kutokana na shughuli alizokuwa nazo.
|
Waislamu hawatokubali kusingiziwa
mambo
Serikali ya Sudan yadhamiria kuleta
amani ya kudumu
Mwalimu alaumiwa kuwashawishi watoto
waingie ulokole
Wanawake Arusha watakiwa
kutafuta elimu
Tamsa Tanga yapata viongozi
wapya
Mjue Dr. Abuu Ameena Philips: Mwanaharakati aliyewasilimisha askari 3000 wa Amerika Barua ya Ofisa Elimu ina agenda nyuma
yake
Nabii Isa Mwana wa Maryamu ni Yesu huyo huyo!! Kuanzishwa ‘Islamic Club’ ni ajenda ya siri inayoweza kuhatarisha amani Tanzania Agenda ya siri
Hatua ya Rais kutengua uteuzi wa
Parole ni ya kizalendo
Serikali iwahurumie raia wake
Wanawake Waislamu Wilayani
Masasi waanzisha Jumuiya
Kuhifadhika kwa mwanamke ni kuhifadhika
kwa jamii
Waislamu wekezeni kwenye
kheri -Mwinyi
Biashara ya ufuska yavamia
Z’bar Polisi uchwara’ wanufaika
Asimamishwa uongozi kwa kutoa
fat’wa ya Hitma
Aqswa waazimia kufuata Qur’an
na Sunna
Mashairi - uzawa wa Mtume (S.A.W)
|