|
Na. 050 Jumatano Mei 31 - Juni 5, 2000 |
|
|
|
|
|
Sokoto yaanzisha sheria ya Kiislamu Lagos, NIGERIA JIMBO la Sokoto lililopo Kaskazini mwa Nigeria limeanza rasmi Jumatatu wiki hii kutekeleza sharia za Kiislamu, mwaka mmoja tu baada ya Nigeria kurejea katika mfumo wa demokrasia. Zamfara lilikuwa ni jimbo la kwanza nchini humo mnamo Januari 27, mwaka huu kuanza kutekeleza sharia za Kiislamu licha ya upinzani kutoka kwa Wakristu na serikali ya Shirikisho. Mnamo mwezi Februari, jimbo la Kaduna lilifuata nyayo hizo, ambapo ilitokea mapigano yaliyoacha wahanga zaidi ya 1000 kugharimu uhai. Upinzani kutoka kwa Wakristu wa Nigeria unatarajiwa kuendelea, huku wakidai kuwa sharia ya Kiislamu kutumika kutoka kiwango cha familia hadi ngazi ya Taifa ni ukiukwaji wa katiba. Gavana wa jimbo hilo, Bwana Attahiru Bafawara amewateua mahakimu 43 kuanza kazi katika mahaka zaidi ya 35 jimboni humo. Imeelezwa zaidi kuwa baadhi ya makundi ya jumuiya za Wakristu wanaopenda sharia ya Kiislamu itumike wamekwisha arifiwa juu ya mpango huu wa serikali.
Chechnya yaua askari 66 wa Russia
Moscow, RUSSIA WAPIGANAJI wa Kiislamu wa Chechnya wiki hii wamewaua askari wapatao 66 wa Russia katika mapigano yaliyotokea mara mbili kusini mashariki mwa Chechnya. Msemaji wa wapiganaji wa Chechnya, Bw. Movladi Udugov amesema kuwa mapema siku ya Alhamisi walishambulia ngome ya Russia kijijini Betti-Mokhk ambapo katika mapigano hayo waliwaua askari 46 wa Russia na kuwaacha mashahidi wawili wa Chechnya. Katika shambulio jingine Alhamisi alasiri, lililofanywa na Russia, Wachechen saba waliuawa na askari wa 20 wa Russia kupoteza maisha. Hiyo ilikuwa huko Zhaini-Vedeno. Russia imepinga vikali habari hizo, msemaji wa Rais Vladimir Putin Bwana Sergei Yastrzhemsky alisema huu ni uzushi mtupu. Aliongeza kuwa katika kipindi cha saa 24 ziilzopita askari mmoja tu wa Russia amefariki kutokana na kujeruhiwa vibaya. Amedai zaidi kuwa helikopta za mabomu zilishambulia na kuua askari 12 wa Chechnya siku ya Alhamisi huko wilaya ya shatoi kusini mwa Chechnya. Umoja wa Ulaya unaotarajiwa kuzungumzia suala la Chechnya siku ya Jumatatu katika mkutano kati yake na Russia, Bwana Javier Solona, Mkuu wa Usalama na masuala ya nje ya Umoja wa Mataifa alisema. Russia iliivamia Chechnya mnamo Oktoba Mosi mwaka jana kwa lengo la kutaka kutawala.
Ethiopia, Eritrea zaanza mazungumzo
Algiers, ALGERIA MAJIRANI wa pembe ya Afrika, Ethiopia na Eritrea zimeanza hapo jana mazungomzo katika kutatua mgogoro wa mpaka katika vita vilivyodumu miaka miwili sasa. "Waziri wa sheria wa Algeria Bwana Ahmed Ovyalia alianzisha mazungumzo katika mkutano kati yake na ujumbe wa Ethiopia ulioongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ethiopia Bwana Seyeum Mesfin", alisema ofisa mwandamizi wa Algeria. Ujumbe wa Eritrea unaoongozwa na Waziri wa mambo ya nje Bwana Haile Woldensal. Mazungumzo hayo yanasimamiwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Nchi Huru barani Afrika (OAU) Bwana Abdelaziz Boutelfika wa Algeria. Bila kutaja ajenda za mkutano afisa mmoja wa Algeria amesema kuwa kati ya siku tatu hadi nne mazungumzo yatamalizika. Ethiopia imesema kuwa imeyaondoa majeshi yake kutoka magharibi mwa Eritrea hapo jana ambapo imedai kuwa imewaua, kuwazingira na kuwakamata mateka askari wa Eritrea katika kampeni yake hiyo iliyodai kuwa ilikuwa na lengo la kudhoofisha nguvu za adui za kivita na kuikomboa ardhi. Msemaji wa Eritrea Bwana Ymane Gebremeskei amesema, bado anatafuta uhakika wa kujitoa kwa Ethiopia. Katikati ya uwanja wa vita inasadikiwa Ethiopia imerudishwa nyuma zaidi ya maili 60 na askari wa Eritrea.
Clinton ziarani Ulaya
Lisbon, URENO RAIS Bill Clinton wa Marekani hapo jana ameanza ziara itakayomchukua katika nchi kadhaa za bara za Ulaya. Baada ya kuwasili mjini Lisbon, Rais huyo alikuwa na mazungumzo na viongozi wa Ureno katika masuala yanayohusu silaha na hali ya utulivu barani Ulaya pamoja na utafiti wa dawa ya ukimwi. Katika ziara, Rais huyo anatarajiwa kuvishwa nishani na umoja wa Ulaya ya Amani, kutokana na mchango wake wa kuleta amani katika migogoro ya Bosnia, Kosovo na Balkan. Nchi nyingine anazotarajiwa kuzuru ni Ujerumani, Russia, Ukraine na Ireland ya kaskazini. Clinton anatarajiwa kuwasili kesho nchini Ujerumani ambapo licha ya kuvishwa nishani atakuwa na mazungumzo na mwenyeji wake Kansela Gehard Schroeder. Hii ni ziara ya 70 tangu ashike madaraka ya Urais takriban miaka saba na nusu hivi sasa, ambapo anatarajia kumaliza wadhifa huo mnamo mwezi Januari mwaka ujao, baada ya kutumika vipindi viwili vya miaka minne minne. Akiwa Ujerumani atakutana na waziri mkuu wa Israel Bwana Ehud Barak kuzungumzia suala la amani ya mashariki ya kati, mazungumzo ambayo yalisitishwa wiki moja kabla baada ya kutokea mapigano ukanda wa Gaza. Maudhui ya safari ya Bwana Clinton ni kuimarisha masuala ya biashara na usalama. Nchini Russia atakutana na Rais Vladimir Putin
na kumalizia ziara yake hiyo ya wiki moja kwa kusimama muda mfupi nchini
Ukraine.
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Zanzibar wadai kuyumbishwa na Bara Serikali yatoa muelekeo wa Bajeti na kutangaza njaa Habari za ndani
SMZ haishughulikii mikarafuu -Maalim Seif Mwalimu Mkuu Msimbazi Mseto atishia kujiuzulu Hizi ni 'arobaini' za mapandikizi Waislamu Mbeya wamsusa Sheikh Mkuu wa BAKWATA Masheikh wa BAKWATA waongoza sherehe za kuwasimika makamanda wa vijana wa CCM MAKALA
Makala
MPASHO NASAHA
Kalamu ya Mwandishi
MAKALA
Habari za Kimataifaza Kimataifa Lishe
RIWAYA
Ambari, Mwakipesile wajitosa kugombea DRFA |
|
|
|
|