|
Na. 049 Jumatano Mei 24 - 30, 2000 |
|
|
|
|
|
Wenye mamlaka ya kumuweka mtu Ikulu ni wananchi
Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Mhe. Seif Shariff Hamad amewataka viongozi wa CCM kufahamu kuwa wananchi ndio wenye uwezo na mamlaka ya kumuweka madarakani mtu na chama wanachokitaka wao na si vinginevyo. Maalim Seif aliyasema hayo Mei 21, mwaka huu katika viwanja vya Malindi mjini Zanzibar alipokuwa akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara wa chama chake. Kauli hiyo ya Katibu Mkuu wa CUF ambaye anatarajiwa kuwa mgombea pekee wa chama hicho wa kiti cha Urais wa Zanzibar imekuja kufuatia kauli ya Mwenyekiti wa CCM Mhe. Benjamin William Mkapa kuwa hawatakiachia chama kisicho na ridhaa ya ASP na TANU kuiongoza Tanzania. Chama cha Mpinduzi kilizaliwa mwaka 1977 kwa kuunganisha vyama vya TANU na ASP. Maalim Seif alisema kuwa sheria iliyoanzisha mfumo wa vyama vingi vya siasa inataka chama kisiwe na mafungamano na vyama vya zamani, lakini kwa mshangao Mwenyekiti wa CCM anatamka hadharani kauli inayokwenda kinyume na sheria hiyo wakati wao ndio walioipitisha. "Ni nani huyo hasa ambaye wananchi wakishaamua kuiweka CUF madarakani atazuia", aliuliza Maalim Seif na kuongeza kuwa hakuna mamlaka inayozidi maamuzi ya wananchi, kwani wao ndio wenye maamuzi ya mwisho. Aliwatanabanisha Wazanzibari kuwa macho na kukataa Rais wa kupendekezwa na Bara kwani mara nyingi huwa wanatekeleza kila jambo linaloamuliwa hata kama halina manufaa kwa Zanzibar. "Analotaka Bw. Mkapa ni mumchague mtu ambaye lolote litakalofanywa Zanzibar asema ‘hewala bwana....’, ndio maana akasema nitawaleteeni kijana mzuri", alisema Maalim Seif. Akizitaja sababu zilizopelekea yeye kutohudhuria sherehe za Muungano zilizofanyika Uwanja wa Taifa hapa Jijini Aprili 26, mwaka huu, Maalim Seif alisema kuwa yeye kama kiongozi wa wananchi wa Zanzibar isingekuwa vyema kwake kuhudhuria sherehe hizo wakati wanachi Zanzibar wanapigwa na kuteswa na polisi wa muungano. "Siwezi kukaa meza moja na mtesaji wakati wananchi wanateswa", alisema Katibu Mkuu huyo wa CUF. Akizungumzia mwafaka visiwani humo, Maalim Seif alisema kuwa shutuma zote zinazotolewa na CCM juu ya CUF kuhusu suala la utekelezaji wake ni uzushi na kwamba hazina msingi wowote kwani CUF imetekeleza kikamilifu vipengele vyote vya mwafaka kama vile kumtambua Rais wa Zanzibar pamoja na serikali yake na pia wawakilishi wa CUF kuhudhuria katika Baraza la Wawakilishi. Isipokuwa wanaokwamisha utekelezaji wa mwafaka huo ni CCM. Aidha, Maalim Seif aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi wakati wa uandikishaji na hatimaye kuzitumia vyema kura zao ili kuleta mabadiliko ya kisiasa Visiwani humo. Alisema Zanzibar inahitaji mabadiliko na uongozi utakaoondoa aina zote za mtengano katika jamii. Ili kufanikisha hilo, Maalim Seif alisema kuwa "Rais wa CUF" atakayeshika madaraka ataunda serikali ya Umoja wa Kitaifa ili kila mtu ajihisi ni serikali yake. Mkutano huo pia ulihudhuriwa na
viongozi wengine wa wa CUF wakiwemo Makamu Mwenyekiti Shaaban Mloo, Katibu
wa Kuratibu Mwafaka kwa upande wa CUF,Bw. Abdulraham Muhammad Dedes.
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Chuo Kikuu Dar wafanya mitihani katika Bwalo la chakula Udini wa CCM utaisambaratisha nchi -Tambwe ‘Kutoweka’ kanda ya Kakobe: CCM yatuhumiwa Maalim Seif awaambia Wazanzibari: Wenye mamlaka ya kumuweka mtu Ikulu ni wananchi Mkapa afurahia maendeleo Pwani ‘Zawadi’ ya Uchaguzi yatishia kusambaratisha taasisi ya Kiislam Tanga Serikali yakemea mwanamke kudhalilishwa Ushauri Nasaha
MAKALA
Makala
Kalamu ya Mwandishi
MAKALA
Makala
Makala
RIWAYA
Lishe
|
|
|
|
|