|
Na.164 Jamada Awal 1419, Agosti 28 - Septemba 3, 1998 |
|
Na Suleiman Simba, Kigoma MSIKITI wa Wagoma mjini hapa umepata viongozi wapya baada ya kufanyika uchaguzi Jumapili ya Agosti 23, 1998. Waliochaguliwa kushika uongozi wa Msikiti huo ni Bw. Isa aliyeshika nafasi ya Uenyekiti, Sheikh Ibrahim Misango (Imamu) na Sheikh Hemed Shaaban Babadudu ambaye anakuwa naibu Imamu. Wajumbe wengine waliochaguliwa wametajwa kuwa ni Bw. Saliboko Abas Mrombo, Amrani Mrombo, Hemed Id pamoja na kuwa mjumbe pia ameshika nafasi ya unaibu Katibu. Baadhi ya waumini walioshiriki uchaguzi huo wamesema wamefurahishwa
na jinsi uchaguzi huo ulivyoendeshwa hadi matokeo na wanamatarajio makubwa
kwa viongozi hao kuwa huenda wakawa chemchem ya maendeleo ya Msikiti huo
na waumini wake.
- Vitabu vinne vya Mungu vyahubiriwa
Na Said Shariff MUHADHARA wa kwanza wa Kiislamu umefanyika hivi karibuni baada ya mihadhara hiyo kukwama kufanyika kwa kipindi cha zaidi ya miezi sita kufuatia Polisi kuvamia Msikiti wa Mwembechai ambapo Waislamu kadhaa waliuawa. Muhadhara huo ambao ulifanyika Masjid Hijaz Kigogo Mwisho njia panda Jijini, kwa muda wa wiki mbili kuanzia Agosti 4, 1998 uliwajumuisha wahadhiri kutoka vikundi vya Khidamat Da’awaat Al-Islamiya na Al-Mallid International Propagation Centre. Vitabu vinne vya Mwenyezi Mungu, Zaburi, Torati, Injili na Qur’an vilihubiriwa katika muhadhara huo ambapo wahadhiri walitoa mada mbalimbali. Kulikuwa na vipindi vya maswali na kujibiwa kwa kutumia maandiko (aya) matakatifu ya Allah (sw). Wakristo wanne waripotiwa kuingia Uislamu kufuatia muhadhara huo. Wakati huo huo, wazazi Waislamu wa Kibamba wamelalamika kwamba watoto wao katika shule za msingi wamekuwa wakigawiwa Biblia. Wamedai kwamba wamewaona walimu wakuu wa shule husika hata hivyo wamedai kwamba hawajui lolote. Walimu hao wakuu wamesema kwamba wamegundua kwamba wapo waalimu binafsi
ambao huwashawishi watoto na kuwapa Biblia wasome, kwani ni neno la Mungu.
Na Ashraf Yusuph, Moshi WAISLAMU mjini Moshi wamehimizwa kuitumia Misikiti katika kuendeleza na kuilinda jamii ya Kiislamu. Hayo yamesemwa na Sheikh Ramadhani Hamza katika khutba ya sala ya Ijumaa katika ufunguzi wa Msikiti wa Al-Haramain Islamic Foundation hapo hivi karibuni ikiwa ni sehemu ya khutba na shukrani kwa wale wote walioamini kweli kweli, na shukrani kwa wadhamini wa Msikiti huo Al-Haramain Islamic Foundation. Akinukuu aya za Qur’an na tafsiri zake, Sheikh Ramadhani alisema, "hakika Misikiti ni mali ya Mwenyezi Mungu" (ingawa wajengaji na watu). Hivyo pasiwepo na dhana au fikra kuwa Misikiti ni mali ya mtu au watu fulani. Aliendelea Sheikh huyo kuwa pamoja ardhi yote kuwa ni Msikiti bado Mtume (saw) alipohamia Madina kutoka Makka kitu cha kwanza kufanya alijenga Msikiti ili iwe ni kituo cha harakati za Kiislamu. Sheikh Ramadhani alionya juu ya imani potofu kwa baadhi ya waumini kusema kuwa Misikiti ni mali ya watu au dhehebu fulani, hiyo inapelekea kuwafarakanisha Waislamu badala ya kuwaunganisha. Sheikh Ramadhani alihitimisha khutba ya Ijumaa kwa kuwakaribisha waumini wote wa Kiislamu kuja kufanya ibada na kusoma katika Madrasa ya Al-Haramain bila woga wala kujali itikadi zao. Msikiti huo wa Al-Haramain ni mmoja kati ya Misikiti mizuri na mikubwa katika mji wa Moshi, upo sehemu ya Njoro-Railways. Kutokana na ukubwa wa Msikiti huo pamoja na madrasa iliyojengwa baadhi ya waumini wa mji wa Moshi Majengo na Njoro wameonyesha matumaini yao kuwa Masjid Al-Haramain ni kituo cha elimu na maendeleo ya Waislamu wa Moshi mjini na nchi nzima kwa ujumla. Sheikh Ramadhani ni muasisi wa Madrasa maarufu hapa Mji Mpya Njoro na Moshi mjini ambayo inaongoza kwa kutoa taaluma zote za dini, inayojulikana kama Madrasat Iyahudiin. Msikiti wa Al-Haramain utatoa fursa kwa Waislamu wa Moshi Mjini, Majengo na Njoro wenye uchu wa elimu ya dini kuchota elimu kwa mwanazuoni Sheikh Ramadhani Hamza ambaye ndiye Imamu mkuu na Amir wa Msikiti huo. Wakati huo huo, vijana wa Kiislamu Majengo Moshi wameanzisha jumuiya yao kwa lengo la kuleta umoja na mshikamano baina yao. Vijana hao wameazimia kufuata Qur’an na Sunna ya Mtume (saw) katika maisha yao ya kila siku. Aidha, vijana hao wameazimia kushirkiana katika mambo ya harusi, maradhi pamoja na vifo ili kuondoa tofauti baina yao kiitikadi. Vijana hao wamejiwekea mikakati kabambe kama vile michango maalum ya kila mwezi ili baadaye kuweza kutumika katika masuala mbalimbali ya Uislamu na umoja huo. Wameazimia kuanzisha miradi mbalimbali ili kuweza kupata fedha za kuendesha umoja huo pale mipango itakapokamilika. Na Mwandishi Wetu WANAWAKE wametakiwa kuchukua hadhari kubwa dhidi ya kampeni zinazoendelea za kudhibiti uzazi kwani huenda zikawaletea maangamizi makubwa. Imeelezwa kwamba madawa kemikali na njia mbalimbali zinazotumika kuzuia mwenendo wa kawaida (maumbile) wa mwili kibaolojia; imekuwa ndio sababu kubwa ya matatizo mengi yanayowasibu kina mama sasa hivi. Matatizo hayo ni pamoja na kansa katika sehemu za uzazi, shinikizo la damu na matatizo mbalimbali yahusuyo hali za wanawake. Akiwasilisha mada katika hafla ya kuwaaga wanachuo wa M.C.H Same hivi karibuni, mshiriki mmoja Mama Kiseto alisema kwamba mbali na matatizo hayo ya kiafya yapo matatizo makubwa ya kijamii ambapo huenda jamii ikafika mahali ikakosa nguvu kazi. Aidha, kwa kutojua mambo ya ghaibu mara nyingi wazazi hujuta kwa ukiwa baada ya kukosa wa kuwalea au kuwafariji kwasababu mtoto mmoja au wawili waliowategemea waweza kufa au kuharibikiwa kimaisha. Mama Kiseto ambaye ni Mwalimu wa shule ya msingi Chalao Mlimani, Same alisisitiza kwamba mbali ya kuwa kuacha kuzaa kwa kuchelea hali ya maisha ni kuingilia milki ya Mwenyezi Mungu, lakini pia ni mpango ambao hatima yake ni kumuangamiza mwanadamu mwenyewe. Akizungumzia suala la mahari, Mama Kiseto alisema kwamba mahari ni zawadi na sio bei na hivyo sio lazima iwe fedha au ng’ombe, mbuzi n.k. Aidha, amesema kwamba kwa mujibu wa Qur’an apewaye mahari ni yule anayeolewa na kwa hivyo basi yeye ndiye anayepanga kiwango cha mahari. Kwa hiyo akasema si haki na wala si katika sheria ya Allah wazazi kuwapangia mahari mabinti zao kulingana na rangi, sura au elimu. Kwa upande mwingine, mama Kiseto ameyataka mashirika na taasisi zinazodai kupigania haki za wanawake ziangalie hali inayokubuhu ya kudhalilishwa wanawake kupitia matangazo ya biashara, uvaaji nguo fupi na kujichubua ngozi pamoja na kupungua kasi ya ndoa huku ufuska ukiongezeka. Mama Kiseto alisisitiza kwamba haki na heshima ya wanawake hupatikana katika Uislamu na wala si mila, desturi na kampeni zilizo nje ya Uislamu. Kati ya wahitimu 36 wa M.C.H. Same, kwa mwaka huu 1998, 9 tu ndio Waislamu. Pamoja na uchache wao wahitimu hao Waislamu waliandaa hafla kubwa ya kuagana na wenzao. Katika hafla hiyo ilisomwa Maulid Nabii, ambapo mada mbalimbali zilitolewa
|
TAHARIRI: Dawa ya ugaidi si kufanya ugaidi ndani ya ugaidi Bakwata yalaani ubabe wa Marekani
Wanakijiji wawapiga Polisi
Olesiva
Waislamu washinda kesi Same
Wasafiri ATC wadai ndege ya Jeddah
inahujumiwa
Mahojiano kati ya CNN na Bwana Usama bin Ladin Historia ya damu za mashujaa Afghanistan Msikiti wa Wagoma Kigoma wapata
viongozi wapya
Muhadhara wanguruma Masjid
Hijaz
Waislamu waitumie Misikiti
ipasavyo
Mpango wa kudhibiti uzazi utawaangamiza
wengi
Hoja za kutofautisha Yesu na Issa
ni udhaifu, ni uzushi mtupu! - 3
Wanawake wa Kiislamu washiriki
maonyesho ya kilimo
Wanawake wa Kiislamu washauriwa
kupigania haki zao
Africa Muslims Agency: Inavyohudumia
jamii
Kitengo cha Zakkah chasafirisha wanafunzi
Kupinga kifo cha Yesu ni kumpinga
Mungu?
Zanzibar na biashara ya utumwa
Marekani ishitakiwe
MAPENDEKEZO YA KATIBA YA SHIRIKISHO LA TANZANIA - 3
|
Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua kwa: webmaster@islamtanzania.org