|
Na. 042 Jumatano Aprili 5 - 11, 2000 |
|
|
|
|
|
Kufuatia washabiki kumzomea:
KATIKA hatua ambayo ni ya kawaida mmiliki wa timu ya Kajumulo World Soccer Alex Kajumulo ametishia kuinyang'anya klabu ya Simba ya Dar es Salaam kocha ambaye amewaazima kwa mwezi mmoja. Abdallah King Kibadeni aliruhusiwa na Kajumulo kuisuka timu ya Simba baada ya Nzoyisaba Tauzany kuzuiliwa na Idara ya Uhamiaji kutokana na kutokuwa na kibali cha kufanya kazi nchini. Kajumulo ametoa tishio hilo kufuatia washabiki wanaoaminika kuwa wa klabu ya Yanga kumzomea alipokuwa akiteta na mwamuzi wa akiba katika pambano la timu yake na Bandari Mtwara. Pambalo hilo lilipigwa uwanja wa Taifa Jijini Jumapili iliyopita katika michuano ya awali ya ligi kuu Tanzania Bara lililomalizika kwa Bandari kufungwa 2-0. Wakati akizungumza na mwamuzi wa akbia ambaye hata hivyo jina lake halikupatikana mara moja zilisikika sauti kali toka jukwaa la kijani zenye ujumbe wa rushwa, rushwa. Kufuatia ujumbe huo, Kajumulo aligeuka na kusema ... "kama mnanizomea nitawanyang'anya kocha wangu", aliwaambia washabiki wa Simba ambao nao mara moja walimjibu. "Sio sisi ni hao Yanga". Walisikika na kumfanya Kajumulo akae kwenye benchi la timu yake. Hata hivyo, haikuweza kufahamika mapema kama aliridhika na majibu hayo. Waliofuatilia kwa makini mazungumzo ya Kajumulo na refa wa akiba yaliyofanyika wakati wa mapumziko wamelithitishia NASAHA kuwa alikuwa akilalamikia uamuzi mbaya katika mchezo huo. Hata hivyo, mara ngwe ya pili ilipoanza timu ya Kajumulo ilipata peneti iliyofungwa kwa ustadi na beki George Masatu baada ya Madaraka Suleiman kuangushwa ndani ya eneo la hatari.
Kipukuswa kufuata nyayo za 'Mgosi' Hazali Na Mwandishi Wetu ABDALLAH Kipukuswa, Kaimu Mwenyekiti wa klabu ya Simba ya jijini anayegombea nafasi ya Uenyekiti wa klabu hiyo amedai kufuata nyayo za mtangulizi wake Yusufu Hazali. Endapo wana Simba watamridhia kukalia kiti hicho amesema atafanya mazuri yote yaliyofanywa na Hazali na kusahihisha kasoro ndogo ndogo zilizojitokeza wakati huo. Kipukuswa amejigamba kuchukua nafasi hiyo katika uchaguzi utakaofanyika Jumapili ijayo kwa kuzingatia utendaji wake mzuri wakati akiwa Makamu na Kaimu Mwenyekiti. Jumla ya wanachama 23 walikuwa wamechukua fomu za kugombea uongozi, miongoni mwao watatu wakipigania Uenyekiti na Ukatibu.
Hazali sio Yanga ni Simba 'kindakindaki' Na Mwandishi Wetu ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Klabu ya Simba ya Jijini, Hazali amesema jana habari hizo zililenga kuwapotosha wana Msimbazi na Watanzania kuhusu mapenzi yake kwa Simba. "Habari hizo kwa kweli sio sahihi hata kidogo na zilisemwa kwa lengo la kunivunjia heshima na kunigombanisha na wana Simba wenzangu", amesema. Katika habari zilizotolewa na gazeti hili wiki mbili zilizopita ilidaiwa kuwa Hazali hana mapenzi na klabu ya Simba bali Yanga. Kufuatia uchunguzi uliofanywa na NASAHA kwa karibu wiki mbili sasa imebainika kuwa habari zilizodai kuwa 'Hazali ni Yanga damu' hazikuwa sahihi na hazikutolewa kwa nia njema. Kadhalika wanachama kadhaa wa klabu ya Simba waliongea kwa nyakati na gazeti hili wamethibitisha kuwa Hazali ni miongoni mwa wanamsimbazi wachache wenye mapenzi ya dhati na Simba. "Na kwa kweli Hazali sio mwanachama na mpenzi wa hivi hivi tu, ni Simba watoka nitoke ambaye amekuwa ndani ya Simba kwa miaka dahari iliyopita", amedai mwanamsimbazi mwingine ambaye ni wa makamo. Kwa sasa Hazali anatumikia adhabu ya mwaka mmoja aliyopewa na Msajili wa Vilabu na Vyama vya michezo nchini Leonard Thadeo kwa madai ya uongozi mbaya.
Na Mwandishi Wetu KOCHA Mkuu wa klabu ya Kariakoo ya Lindi, Salum Madadi amezionya timu zinazoshiriki ligi kuu Tanzania Bara kuwa zisitarajie kupata mteremko hata kidogo mbele ya timu yake. Ametoa onyo hilo mwanzoni mwa wiki hii Jijini katika mazungumzo na mwandishi wa habari hizi muda mfupi kabla ya kuelekea mkoani Lindi kwa maandalizi zaidi. "Kimsingi timu yangu ni nzuri, kwa sababu tumefanya usajili mzuri na tumejiandaa kiasi cha kutosha kwa hiyo timu pinzani zisitegemee kupata mteremko kutoka kwetu", amesema. Kadhalika, amezitaka timu pinzani kuachana na porojo za kuupotosha umma kama zilivyofanya mwaka jana kuwa Lindi kuna uzalendo kiasi cha kupindisha sheria 17 za soka kwa nia ya kuinufaisha timu ya Kariakoo. Katika mchezo wa fungua dimba Kariakoo ilitoka sare ya 1-1 na Reli ya Morogoro, mchezo uliochezwa mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki. Reli walilazimisha bao dakika ya 89 ya mchezo kupitia kwa Samwel Msuku. |
YALIYOMO
Tahariri
Mbukuzi
anguruma Chuo Kikuu:
Kuelekea
uchaguzi mkuu 2000:
Maalim Seif afunguliwa mashitaka ‘Tume ya Keenja’ haikufanya ilichoagizwa - Wananchi MPASHO NASAHA
Ushauri Nasaha
MAKALA
WAZO LA WIKI
MAKALA
Kalamu ya Mwandishi
Makala
MAKALA
Riwaya
Lishe
Madadi azionya timu za Ligi Kuu |
|
|
|
|