|
Na. 036 Jumatano Februari 23 - 29, 2000 |
|
|
|
|
|
Ulimbukeni wa siku ya Valentino Na Abu Halima Sa Changwa WIKI iliyopita kuna watu walikuwa katika mashamsham ya siku ya Valentino ambayo imebatizwa jina la "siku yawapendanao". Siku hii iliwekwa na watu fulani kwa ajili ya kumkumbuka ya mtu mmoja kwa jina la Mtakatifu Valentino, ambaye aliuawa kwa kukiuka matakwa ya watawala wa wakati wake, kwa sababu alikemea baadhi ya mila zao na akawa anafungisha ndoa zilizopigwa marufuku katika wakati huo. Pengine walioiweka siku hii walikuwa na maana nzuri kabisa. Tatizo ni kwamba siku hizi zimepewa tafsiri na matumizi tofauti na baadhi ya watu ambao huzipapatikia. Watu wengi huzipa siku matumizi kwa jinsi wanavyoona wao. Kwa mfano, kuna siku huwa zinaitwa za "vunja jungu" ambazo ziko kabla ya kuanza mfungo wa Mwezi wa Ramadhani na baada ya kufunga. Siku ya kwanza huchukuliwa na wachafuzi wa siku za watu kama ni siku ya kuyaaga maasi kwa kuyazamia kisawasawa, na siku za baada ya kufunga Ramadhani huchukuliwa kama siku ya kulipiza kisasi kwa kuogelea tena katika mambo maovu. Hadithi ni hiyo hiyo kwa siku ya Valentino. Nilikuwa nasikiliza redio moja ya hapa nchini. Watangazaji wawili, mmoja mwanume na mwingine mwanamke, walikuwa wakipigia debe siku hii ya Valentino, ambayo ni ngeni mno miongoni mwa Watanzania wengi. Watu wengi waliokuwa wakiwasiliana na watangazaji hawa kwa simu walionesha kuelewa kwamba wapendanao ni wale wenye mahusiano ya kijinsia, au ya boyfriend na girlfriend,(kwa lugha ya mpasho NASAHA tunamwita kila mmoja wa mzinifu mwenza). Watangazaji wale nao walishinikiza dhana hii kwa kuwaambia "wapendanao" hawa yanayofanywa wakati wa siku hizi hapa kwetu, nayo ni kwenda beach kupunga upepo kama Wazungu, au kwenda kwenye majumba yanayoitwa ya starehe. Kilichoniboa zaidi mimi ni vile wale watangazaji walivyokuwa wakiongea, hasa ukizingatia mmoja alikuwa dume mwingine jike. Walikuwa wakiongea katika hali ya kuamsha hisia fulani miongonni mwa wasikilizaji wao, na nihisia hizo hizo za "uzinifu wenza",. Kwa lugha ya ki-mpasho nasaha, walikuwa wanamisanya misanya (kumisanya ni kuongea upuuzi au mambo yasiyo na faida na jamii). Hii halikunishangaza sana kwa sababu nafahamu kwamba jamii yetu imefikia hatua kwamba upuuzi ndio umekuwa na bei zaidi kulikou ungwana. Ukitaka kuwa maarufu hapa kwetu usiwe mwanafalsafa (Philosopher), kuwa mtu wa kumisanya misanya, hapo wewe ndio utakuwa mtu wa millennium mpya. Wanafalsafa kwa jamii yetu wana tatizo la Y2K. Hawafai kuwepo. Sasa hivi, gazeti linaloandika masuala muhimu ya kijamii linakuwa halina bei, kwa sababu upuuzi ndio umekuwa fasheni, kwa vile sehemu kubwa ya jamii ni wapuuzi. Imefikia sasa hivi watu wanaenda na upuuzi, kwa vile wapuuzi wengi ndio wanunuzi, basi hata wasomi inabidi waandike au waongee upuuzi ili makala zao au maongezi yao yawavutie wengi, na ndio maana magazeti ya manyang'unyang'u sasa hivi yanauzwa zaidi ya magazeti ya masuala ya kuijenga jamii. Wazungu wana methali yao inayosema, "Where ignorance is bliss, 'tis folly to be wise", yaani, mahala ambapo ujinga unachukuliwa kama ni baraka, ni upambavu kuwa na busara. Kama huamini maneno yangu, andika mazazeti mawili, moja ulipe kichwa cha habari; Mkuu wa mkoa apania kutokomeza ujambazi. Halafu jingine uandike; Mkuu wa mkoa alewa hadi kujisaidia kwenye nguo; halafu uone ni gazeti lipi litapendwa na kununuliwa zaidi, na kuwa ndio gumzo la wabongo walio wengi. Nikiacha magazeti, kuna vituo vingi vya redio vilivyoanzishwa ambavyo havifanyi lolote zaidi yakumisanya. Ndio hivi hivi vinavyo saidia katika kupotosha maana ya siku za watu. Ramadhani ikikaribia kwisha basi kutwa kitatangaza vunjajungu huku, vunjajungu kule. Ndio hivi vimekazania kuiingiza hii siku kuu ya watu, ya Wakristo, na kuipa picha ya "kupendana" kwa wazinifu wenza. Ukichungza kwa makini utakuta kwamba siku ya Valentino imekuwa ni kinyume tu cha Siku ya Ukiwmi Duniani. Katika Siku ya Ukimwi Duniani, watu hutafakari jinsi ya kupambana na gonjwa baya la zinaa lililokumba dunia. Redio na magazeti ya maana duniani hushiriki katika kuhamasisha mapambano dhidi ya ukimwi. Kinyume chake, Valentine Day imekuwa ni siku ya kuwashawishi watu siku hiyo "wapendane" zaidi. Basi kila mtu siku hiyo atahakikisha haipiti bila ya "kupenda". Redio na magazeti ya ovyo siku hiyo ndiyo yatapata fursa. Waandishi na watangazaji watamisanya kutwa, na kuandika na kutangaza mambo ya ovyo, yasiyofaidisha jamii kwa lolote. Hata kama ni entertainment, basi ndiyo iwe siku nzima mna misanya tu, hamna la maana? Halafu suala ni kwamba, kwangu mimi, kama Valentine Day nisiku ya wapendanao, basi kila siku kwangu ni Valentine, kwa sababu sitangojea siku yakupangiwa kumpenda nimpendaye, yaani mke wangu. Nyie wenye kupendana siku moja yakupangiwa hebu nielezeni mimi ambaye kila kukicha Ummu Halima namuona mpya, siku ya Valentine nifanyeje? |
YALIYOMO
Tahariri:
‘CUF tumejiandaa kuchukua serikali' Suala la Mwembechai lazua mtafaruku Mabadiliko ya katiba ya Zanzibar: CCM Z'bar ina nafasi ya ushindi MPASHO
NASAHA
Habari
za ndani
Ushauri
Nasaha
MAKALA
WAZO
LA WIKI
Makala
ya Kimataifa
Kalamu
ya Mwandishi
MAKALA
LISHE
|
|
|
|
|