AN-NUUR 
Na.185 Shawwal 1419, Januari 29 - Februari 4 , 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Mashairi
 

Miaka 37 ya uhuru, lakini mhh! 

Naanza kwa kumtaja, Mola aliye Karima, 
Duniani amejaa, kwa zake nyingi rehema, 
Sifa hii haikuja, bali kwa zake hekima, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Hodi hodi gazetini, Mhariri nimekujua, 
Maswali yamenihini, majibu sijayajua, 
Sikizeni kwa makini, malenga mtayajua, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Neno lanishangaza, siku nyingi nimewaza, 
Bali leo nauliza, kitu hiki chanikwaza, 
Mabangoni wamejaza, uhuru kuutangaza, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Muda mwingi umetimu, leo inaadhimishwa, 
Tatu saba imetimu, ukoloni kuhamishwa, 
Imekatika misimu, wananchi tumechoshwa, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Zimekithiri nchini, kero zimetapakaa, 
Ofisini na shuleni, huduma za kubagua, 
Uhuru huu ni nini, leo washeherekea, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Wananchi wateseka, hujuma zimeenea, 
Nzasa wanasikitika, ukimbizi wahofia, 
Bagamoyo na Tandika, matunda wayazuia, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Watu wengi wateseka, huduma zilivyo duni, 
Viongozi waneemeka, hawatekelezi ilani, 
Kodi nayo waitaka, matunda hatuyaoni, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Islamu tunalia, uonevu umezidi, 
Chuki anaangamia, Salehe kama shahidi, 
Sote tunashuhudia, imetoweka ahadi, 
 Uhudu wa Tanzania, maana siitambui! 

Uhuru huu wa nani, ndugu nisaidieni, 
Ni wa Anna ama Johni, jibu nibainishia, 
Nimechunguza makini, uhuru huo sioni, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Kadi tama kituoni, wenzangu nawaachia, 
Jibu nisaidieni, bado  nasisitizia, 
Nami niwe shereheni, uhuru nikitambua, 
Uhuru wa Tanzania, maana siitambui! 

Fatma H. Mkombozi, 
Jangwani High School, 
Dar es Salaam. 



Mola wasitiri 

Rabi Mola wasitiri, viumbe walofariki, 
Waondolee shubiri, hiyo siku ya hilaki, 
Uwaepushie shari, na adhabu za makuki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Maombi yetu Ghafuri, twaomba uyaafiki, 
Vifo vimetuathiri, hiki baada ya hiki, 
Nyoyo zimetahayari, huzuni kutamalaki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Vimetutia dosari, hali hatuzimiliki, 
Idadi naikariri, watatu walohiliki, 
Mwanavita ya Bakari, mauti kumdiriki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Wa pili yake nambari, alefuata twariki, 
Abdallah mashuhuri, mwadini ndie atiki, 
wa tatu namuhubiri, alepambana na dhiki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Mamepuju jamadari, maradhi yalimsaki, 
Hali ikawa dhahiri, mwili kuwa kititiki, 
Juhudi za daktari, nduli kaziona feki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Wote hawa majasiri, mwadini alishiriki, 
Kawazaa kwa uzuri, malezi yalibariki, 
Idadi naisitiri, kuibaini si haki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Kigombe yao bandari, kwengine hawahusiki, 
Walidumu kwa fahari, bila kuwa mamluki, 
Kizazi kilishamiri, kufikia halaiki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Mwazema fukolaari, Kigombe hawashikiki, 
Kwa wingi na uhodari, na mali kutowadhiki, 
Mola kawajaza mori, kutafuta hawachoki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Dua ni kwake Jabari, tumuombe mwenye haki, 
Awaepushe na shari, humo ndani ya handaki, 
Uwape sitighifari, pepo isiwadhihaki, 
Harufu zitamalaki, bustani za kaburi. 

Ally Mwazema Saidi (Nyenga), 
P.O. Box 2112, 
Tanga. 
Upinzani dhidi ya 

Juu 
 

YALIYOMO 
  

Tahari 
Kama hakuna haki watu watachukua sheria mkononi 

Kupokelewa kwa malalamiko ya Waislamu: Masheikh wasubiri ukweli wa Mkapa 

Afariki baada ya kutokwa damu nyingi: Yadaiwa hakuwa na sh. 4,000 

Nyumba ya Wakfu iliyoporwa yarejeshwa 

Kamanda Gewe atakiwa amkamate Daniel 

Sheikh awasambaratisha walevi Liwale 

Msikiti wavamiwa na kuvunjwa milango, madirisha 

Mjue Usama bin Ladin -2 

Msikiti wa Mwinyimkuu wafanya sensa 

Njaa hakuna, tunategemea kula silaha 

Parole kwa mbinde! 

Mabaraza yawatetee Waislamu - Sheikh Bafadhil 

Hali ya Uislamu Lukulunge, Kongwa inatisha 

Waislamu Kondoa waagizwa kuyatunza magazeti ya ANNUUR 

I.P.C yatakiwa kujitangaza 

Kutoka magazeti ya zamani 

Sabato ni ya Waisraeli, Mungu alikwishaiondoa 
Na Muhibu Said 

Waislamu wachoma moto nguruwe 

Tume ya kubadili Katiba Kenya: Waislamu kuwakilishwa 

Waislamu Msonge waomba wanusuriwe 

Sayansi na Teknolojia 
[PELEKA FAX NCHI ZA NG’AMBO BURE! – (2)] 

Masomo ya Kiislam 

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na Lishe 
[Mwongozo wa mlo wa kila siku] 
 
 


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita