|
|
|
TOKA Mh. Rais Mkapa aingie madarakani amekuwa akikariri kwamba serikali yake itakuwa ya haki inayopiga vita rushwa; uonevu na upandeleo. Aidha, akiwa mgeni rasmi katika Baraza la Eid el Fitr hivi karibuni Mh. Rais Benjamin William Mkapa alisisitiza kwamba serikali yake haipo tayari kuona watu wanaonewa kwa ajili ya dini yao, kabila au sababu nyingine yoyote. Mh. Mkapa alitoa kauli hiyo kufuatia risala ya Waislamu iliyoorodhesha dhidi ya msururu wa malalamiko dhidi ya serikali yake. Katika ujumla wake risala hiyo imeonyesha kwamba Waislamu wanaonewa na hawatendewi haki. Kauli hii ya Mh. Rais imekuja wakati Waislamu wanavutana na vyombo vya dola pamoja na vile vya sheria kuhusu nyumba zao za Wakfu ambazo zimeporwa na Bw. Daniel Zakaria. Mwenendo wa vyombo vya sheria na vile vya dola umekuwa ukitia wasiwasi kiasi cha Waislamu kupoteza imani na kuamua kujisaidia wenyewe. Katika hatua hiyo, mwishoni mwa wiki iliyopita Waislamu waliitwaa nyumba ya Wakfu iliyogeuzwa baa wakaisafisha na kuweka ulinzi wakisubiri atakayekuja kudai kwamba ni mali yake. Polisi kutoka Msimbazi hapana shaka kwa ombi la Bw. Daniel walifika na kuwakamata baadhi ya vijana waliokuwa wakilinda nyumba hiyo. Ni kituo hicho hicho cha Msimbazi ambapo awali ilitolewa (RB) ya kusakwa kwa Bw. Daniel kwa kosa la kughushi hati za nyumba. Vipi leo Bw. Daniel kajitokeza mwenyewe, badala ya kukamatwa anapewa ulinzi kutetea nyumba alIzotuhumiwa kughushi hati zake! Bw. Daniel ana vielelezo vya mahakama vinavyompa haki ya usimamizi wa nyumba za Hajat Aziza. Haki hiyo anapewa wakati ipo hati ya kiapo mahakamani inayoonyesha kwamba nyumba hizo ni Wakfu. Hali kama hii hupelekea kujengeka dhana ama ya kuwepo rushwa au upendeleo. Vyovyote iwayo, rushwa ni adui wa haki na uonevu, upendeleo na ubalakala katika sheria ni mambo yasiyo kubalika katika jamii. Uislamu umesimama juu ya haki. Kama ambavyo hathubutu kudhulumu; kukubali kudhulumjiwa ni mwiko pia kwake Muislamu. Kama ni kulalamika Waislamu wamelalamika sana. Pengine umefika wakati vyombo vya sheria na vile vya Dola, viwe makini zaidi, vinginevyo vitapoteza umuhimu wake na kuzaa hali tusiyoiomba. WAISLAMU Jijini Dar es Salaam wamemtaka Kamanda Gewe amkamate Bw. Daniel Zakaria kwa kosa la kughushi hati za nyumba na kutaka kuzipora. Wito huo umetolewa kufuatia ushahidi mpya uliopatikana kuelezea jinsi Bw. Daniel alivyokuwa amefanya jaribio la kupora nyumba za Hajat Aziza Bint Omar toka akiwa hai. Ushahidi huo unaonyesha kwamba mwaka 1986 Bw. Daniel alighushi hati za nyumba na kuandika jina lake la Daniel Zakaria. Taarifa zilipelekwa kituo cha Polisi Msimbazi ambapo ilitolewa hati ya kusakwa Bw. Daniel. Hata hivyo Bw. Danile hakuonekana hadi alipofariki Hajat Aziza. (Marehemu) Hajat Aziza alipewa barua na Polisi akapewa hati mpya na jina la Daniel Zakaria likafutwa kwenye vitabu vya ofisi ya kodi ya mapato. Katika hali isiyoeleweka Bw. Daniel kupitia mahakama ya Kisutu alipewa kibali cha usimamizi wa nyumba hizo. Kufuatia shauku ya Waislamu kutaka kujua ni kwanini Bw. Daniel hajakamatwa, ANNUUR iliwasiliana na Kamanda wa polisi mkoa wa Dar es Salaam Bw. Alfred Gewe. Hata hivyo, Kamanda Gewe alipoombwa
aeleze ni kwa nini Bw. Daniel hajakamatwa na hati ya polisi ya kukamatwa
mtuhumiwa humaliza uhalali wake baada ya muda gani, hakutaka kusema lolote
akidai kwamba suala hilo lishahukumiwa mahakamani.
|
YALIYOMO
Tahari
Kupokelewa kwa malalamiko ya Waislamu: Masheikh wasubiri ukweli wa Mkapa Afariki baada ya kutokwa damu nyingi: Yadaiwa hakuwa na sh. 4,000 Nyumba ya Wakfu iliyoporwa yarejeshwa Kamanda Gewe atakiwa amkamate Daniel Sheikh awasambaratisha walevi Liwale Msikiti wavamiwa na kuvunjwa milango, madirisha Msikiti wa Mwinyimkuu wafanya sensa Njaa hakuna, tunategemea kula silaha Mabaraza yawatetee Waislamu - Sheikh Bafadhil Hali ya Uislamu Lukulunge, Kongwa inatisha Waislamu Kondoa waagizwa kuyatunza magazeti ya ANNUUR Sabato ni ya Waisraeli, Mungu alikwishaiondoa
Tume ya kubadili Katiba Kenya: Waislamu kuwakilishwa Waislamu Msonge waomba wanusuriwe Sayansi na Teknolojia
Chakula na Lishe
|