|
|
Tukio hilo lilitokea katika Masjid Nuru ulioko kata ya Bazirayombo kata ya Chato wilayani Biharamulo. Kadhia hiyo ilifuatia baada ya kundi hilo kupiga disko kwa sauti ya juu kiasi ambacho Waislamu hawakuweza kusikilizana katika swala. Waumini wa Msikiti huo waliamua kwenda kwa wanaopiga disko hilo ndani ya ukumbi uliopo katika nyumba ya wageni (Guest House) iliyoko jirani na Msikiti huo na kuwaomba wapunguze sauti kama sio kuzima kabisa, kwani ibada yao haifanyiki kwa utulivu unaotakiwa. Mpiga disko aliyejulikana kwa jina la Abdallah Omar aliamua kupunguza sauti ya muziki huo jambo ambalo washabiki (wachezaji) hawakuwa tayari na hilo wakaamua kuwafuata Waislamu ili kujua ni kwanini waharibiwe starehe zao kwa masuala ya ibada (swala). Kabla ya kufika Msikitini walikutana na kundi la Waislamu waliokwenda kuwaomba wapunguze sauti ya muziki. Ndipo mzozo mkali ulipoanza na kurushiana makonde na bakora jambo ambalo liliwafanya waumini (Waislamu) kukimbia kwa vile walikuwa wachache kuliko kundi jingine. Kundi hilo halikuishia hapo lilikwenda moja kwa moja Msikitini na kuvamia milango na madirisha wakaivunja vunja. Aidha, misahafu (Qur’an), miswala pamoja na jeneza viliteketezwa kwa moto kabisa. Mwandishi wa habari hizi alipoongea na Mkuu wa wilaya kuhusiana na kadhia hii; mkuu huyo alionyesha kutokuwa tayari kulizungumzia japo analifahamu vizuri badala yake alitakakujua ni nani aliyefikisha taarifa hizi gazetini. Hata hivyo, aliamua kulizungumzia ambapo alidai kuwa hili si suala la kidini bali suala la kijamii kwani mpiga disko ni Muislamu. Amesema kwamba vyanzo vyake vya habari vyaonyesha kwamba kundi fulani lililojiita la Kikristo lilimuomba Bwana Abdallah ambaye ni mfanyabiashara aonyeshe kanda za Kikristo siku ya Krismasi ambazo zingeonyesha historia ya Yesu Kristo. Wakati Bwana Abdallah anangojea watazamaji wajae ndani ya ukumbi aliweka kanda za muziki kuwaburudisha watu ambao tayari walishaingia ukumbini tayari kwa maonyesho ya sinema (picha) zilizokusudiwa. Muziki huo ukawa ndio chanzo cha vurugu hizo. Aidha, Mkuu wa wilaya alisema kwamba analiita suala la kijamii lililowahusisha vijana wa kihuni kwa sababu wale waliotoka Msikitini hawakuingilia mlango wa mbele kama kawaida bali walitumia mlango wa nyuma jambo ambalo si la kawaida. Si hivyo tu, bali waliingia na bakora tayari kwa mapambano. Kundi la pili nalo ni la kihuni kwa sababu hapakuwa na uhusiano kati ya Msikiti na watu waliwafuata kuzima disko lao. La msingi wangepambana nao kisha baada ya kuona wamekimbia wangeendelea na starehe zao. "Kwa hiyo, ndugu mwandishi hilo ni suala la kijamii na wala si la kidini", alimalizia sehemu hiyo. Hata hivyo; Mkuu huyo wa wilaya alisema bada ya yeye kupata taarifa hizo akiwa mkutanoni Bukoba mjini alilazimika kwenda haraka baada ya mkutano huo ili kushughulikia suala hilo. Aliongeza kusema kuwa alikwenda eneo la tukio na kukutanisha pande zote mbili (Wakristo na Waislamu) kwa lengo la kusuluhisha mgogoro huo na si kusikiliza kesi. "Kwa bahati nzuri ndugu Mwandishi tulikubaliana kwamba suala hilo ni la wahuni na hivyo lisiendelee zaidi ya hapo na wala asilitoe yeyote katika vyombo vya habari kwani lingeleta sura mbaya katika jamii ", alimalizia Mkuu wa Wilaya. |
YALIYOMO
Tahari
Kupokelewa kwa malalamiko ya Waislamu: Masheikh wasubiri ukweli wa Mkapa Afariki baada ya kutokwa damu nyingi: Yadaiwa hakuwa na sh. 4,000 Nyumba ya Wakfu iliyoporwa yarejeshwa Kamanda Gewe atakiwa amkamate Daniel Sheikh awasambaratisha walevi Liwale Msikiti wavamiwa na kuvunjwa milango, madirisha Msikiti wa Mwinyimkuu wafanya sensa Njaa hakuna, tunategemea kula silaha Mabaraza yawatetee Waislamu - Sheikh Bafadhil Hali ya Uislamu Lukulunge, Kongwa inatisha Waislamu Kondoa waagizwa kuyatunza magazeti ya ANNUUR Sabato ni ya Waisraeli, Mungu alikwishaiondoa
Tume ya kubadili Katiba Kenya: Waislamu kuwakilishwa Waislamu Msonge waomba wanusuriwe Sayansi na Teknolojia
Chakula na Lishe
|