|
|
|
KATIKA makala yetu ya chakula na lishe ya wiki iliyopita tulijifunza saumu na lishe ya mama mjamzito. Makala hiyo ni mfululizo wa masomo maalumu ya chakula na lishe kwa wasomaji wetu Waislamu wanaoendelea na mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani. Katika kuendeleza lengo hilo, makala ya juma hili inatazama saumu na lishe ya mama anayenyonyesha. Tulijifunza katika makala ya wiki iliyopita kuwa mama aliyekwishajifungua (anayenyonyesha au la) wanaruhusiwa na sheria ya dini ya Kiislamu kuahirisha funga zao. Kwa maneno mengine wanaruhusiwa kula mwezi wa Ramadhani na watawajibika kulipia siku zao wakati hali zao zitakapokuwa za kawaida. Hata kama zitakutana Ramadhani mbili kama sababu ya kutokufunga bado ipo atazilipia siku za mbele. Baadhi ya kina mama wa Kiislamu wamekuwa wakisita kuitumia ruhusa hiyo (ya kuahirisha kufunga) kwa hoja dhaifu. Kwa mfano, wapo kina mama wa Kiislamu (wenye mimba hata za miezi minane) ambao wanafunga kwa hoja kuwa hawawezi kulipia katika siku ambazo hakuna wengine wanaofunga. Sheria ya dini ya Kiislamu imewapa kinamama wenye mimba na wanaonyonyesha (na Waislamu wenye nyudhuru nyingine) uhuru wa kufunga au kuahirisha funga kwa hoja kwamba watazame afya za watoto wao (wanaonyonya au wale walio tumboni). Kwa hiyo, kudai kuwa ukiahirisha saumu itakuwa tabu wakati wa kuilipa kwa sababu hakuna watu wengi watakaokuwa wanafunga kama ilivyo wakati wa mwezi wa Ramadhani ni makosa. Sambamba na hoja hiyo, swala la kuathirika kiafya kwa mama mjamzito (au anayenyonyesha) na mtoto wake aliyetumboni (au aliyekwisha zaliwa) tunaweza kulilinganisha na mvuta sigara au anayekunywa pombe. Mvuta sigara au mnywa pombe si rahisi mwanzoni kuona anavyoathirika na na ndiyo maana wapo wanaodai kuwa mbona afya zao ni sawa au bora zaidi ya wale wasiovuta sigara au kunywa pombe! Lakini kadiri siku zinavyokwenda inafikia mahali mvutaji sigara au mnywaji pombe anaona athari mbaya ya "kazi" yake ya uvutaji au ulevi. Halikadhalika, mama mjamzito au anayenyonyesha anaweza kuiona athari ya yeye kufunga katika mwili wake au kwa mtoto. Kwa mfano, mama mjamzito au yule anayenyonyesha asipopata lishe ya kutosha (hata kwa masaa kumi na nne au zaidi kidogo kama ilivyo katika funga) anaweza kuathiri ukuaji wa mtoto kiakili. Athari kama hiyo mama hawezi kuiona kwa macho yake. Kwa hiyo, ushauri wa watalaamu wa afya, tiba na lishe lazima uheshimiwe. Baada ya utangulizi huo, ni vyema sasa tukarudi katika kiini cha makala yetu ya wiki hii. Lishe bora ya mama baada ya kujifungua ni jambo la muhimu sana. Hii ni kwa sababu mama huyo anahitaji kurekebisha mwili na hali yake ya lishe iliyoathirika wakati wa ujauzito. Zaidi ya hayo, hali nzuri ya lishe ya mama itauwezesha mwili wake kujilinda na maradhi na vile vile mwili kuweza kutoa maziwa ya kutosha kwa ajili ya mtoto wake mchanga. Baada ya kujifungua mama anahitaji kula vyakula vya mchanganyiko. Vyakula hivyo ni: Vyakula vya kujenga mwili kwa mfano, nyama, samaki, maharage, kunde, njegere, choroko, dengu, mbaazi, n.k. Vyakula vingine ni vile vya kutia nguvu na joto mwilini kama vile mahindi, mtama, uwele, ulezi, mpunga, ngano, ndizi za kupika, viazi, mihogo, asali, mafuta, n.k. Pia kundi lingine la vyakula ni vile vya kulinda mwili kwa mfano matunda na mboga za majani za aina mbalimbali. Mama anayenyonyesha anahitaji mlo wa mchanganyiko tuliouona hapo juu. Lazima apate milo ya aina hiyo mara nne au zaidi kwa siku. Pia ale chakula zaidi ya kile anachokula siku za kawaida. Ni matarajio yangu kuwa baada ya maelezo ya hapo juu, hikma ya sheria ya dini ya Kiislamu ya kuwaruhusu kina mama wanaonyonyesha kuahirisha saumu zao iko wazi. Hivyo basi, na tuipokee. |
YALIYOMO
Tahariri
Wananchi wahoji kuhusu polisi aliyeua Arusha Dondoo za Saikolojia
Kona ya Wacha Mungu
Jicho la Uzalendo: Bhabhoo! Muungwana
huyoo!
Maulana Sayyid Jamal-Din Afghan 1214 - 1254 (1838-1897) Mafunzo kuhusu funga ya Ramadhani
Marekani ni mtetezi au adui wa haki?:
Umoja wa Mataifa upo upande gani?
Dawa ya ukimwi ni mwenendo mwema
Mwalimu Maif: Mwanamke aliyetumia maisha yake kufundisha Qur'an Wazazi waaswa kutoshabikia maovu Je, hivi tuendelee kushika amri za
Mungu tena? (jibu)
Mapinduzi, Muungano kwa manufaa ya nani? Fufueni EAMWS - Sheikh Amana
Msiitupie lawama serikali - Dk. Omar Baada ya kuvunjiwa nyumba,
kuchomewa vyakula na Serikali: Nzasa sasa wafuturu Maembe
Acheni mifumo mibovu, fuateni Qur'an - Sheikh Kilemile Sayansi na Teknolojia
Chakula na lishe
|