AN-NUUR 
Na.179 Shaaban  1419, Desemba 11 - 17, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Ijue SUA Madrasa Moro
 
  • Ilianzishwa na wanafunzi wa Chuo Kikuu kambi ya Mazimbu 
  • Inasomesha familia tatu za SUA 
Na Mussa Ally, Morogoro

"LICHA ya kupigwa vita na wasomi kadhaa wa SUA Mazimbu Campus wakiwemo wasomi Waislamu, SUA Madrasat ikiwa na wanafunzi 50 hivi sasa imepita hatua moja mbele kuelekea kwenye kiini cha malengo yake". 

Hiyo ni kauli ya mwalimu Mohammed Abdallah Mazohanya Ustaadh wa Madrasa hiyo akilifamisha AN-NUUR hali halisi ya madrasa yake, 

Madrasat SUA Mazimbu Campas ilianzishwa mapema mwaka 1997 na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Morogoro kwa lengo la kutoa elimu ya msingi ya dini ya Kiislamu kwa wana watoto wa wafanyakazi wa chuo hicho na pembezoni mwake. 

Mazimbu Campas ilipo madrasa hiyo ni miongoni mwa sehemu chache za kitaaluma zenye wakazi wengi Waislamu mjini hapa, hivyo suala la kuwepo madrasa lilikuwa ni la lazima. 

Na hicho ndicho hasa kilichowapelekea wasomi hawa wa Kilimo kuanzisha shule hiyo. 

"Tulianza kwa taabu sana kutokana na wasomi wengi wa Kiislamu wenye fikra za kimagharibi kutuoona umuhimu wa watoto wao kufunzwa maarifa ya Kiislamu. Wanaona madrasa zanawaharibia masomo mengine ya shuleni watoto wao, hata hivyo mzee wetu Bw. Said Waziri Mbwana ametupatia darasa nyumbani kwake, tunamshukuru sana" alisema mwalimu Mohammed na kuongeza "kuna watoto wa familia tatu tu za wasomi wa hapa SUA, wengine wote wanatoka nje ya kambi, hili pia ni tatizo". 

Madrasa hiyo licha ya matatizo hayo inawafunza vijana hao wadogo maarifa ya Kiislamu, lugha ya Kiarabu, Kiswahili, Kuandika na wako mbioni kufunza lugha ya Kiingereza, Hisabati na Sayansi. 

Licha ya kuwa ina muda mfupi tangu kuasisiwa kwake, lakini wanafunzi wake wanaonyesha matumaini ya kufikia kwenye malengo. 

"Tunachohitaji ni ushirikiano mzuri na wazazi, hilo litatusaidia kutoka hapa tulipo na kufika pale tulipokusudia kwa mafanikio", alisema Mwalimu Mohamed. Mmoja wa wazazi na waasisi wa madrasa Dk. Ally Fungo ametoa mfano wa ushirikiano huo kwa kujitolea posho kwa mwalimu kila mwezi." 

Kuhusu suala la mtaala, mwalimu huyo alisema kuwa, mara kadhaa wamekuwa wakitumia mitaala ya nchi jirani ambayo mazingira yake ni tofauti kidogo na yetu, hivyo amefurahishwa sana kusikia habari njema ya mitaala mipya ya Kitanzania iliyoandaliwa na IPC kutolewa. 

"Lakini tunaisikia tu, bado hatujaipata wala kuiona katika maduka ya vitabu. Tunaomba taasisi husika kutusambazia ‘silabasi’ hizo mapema iwezekanavyo ili wakati usitiache nyuma", alimalizia kusema Mwalimu Mohamed Abdallah. 


Kiteto wakosa darsa kwa kupinga Ramli
 

INASEMEKANA kwamba mwalimu aliyekuwa akifundisha dini kijijini Matui wilayani Kiteto amefukuzwa na hivyo kuwakosesha Waislamu darsa. 

Imeelezwa kwamba kufukuzwa kwa mwalimu huyo kumechochewa na baadhi ya watu wanaohisi wanaharibiwa biashara yao ya sihri na ramli kutokana na Waislamu wengi kuiva katika Tawhiid. 

Habari zaidi zimefahamisha kwamba, baada ya Waislamu wengi kuivishwa katika elimu ya Tawheed wamekuwa wakipinga mambo mengi ya shirki ambayo yalikuwa yamezoeleka kijijini hapo. 

Hali hiyo imeelezwa kwamba ndiyo iliyopelekea baadhi ya watu wasiotaka kuachana na jadi zao kujenga hoja kwamba Ustadh anafundisha kinyume na wao walivyosomeshwa zamani na Masheikh wao. 

Baadhi ya Waislamu waliongea na mwandishi wa habari hizi walisema kwamba mwenendo kama huo utapelekea Uislamu kuendelea kuwa kitu kigeni vijijini. 

Ustaadh Haruna J. Mdoe aliye miongoni mwa waathirika alisema kwamba si rahisi kumpata Sheikh kukubali kuishi kijijini ili awaelimishe watu. Kwa hiyo kufukuzwa kwa huyo ambaye tayari alikuwa amejitolea kuyakabili maisha ya kijijini ili Waislamu wanufaike na elimu yake ni dhahiri kutawakatisha tamaa hata wengine kuja. 

Ustaadh aliyefukuzwa ambaye hakupendelea jina lake litokee gazetini alisema kwamba yeye anaamini hakufanya lolote kinyume na Uislamu na pia taratibu za ufundishaji na hivyo anachofanya ni kuwasiliana na muajiri wake Ofisi ya Bakwata mkoa wa Arusha ili kujua hatma ya ajira yake. 

Kijiji cha Matui kina vitongoji sita ambavyo ni Azimio, Bwawani, Chapakazi, Juhudi, Kivukoni, Maweni na Soweto. 

Kijiji pekee chenye madrasa hivi sasa ni Azimio ambapo mamia ya watoto husoma chini ya mwalimu mmoja tu Ustaadh Mohammed Kisisa. 



Ustadh ayeyuka na saruji ya Msikiti mjini Arusha  

USTADHI mmoja (jina tunalihifadhi) anadaiwa kutoroka na mifuko 62 ya saruji ambayo ilitolewa na mfadhili mmoja kwa ajili ya ujenzi wa Madrasa ya Ngarenaro. 

Taarifa kutoka Msikiti Mkuu wa Ijumaa Ngarenaro zimeeleza kwamba Ustadh huyo alikabidhiwa mifuko hiyo 62 na mmoja wa wadhamini wa Msikiti huo lakini badala ya kuiwakilisha Msikitini akamuuzia mfanyabiashara mmoja kwa shilingi laki tatu. 

Ustadhi huyo ambaye pia ni mwalimu wa madrasa ya Msikiti huo, inasemekana ameiuza simenti hiyo kwa mfanyabiashara mmoja mwenye duka karibu na ofisi za Idara ya Maji Mkoa. 

Habari zaidi zimeeleza kwamba Ustadhi huyo alipohojiwa na uongozi wa Msikiti alikiri kosa na akaomba apewe watu wa kuandamana naye kwenda kuonyesha saruji hiyo ilipo. 

Hata hivyo, aliwatoroka watu aliofuatana nao walipofika maeneo ya Ol-Matejo na mpaka sasa hajulikani alipo. 

Sheikh na Imam Mkuu wa Msikiti wa Ngarenaro alipohojiwa na gazeti hili alikiri kuwepo kwa tukio hilo. 

Hata hivyo, hadi tunakwenda mitamboni suala hili lilikuwa halijafikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa madai kwamba uongozi umempa muda mtuhumiwa ajirudi. 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
Maoni
Waislamu tunakusudiwa kufanywa watumwa wa nani?

Wananchi waingiwa na hofu kuhusu silaha

Serikali yagwaya kwa wafugaji nguruwe 
Na Muhibu Said

Hakuna njama za kupindua Bakwata - Sheikh Yahya

MARADHI YA KISAIKOLOJIA:: VOYEURISM
Na. Abu Halima Sachangwa

Tathmini: Miaka 37 ya uhuru wa Tanganyika
Na Maalim Mwalimu

Adabu katika swala

Mdahalo kati ya Waislamu na Wakristo: Batendi hakumuelewa Mkomidachi
Na Ally Said

Muhammad (s.a.w.) katika Unabii wa Isaya  (a.s.)
Na Sheikh Bernard P. Nyangasa, Korogwe

Ijue SUA Madrasa Moro
Na Mussa Ally, Morogoro

Kiteto wakosa darsa kwa kupinga Ramli

Ustadh ayeyuka na saruji ya Msikiti mjini Arusha

Akina mama Muheza waungana kufanya Daawa
Na B. Mwakangwale

Wanafunzi Waislamu Mbeya wapata uongozi
Na B.  Mwakangwale

Je, hivi tuendelee kushika amri za Mungu tena? - 2
Na Mwinjilisti Bunga E. Dettu

Njia ya uzima ni nyembamba,  waionao ni wachache - 2
Na Yasin Valerian Massawe

Waandishi andikeni ukweli - Kamati
Na Mwandishi Wetu

Sheikh Jongo  aichachamalia Uwawaru
Na Badru Kimwaga

Waamriwa kurejesha Mali ya Mirathi
Na Njuki  A.

Waislamu Mlimba Moro mashakani
Na Q. Mataita

Sayansi na Teknolojia 
[Ielewe Modem yako] 
 
Mafundisho ya Quran

Masomo ya Dini ya Kiislamu 

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Futari ya Tende] 
 
Tangazo
Vitabu na Mihutasari ya Maarifa ya Uislamu
 
 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita