AN-NUUR  Na.174 Rajab 1419, Novemba 6 - 12, 1998 
 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
JIFUNZE KUUNGANISHA KOMPYUTA (IV)
 
Hassan Omar
  

UTANGULIZI 
  

Sababu za kutaka kuunganisha kompyuta mbili au zaidi zipo nyingi. Kwa mfano unaweza kuwa na haja ya kuyafanya majalada au mafaili yaliyo kwenye kompyuta moja yaweze kusomeka kutoka kwenye kompyuta nyengine. Au unaweza kuwa unayo printa moja tu uliyoiunganisha na moja kati ya kompyuta zilizopo lakini ukataka kompyuta zaidi ya moja ziweze kuitumia printa hiyo. Au pia, unaweza kuwa unayo line moja tu ya simu uliyoiunganisha na moja kati ya kompyuta zilizopo, kompyuta ambayo ndio pekee yenye modem, lakini ukataka kompyuta nyengine ziweze kuitumia line hiyo hiyo ya simu na modem hiyo hiyo moja. 

Ukiwa na haja zilizoelezwa hapo juu, hapana shaka utahitaji kuziunganisha kompyuta zako kwa njia fulani. Sehemu tatu za mwanzo za makala hii zimejishughulisha zaidi na njia za kutimiza haja ya kuweza kuyasoma majalada ya kompyuta moja kutoka kwenye kompyuta nyengine. Lakini njia hizo hazitafaa kutimiza haja ya kuweza kutumia printa au modem iliyounganishwa na kompyuta moja wakati ukiwa unatumia kompyuta nyengine. Kwa haja kama hizo utahitaji njia maalum ya kuziunganisha kompyuta zako ili kwa pamoja ziweze kufanya kitu kinachoitwa Local Area Network, au kwa ufupi "LAN". 

LAN ziko za aina kadhaa, lakini katika makala hii tutaelezea jinsi ya kuziunganisha kompyuta zinazotumia Windows 95 (au Windows 98), kufanya aina ya LAN inayojuilikana kama "peer-to-peer", yaani kiungo kati ya kompyuta ya kawaida na kompyuta nyengine ya kawaida (PC-to-PC), na sio LAN ya kuunganisha kompyuta za kawaida na server

Kama unataka kuziunganisha kompyuta (PC) ili zifanye LAN, na moja kati ya kompyuta hizo unataka iwe server ya kuzihudumia kompyuta nyengine, basi kwenye hiyo kompyuta itakayofanya kazi kama server utahitaji kutumia programu-mama ya utando (network operating system) kama vile Linux, Windows NT au Novell Netware. LAN ya namna hiyo hatutaizungumza kwenye makala hii. LAN ya aina ya peer-to-peer inaweza kufanywa kirahisi kwa kutumia kompyuta zenye Windows 95 au Windows 98 kwani programu-mama (operating system) hizo tayari zinao uwezo wa kutengeneza LAN za namna hiyo. 
  

VIFAA VINAVYOHITAJIKA 

Kifaa muhimu kinachohitajika kuziunganisha kompyuta kufanya LAN ni kadi ya utando , kwa Kiingereza, "network interface card" (NIC). Kila kompyuta itahitaji kuwa na NIC yake. 

network card
Picha 1: Kadi ya utando (network interface card)
 
NIC zipo za kasi (speed) na aina tafauti. Zipo NIC za aina ya ISA (Industry Standard Architecture) na pia za aina ya PCI (Peripheral Component Interconnect) kulingana na aina ya basi la data (data bus) linalotumiwa na kadi hiyo au aina ya upenyo wa motherboard inapoweza kuchomekwa kadi hiyo. NIC zinazotumika kwenye basi la data la aina ya PCI bila shaka ni bora zaidi kwa utendaji kazi kuliko NIC za aina ya ISA. Hii ni kwa sababu, basi la aina ya PCI linahimili kasi kubwa sana ya kusafirisha data – kiwango cha juu cha kasi hiyo ni megabaiti 264 kwa sekunde moja (264 Mbytes/sec)! Basi la data la aina ya ISA linahimili kasi ya juu ya kusafirisha data isiyozidi 8 MHz (au 8 Mbits/sec). Lakini kwa ujumla, kwa matumizi ya nyumbani na kwenye ofisi ndogo NIC za ISA ambazo ni za bei nafuu zaidi, kuanzia US$20 na kuendelea, zinatosha kabisa. 

NIC pia zinatafautiana kwa aina za nyaya zinazoweza kuchomekewa. Kuna ambazo zinaweza kutumika pamoja na nyaya za aina ya UTP (Unshielded Twisted Pair) zenye plagi za aina ya RJ-45 (Registered Jack 45) , na ziko nyengine ambazo zimetengenezwa kutumika pamoja na nyaya za aina ya coax (yaani coaxial cable) zenye kiungo (connector) cha aina ya BNC (Bayonet Nut Connector). Waya huu wa coax unafanana na ule unaotumika pamoja na TV lakini tafauti yao ni kuwa waya wa coax unaotumika kwenye LAN ni wa 50 ohms wa aina ya RG-58, wakati ule unaotumika pamoja na TV ni wa 75 ohms. Hizo 50 ohms na 75 ohms ni za kipimo maalum cha waya kinachoitwa kwa Kiingereza "characteristic impedance". Kwa hivyo, characteristic impedance ya waya unaotumika kwenye LAN ni 50 ohms
 
Baadhi ya NIC zinazo sehemu za kuchomekea plagi ya RJ-45 na pia sehemu za kuchomekea kiungo cha BNC. Plagi za aina ya RJ-45 ziko kama plagi za simu za kawaida zinazotumika Marekani, yaani za aina ya RJ11, lakini plagi za RJ-45 ni pana zaidi. Ukiwa na kifaa kinachoitwa "RJ-45 Crimp Tool" unaweza kutengeneza mwenyewe, na kwa bei nafuu, nyaya za kutumika kwenye LAN. Hata nyaya za coax ni rahisi kuzitengeneza mwenyewe. 

 
Picha 2: Waya za aina ya Unshielded Twisted-pair zenye plagi za RJ-45
 

Lakini watu wengi wanapendelea kutumia nyaya za aina ya UTP zenye plagi za RJ-45 kama zinacvyoonekana kwenye Picha 2, kwa vile ni rahisi kuzitumia. Waya wa aina ya UTP una jozi mbili za nyaya ndani yake – jozi moja kwa kupelekea data na ya pili kwa kupokelea data. Waya huo unaitwa "twisted pair" kwa vile jozi za waya zilizomo ndani yake zimezongwa pamoja kwa mtindo maalum ili zisiweze kuathirika na umeme ulio kwenye anga unaotoka kwenye vyanzo mbali mbali kama vile vifaa vya elektroniki na hata radi. Nyaya hizo unaweza kuzitumia kuunganishia kompyuta kwa masafa yasiyozidi mita 100 kwa mujibu wa viwango vilivyowekwa. 

Ukitumia waya wa coax utahitaji pia kuwa na viungo vya "T" (yaani T-junction) kadhaa kutegemeana na idadi ya kompyuta ulizonazo, na pia utahitaji kuchomeka "50 ohm coaxial terminator" kwenye kila sehemu ya T-junction iliyokuwa haikuungwa na chochote. Huo ni udhia kidogo na ndio maana watu wengi wakapendelea waya za UTP zenye plagi za aina ya RJ-45. Lakini waya za coax zinakuruhusu kuunga kompyuta zako kwenye masafa marefu zaidi, ambayo yanaweza kufikia mpaka mita 185. Lakini masafa kati ya kompyuta mbili zilizoungwa kwa kutumia waya wa coax hayatakiwi kuwa chini ya nusu mita kwa mujibu wa viwango vilivyokubalika. 

NIC za aina ya 10Base-T, ambazo ni maarufu zaidi, zinaweza kupeleka au kupokea data kwa kasi ya juu ya 10 Mbps (megabits per second), yaani bit ("0" au "1") milioni 10 kwa sekunde moja! Hiyo ni kasi kubwa sana, lakini zipo NIC za aina ya 10/100Base-T zenye uwezo wa kupeleka au kupokea data kwa kasi ya juu ya 10 Mbps na pia 100 Mbps. Kama LAN ina kompyuta chache tu, NIC za aina ya 10Base-T zinatosha kukidhi haja. 

10Base-T hasa ni aina moja ya LAN zinazotumia njia ya mawasiliano inayojuilikana kama Ethernet. Kwenye neno 10Base-T , "10" inamanisha "10 Mbits/sec" ambayo ni kasi ya juu ya data inayohimiliwa kwenye LAN ya aina hiyo, "Base" inawakilisha neno "Baseband" ambao ni mtindo wa kusafirisha data unaotumiwa na LAN ya aina ya Ethernet, mtindo ambao ni data za aina ya Ethernet pekee zinazosafirishwa. Herufi "T" inamaanisha "Twisted-pair", ambao ni aina ya waya unaotumiwa kwenye LAN za aina hiyo – LAN hizo zinajuilikana kama Twisted-pair Ethernet

Aina ya waya inaelekeza juu ya masafa ya juu yanayoweza kutumiwa pamoja na waya huo. Kama tulivyoeleza kabla masafa hayo ni mita 100 kwa waya wa aina ya Twisted-pair. LAN zinazotumia nyaya nyembamba za aina ya coax, zinajuilikana kama Thin Ethernet na hizo hujuilikana kama 10Base-2. Hiyo "2" ukizidisha mara 100 inakupa masafa ya juu yanayoweza kutumika kuungnaisha kompyuta kwenye LAN inayotumia nyaya za namna hiyo. Kwa 10Base-2 masafa hayo ni mita 200, lakini hayo ni makisio tu, masafa halisi ni mita 185 kama ilivyoelezwa kabla. LAN za aina ya 10Base-5 zinazotumia waya mnene wa aina ya coax, zinajuilikana kama Thick Ethernet, na zinaweza kutanda kwenye masafa marefu ya wastani wa mita 500. 

Ukihitaji kutengeneza LAN kuunganisha kompyuta mbili tu, utakachokihitaji ni NIC mbili na waya maalum unaojuilikana kama "crossover cable". Waya huo upo wa urefu mbali mbali mpaka futi 25 na bei yake ni kama US$10. Unaweza pia kutumia waya wa aina ya coax kama NIC zako zina kiungo cha aina ya BNC. 

Ukihitaji kutengeneza LAN kuunganisha kompyuta zaidi ya mbili, utahitaji nyaya za kawaida za LAN za aina ya Category 5 10Base-T, (bei yake ni wastani wa US$15 kwa urefu wa futi 25), na kifaa kinachoitwa "network hub" au "concentrator" au "repeater". Hicho ni kifaa ambacho kinatumika kuziunga pamoja nyaya za LAN zinazotoka kwenye kompyuta mbali mbali kufanya mtindo wa kuunganisha kompyuta kwenye LAN unaoitwa "star network". Kwa mfano, ukiwa na "hub" yenye "port" nne za aina ya RJ-45, utaweza kuziunganisha pamoja kwa mtindo wa star, kompyuta nne zilizoko kwenye LAN yako. 

Hub nazo ziko za kasi ya 10 Mbps na pia 100 Mbps. Hub ya 10 Mbps yenye port nne unaweza kuinunua kwa bei ya kama US$50 au zaidi kidogo; na yenye port nane bei yake ni kama US$70 hivi. Hub za kasi ya 100 Mbps bila shaka ni ghali zaidi, kama US$100 kwa hub yenye port nne. Mara nyingi, wanaotengeneza NIC ndio hao hao wanaotengeneza hub. Watengenezaji maarufu ni pamoja na 3COM, Asante, Compex, D-Link, SMC, Intel, na Bay Networks. 

Kuna baadhi ya makampuni yanauza vifaa vya LAN kamili kamili (LAN kit) kwa pamoja. Unaweza kununua LAN kit yenye NIC mbili za aina ya ISA, waya wa aina ya UTP wenye plagi za RJ-45, hub ya port nne, diskette zenye programu na driver zote zinazohitajika, pamoja na kitabu chenye maelezo kamili ya kutengeneza LAN kwa kutumia vifaa hivyo. LAN kit ya namna hiyo bei yake ni nafuu sana, kama US$120. 

Baada ya kuelewa vifaa vinavyohitajika, kwenye sehemu inayofuatia tutaelezea namna ya kuitayarisha LAN yenyewe. 

Inaendelea toleo lijalo 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
TAHARIRI  
Tuacheni na njaa yetu msituongezee silaha 

Serikali yakumbushwa kujiunga OIC 
Na Mwandishi wetu 

Polisi walizingira nyumba yangu usiku wa manane - Sheikh Mbukuzi 

Wafungwa waomba Futari na Vikoi 

Macho ya shutuma 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Hoja pofu 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Tafuteni ufalme wa kisiasa 

Ubaguzi katika mfumo wa elimu nchini: Chuo Kikuu chasikia kilio cha wanawake 

'Vichupi' vya nini Kimiti? 
Na. Said Rajab 

Mjadala wa Katiba na haki za Waislamu 
Na Masoud Mohammed Mbogo 

Mdahalo kati ya Waislamu na Wakristo- 3 
Na Nandenga wa Mkomidachi 

Waliochukuliwa utumwa Uarabuni 
Na Hassan Omar 

Madrasatul Maamury Islamiya 

Teknologia: Jifunze Kuunganisha Kompyuta (4) 
Na Hassan Omar 

Kuweni wabunifu muinue taaluma - Wito 

TVZ na kipindi cha 'Wasemavyo' 

Kesi ya Waislamu Mwembechai: Mashahidi washindwa  

Wanyimwa fursa ya kuswali Ijumaa Mwanza 

Shule ya Bakwata yafungiwa Tanga 

Mafunzo ya Qur'an  
Shetani anawaogopesha wenye mali kutoa 

Barua za wasomaji  

Masomo ya dini ya Kiislam  

Chakula na lishe 

Mashairi 

Matangazo 
 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita