AN-NUUR  Na.174 Rajab 1419, Novemba 6 - 12, 1998 
 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Tuacheni na njaa yetu msituongezee silaha

TUNAVYOJUA na ndio hakika yenyewe wananchi wana shida ya huduma bora za afya, kilio chao ni maji safi na salama, shida yao ni barabara mbovu, ukosefu wa umeme wa kuaminika lakini wenye gharama kubwa. 

Kilio cha vijana ni ukosefu wa ajira, kwa wastaafu na wapunguzwa ni mafao haba tena yenye kucheleweshwa. 

Kilio na shida ya wauguzi ni vifaa hasa malipo duni sawa na wenzao waalimu ambao pamoja na kupata kichele kinachowafanya wauze ubuyu darasani badala ya kusomesha, wakati mwingine hukopwa hicho kichele chenyewe. 

Hizi ndizo baadhi tu ya kero za wananchi ambazo serikali ilitangaza na kuahidi kuziondoa. 

Hatujasikia kwamba wapo wananchi wamekabiliwa na kero kubwa ya kupata majambia kwa saabu ya ukiritimba wa biashara ya silaha. 

Maduka ya kaya ya sembe na chumvi yalileta kero kubwa na mateso kwa wananchi. Hatukushuhudia watu kupanga foleni za mawe kusubiri mgao wao wa kununua bastola wala leo hatusikii wananchi wakiilalamikia serikali kwamba ukata na njaa inazidi kwa sababu silaha zimekuwa adimu. 

Wema huu wa kuwarahisishia wananchi kupata silaha mbona hatuuoni kwenye mambo mengine ? 

Mbona hatuuoni kwenye kumrahisishia mkulima kupata mbolea pembejeo na huduma bora za usafirishaji kwa wakati na kwa bei nafuu ! 

Leo kijana kwa sababu hana ajira anastukia kaangukia shingo ya mtu na kuondoka na mkufu, je, akiwa na kasilaha kake ! 

Katika mazingira haya ya rushwa, njaa na kuanguka kwa maadili silaha zimejaa mitaani mpaka zile nzito nzito zisizoruhusiwa ila jeshini, je, itakapokuwa biashara huria. 

Hoja kwamba sheria na taratibu zitatumika kudhibiti upatikanaji wa vibali vya kununua silaha haina mashiko yoyote. Sheria hizo mbona zisifanye kazi leo wakati mwananchi wa kawaida hajui hata kama kuna maduka ya silaha. 

Hivi sasa serikali inadhibiti vibali na biashara yenyewe, lakini silaha zimetapakaa kwa majambazi, je, ukiingiza hisia ya kupata pesa kupitia biashara hiyo. 

Kama sababu ya serikali kurahisisha upatikanaji wa silaha ni kukidhi mahitaji ya wenye mali na mahekalu yao, hao tayari wanazo na kila anayehitaji kwa utaratibu uliopo anapata. 

Kutokana na hali ya uchumi duniani kote hivi leo biashara mbalimbali zimedoda, sikwambii ya silaha ambayo huhitaji kuwepo kwa ugomvi na migogoro mbalimbali. 

Wasiwasi wetu isije kuwa yote haya ni shinikizo la kunusuru biashara ya ‘nchi’ iliyododa. 

Sambamba na hilo pengine wapo wenye ‘amari’ zao kwa ajili ya ujambazi, ujangili na matumizi mengine haramu, hatua hii ya serikali haitahalalisha ‘amari’ hizo ? 

Kama tulivyokwisha sema awali tumezoea kusikia kuondolewa kwa kero za wananchi, je, tuna kero ya silaha leo ? 

Sisi kero yetu njaa; kama ni kero ya silaha labda tuambiwe yupo ‘mwekezaji’ anayetafuta soko la silaha zake ‘zilizododa’. 

  Juu 
 
YALIYOMO 
 
 
TAHARIRI  
Tuacheni na njaa yetu msituongezee silaha 

Serikali yakumbushwa kujiunga OIC 
Na Mwandishi wetu 

Polisi walizingira nyumba yangu usiku wa manane - Sheikh Mbukuzi 

Wafungwa waomba Futari na Vikoi 

Macho ya shutuma 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Hoja pofu 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Tafuteni ufalme wa kisiasa 

Ubaguzi katika mfumo wa elimu nchini: Chuo Kikuu chasikia kilio cha wanawake 

'Vichupi' vya nini Kimiti? 
Na. Said Rajab 

Mjadala wa Katiba na haki za Waislamu 
Na Masoud Mohammed Mbogo 

Mdahalo kati ya Waislamu na Wakristo- 3 
Na Nandenga wa Mkomidachi 

Waliochukuliwa utumwa Uarabuni 
Na Hassan Omar 

Madrasatul Maamury Islamiya 

Teknologia: Jifunze Kuunganisha Kompyuta (4) 
Na Hassan Omar 

Kuweni wabunifu muinue taaluma - Wito 

TVZ na kipindi cha 'Wasemavyo' 

Kesi ya Waislamu Mwembechai: Mashahidi washindwa  

Wanyimwa fursa ya kuswali Ijumaa Mwanza 

Shule ya Bakwata yafungiwa Tanga 

Mafunzo ya Qur'an  
Shetani anawaogopesha wenye mali kutoa 

Barua za wasomaji  

Masomo ya dini ya Kiislam  

Chakula na lishe 

Mashairi 

Matangazo 
 

 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita