|
MASHAIRI
Kumbukumbu
Salamu alaykum, jamani Isilamia,
Namshukuru Karimu, Allahu Mola, Jalia,
Nimeishika kalamu, ya moyoni kuyatoa,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Matendo yakiwa mema, kumbu twaitarajia,
Hata mabaya nasema, kumbukumbu hutujia,
Na umfanyie mnyama, watu watasimulia,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Nakiri mema matendo, yana faraja sikia,
Unajihisi upendo, unapoyakumbukia,
Mabaya yana uvundo, mawazoni kukujia,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Hata ukishafariki, watu watakumbukia,
Nguvu zako na mikiki, matendo kuwafanyia,
Kwa wema au kwa dhiki, jinalo kulitambua,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Beti hii ni khamsa, lengo linawafikia,
Viongozi nawaasa, matendo kuyapimia,
Wanapofanya mikasa, kuwatendea raia,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Kadhia ya Mwembechai, kumbukumbu imekaa,
Ni vurugu walidai, Salehe wakamuua,
Walimuona hafai, kauliwa kama paa,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Kukumbukumbu askari, make mkitambua,
Mmeshaitaka shari, ya akhera na dunia,
Chuki wetu hana heri, risasi kumfyatulia,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Na kwa wale viongozi, uongo wanaotoa,
Walioota mizizi, ya ukubwa Tanzania,
Kumbukumbu waziwazi, vichwani mwatujengea,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbikiwa.
Askari Magereza, madaraka walitwaa,
Mateso wakayakuza, kinamama kuumia,
Walikuwa kama Pweza, kuwaweka kwenye jua,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Kumbukumbu kwa Kitwana, Bungeni kufuatilia,
Ukweli umeunena, Mola atakulipia,
Umesaidia sana, viongozi wameloa,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Hata Ponda na Magezi, wakitajwa twajua,
Omar Juma yu wazi, Yusufu Makamba pia,
Twajua walotuenzi, kwa Mwembechai kadhia,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Kumbukumbu historia, vizazi kufuatilia,
Nawe Waziri Amiri, watoto watakujua,
Na tena wawe tayari, sheria kushikilia,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Uongozi wa Mkapa, awamu hii twalia,
Sheria wamezikwepa, maovu kutufanyia,
Wengine tumeshaapa, CCM kutochagua,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Msione tunasema, muda mrefu sikia,
Kwa kweli limetuuma, Islamu kujifia,
Uuaji kama nyama, iwe mwisho Tanzania,
Matendo ni kumbukumbu, ya mtu kukumbukiwa.
Mwl. Zazibu Iddi Ng’onda,
S.L.P. 78, Shinyanga.
Waislamu tumche Mungu
Bisimillahi Rabbuka, Ubariki ummatia,
Pia nijaze fanaka, nipate kusimulia,
Tuhimizane hakika, Mola kukusujudia,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Mhariri msifika, litawanye shairia,
Wapate soma hakika, yalo ndani ummatia,
Tukimtii hakika, Mtume wetu Nabia,
Tumche Mungu dawamu, janna tupate tulia.
Islam kwa hakika, tubu kwa Mola Jalia,
Na e atupe baraka, kiumbe kutujalia,
Kheri nyingi na fanaka, zitufike ummatia,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Ramadhani ikifika, tubu pia kujutia,
Madhambi kuyafunika, mema kujifanyia,
Dawamu kutowa zaka, fitiri kujitolea,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Kipindi kinapofika, shughuli zote achia,
Daima fika haraka, Sunna kujifanyizia,
Kama zako nne raka, salama kutumizia,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Waheshimiwa wahusika, wazazi wetu na pia,
Mola pia katamka, katika Qur’an pia,
Nalo pia lahusika, ibada yako sikia,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Jamii inapasika, kusoma na kusikia,
Elimu isiyo shaka, moyoni ije tulia,
Kisha pasipo mashaka, muifundishe jamia,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Nane beti nimefikia, kalamu naachilia,
Misikitini kufika. Kumuabudu Jalia,
Peponi nipate tulia, Mola akiniridhia,
Tumche Mungu dawamu, Janna tupate tulia.
Wabillahi Taufiqi
Ustaadh Muhammed Ibn Hakika Machellah,
Almasjid Answary – Makonga,
P.O. Box 298,
Newala – Mtwara – TZ.
Mkwezi (jibu)
Kalamu ninaishika, kuandika gazetini,
Salamu kwa wahusika, wote wa ulimwenguni,
Bwanakheri msifika, jibu weka akilini,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Kwanza ninakupongeza, kwa kuhamia shambani,
Maisha unayaweza, bila ya purukushani,
Mungu atakuongeza, kwa mema ya duniani,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Mimi nilijiuliza, yametokana mageni,
Ya mkwezi kujikwaza, katikati mnazini,
Na nimepeleleza, jibu nimelibaini,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Tusibaki jiuliza, huyo ni mkwezi gani,
Tena wacha jiumiza, huo ni mnazi gani,
Hayo mambo ya Muweza, Muumba ulimwenguni,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Ni kweli na uhakika, mkwezi kwama mtini,
Anaweza salimika, na kushuka mnazini,
Kama ulivyotamka, lakufanya hulioni,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Usiende kwa waganga, wala hospitalini,
Bora nenda kwa Maganga, muulize kwa makini,
Mlingotini na Tanga, hayatokea kwa nini,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Bwanakheri tulizana, umuombe Bwana Mola,
Ndio jambo la maana, nahimiza hala hala,
Mkwezi mjuzi sana, kukwama jua ni hila,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Tamati nakamilisha, jibu hili lipokea,
Kama halijakutosha, usisite kunambia,
Zuberi sijachemsha, swali lako kutegua,
Bwanakheri omba Mungu, mkwezi tasalimika.
Zuberi Mohammed (Amiri)
Box 61428, Dar es Salaam.
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Majeshi ya nje kupelekwa Lesotho: Je, ni sera za Nguvumali?
Nyumba ya Wakfu yageuzwa Baa
Dar
Na Mwandishi Wetu
‘VAT’ yaingia Bakwata Same
Na Mwandishi Wetu
Mchungaji asema hakuna mihadhara ya
kashfa
Na Muhibu Saidi
Maoni yetu: Masheikh tupeni Fatwa
Safari yangu Ufini
Ustaadh Ka-Batembo
Unyanyasaji wa kidini mashuleni, vyuoni
ukomeshwe
Na Abuu Afahah
Wanaume toeni haki za wanawake
Na Zabibu Iddi Ng’onda Box 78, Mwadui
MAONI: Yesu ni yule yule Isa
Na Saleh Ngoi
Hatuna uwezo wa kuwapinga manabii
Na Elia Batendi, S.L.P. 538, DSM
Ukoloni mwingine unaingizwa
nchini?
Sheikh Thabit H. Mbago,S.L.P. 21486,DSM
Khatamy ni ‘Gorbacheiv’ mwingine?
Na Athman Rajab
Tufuate Uislamu kwa vitendo na siyo
kwa maneno
Mwandishi: Maalim Ali Bassaleh
AN-NUUR lina chuki na
Wakristo
Na Charles Kamuhabwa, DSA Mtwara
Msiiparamie ovyo Biblia
Na Sheikh Bernard P. Nyangasa
Yaliyosemwa na viongozi wa dini juu
ya idadi ya watu 1989
Na Rajab Rajab
Uislamu ulivyoingia Zanzibar -2
Waislamu Moro watakiwa kutoyumba
Na Rajab Rajab, Morogoro
Wanawake Masasi wawataka Masheikh
kutangaza sheria za Allah
Na Muhibu Saidi, Masasi
Ugaidi na Uislamu siyo kitu
kimoja – Sheikh Jongo
Na Bakari Musa
Sheikh Abbas awataka wananchi
Dodoma waepuke upuuzi
Na Abu Zubair, Dodoma
Vijana watakiwa kujiepusha
na ‘vijiwe’
Na Badru Kimwaga
Mafundisho ya Quran
Kutoa katika njia ya Allah: Al-Baqarah aya
261-263
Barua za wasomaji
Mashairi
Masomo ya dini ya Kiislam
Chakula na Lishe
Magonjwa yanayoathiri lishe
|