AN-NUUR 
Na.169 Jamadul Akhir 1419, Oktoba 2 - 8, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
 
Darsa la ndoa
 

Wanaume toeni haki za wanawake kuepusha ufisadi 

Chagua mchumba kwa Hadithi za Mtume wetu (saw)

Na Zabibu Iddi Ng’onda Box 78, Mwadui 

AWALI ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu (sw) kuwapa moyo Bi. Zuhra Tajiri na Halima Issa kwa makala zao katika gazeti hili kuchangia mada hii na kutupa ari wengine kuipapasa kwa kuguswa na ukweli uliopo. Mwenyezi Mungu awajazie kheri duniani na akhera. AMIN. 

Mimi katika mchango wangu pamoja na kukubaliana na yote waliyosema wenzangu naendelea kuwalaumu Masheikh, Wazazi na wenzetu wanaume kwa kuwaacha mabinti wanaadhirika hadi kuzaa nje ya ndoa na wenyewe wapo, mwisho kupatikana kizazi kisicho cha Kiislamu, kwa maana ya watoto wasio na msimamo wa dini kisha kudhoofisha Uislamu. 

Eee ndugu zangu Waislamu! Tuamke kuuendea Uislamu kikamilifu. Upande wa Masheikh kila siku wanahimiza swala, swala, swala tano. Al-hamdulilahi kwa jambo hili naweza kuwapa 90%. 

Lakini wameghafilika kabisa katika suala la ndoa. Wameshindwa kuwaelimisha vijana wetu na kuwakemea kwa bidii kama wanavyoamrisha swala. 

Vijana wanapotea na wao wapo. Kosa la kukaa na vimada na kuoa ndoa za serikali ndiyo limeshamiri na kuchanua kama maua. Hata wale wanaojaaliwa kuwa hawachagui mchumba kwa hadithi za Mtume (saw). Huenda Masheikh wetu wangelivalia njuga jambo hili la ndoa, hali isingekuwa kama ilivyo sasa ambapo kila mmoja anayo macho ya kushuhudia na masikio ya kusikia. 

Vijana au wanaume kwa ujumla wanachagua wachumba kwa kipengele kimoja tu kati ya vipengele vikuu vinne alivyoamrisha Mtume (saw) katika kuchagua mchumba, yaani uzuri basi! Ana nywele nyingi, ana macho mazuri, ana shingo ndefu akigeuka utapenda n.k. kuliko binti mcha Mungu. 

Matokeo yake ni hatari inayokuja baadaye kwa wengi ya kutokuelewana kwa kila hali kama mume huyo ni mcha Mungu, hivyo kushuhudia ndoa zikivunjika kila siku au mifarakano na watoto kubaki hawana maadili kwa kukosa malezi ya baba na mama katika Uislamu. 

Na hao watoto ndiyo tunaowategemea kuwa Masheikh wa kesho. Lau kama mume atavumilia na kubaki kuumia tu basi bado watoto hawatapata malezi ya Kiislamu kwa sababu mama ndiye mlezi mkuu anayekuwa karibu na watoto kila wakati. 

Kama yeye anatia dawa kichwani na bintiye atamruhusu na kumpamba kwa kila pambo akishapendeza ndiyo kwanza anamtuma mbali ili aonekane. Matokeo yake ni ufisadi na malezi ya mama huyo na kusababisha ummah wa Kiislamu kupotea, Lakini hayo yamesababishwa na wale wasiotaka kuoa wacha Mungu. 

Shime ndugu zangu Waislamu! Oeni wacha Mungu ambao ni wengi sana hasa katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza kama alivyosema Bi. Halima Issa. Na wengine ni wale wanaosilimu kutoka kwenye ukafiri na kuijia njia ya haki (din ya Mwenyezi Mungu) Uislamu. 

Je, hamuwaoni? Mnataka waolewe na nani? Hamjui kwamba mtaulizwa kesho mbele ya haki? Mtamjibu nini Mwenyezi Mungu enyi wanaume wa Kiislamu! Oeni hao mpate utulivu. Hamuwezi kupata utulivu bila kuoa wacha Mungu. Usipokuwa na utulivu katika ndoa yako hata hizo swala zako tano wanazozikazania Masheikh kwa bidii wakasahau utulivu. 

Na kama ni hivyo unategemea malipo gani kwa swala hizo mbele ya Mwenyezi Mungu? Hivyo viongozi wetu waamrishe swala ambazo ndiyo ufunguo wa peponi sambamba na mambo mengine kwani yote ni amri ya Allah (sw) na yanategemeana. 

Wazazi nao wamechangia kuathiri sanandoa za mabinti zao kwa kuwalazimisha kuolewa na wasiowataka ili hali binti ana haki ya kuchagua mchumba amtakaye. Hupelekewa tu bila kuchunguza mienendo ya hao waoaji na matokeo yake ni kama nilivyokwishasema. 

Enyi wazazi zindukeni! Waulizeni Masheikh na someni vitabu mpate mafundisho ya Mtume (saw) na mwenendo wa masahaba zake. Acheni kuona haya kufuata sunnah za Mtume (saw) hadi mnafikia kuwatokomeza mabinti zenu katika maasi. Hamjui hayo siku ya malipo? 

Kumuomba kijana amuoe binti yako ni suna wala si aibu hata kidogo kama mnavyodhani kuliko kusubiri tu ajaye ndiye huyo huyo bora mwanangu ameolewa au binti anakaa hadi anapata mtoto wa nje ya ndoa. Matokeo yake ni kama nilivyokwishasema. 

Angalia mafunzo haya ya Maswahaba. Sayidna Omar (ra) alimwendea Sayidna Abubakar (ra) kutaka amuoe mwanawe Bi. Hafsa, lakini hakumjibu kitu. Akamwendea Sayidna Uthman (ra) akakataa. 

Hapo Sayidna Omar moyo wake ukaharibika na kwenda kumshitakia Mtume (saw), Mtume akamtoa huzuni kwa kumwambia, "Hafsa ataolewa na mume bora kuliko Uthman, na Uthman ataoa mke bora kuliko Hafsa". Kipindi hicho Sayidna Uthman alikuwa katoka kufiwa na mkewe Bi Ruqaya mtoto wa Mtume (saw). Hivyo Mtume akamuoa Bi. Hafsa na Uthman akamuoa Bi. Umukulthum mwana mwingine wa Mtume (saw). Hapo ndipo Omar akafurahika kweli kweli. 

Baada ya hapo Sayidna Abubakar alimuomba raadhi Sayidna Omar na kumwambia aliwahi kumsikia Mtume (saw) kutaka kumposa Bi. Hafsa. Ila alishindwa kulisema hilo kwani alikuwa hajaruhusiwa. Naye Sayidna Uthman (ra) akamuomba radhi Sayidna Omar (ra) na kumweleza kuwa alikuwa na tamaa ya kuozeshwa binti wa pili wa Mtume (saw). Basi Sayidna Omar akawasamehe na kuishi salama katika kuuendeleza Uislamu hadi umetufikia sisi leo. 

Je, kati yetu ndugu zangu Waislamu kuna mbora kuliko Sayidna Omar (ra) aliyemtafutia bintiye mume? Na ambaye amebashiriwa pepo na Mtume (saw)? 

Hivyo wazazi na wanaume wa Kiislamu hasa vijana wetu yale makosa mliyokwishayafanya msiyarudie kamwe! Tufuate mafunzo ya Uislamu. Amesema Mtume (saw) "Mwanamke huolewa kwa mambo manne, dini yake (ucha Mungu), mali yake, uzuri wake na nasaba yake. 

Basi wewe jitwalie pato kwa mwenye dini. Usipofanya hivyo, fahamu mikono yako itapata mchanga (yaani utakorofika)". 

Mwisho nawahimiza mabinti kupitia gazeti letu tukufu la AN-NUUR kuanzisha kamati ya NUSRA, jitokezeni kwa wingi bila aibu kutafuta wenzi wenu mnaowapenda na watakaowafaa kisha kuwaelimisha wazazi wenu kwa upole ili tupate nusra na tuepuke lawama mbele ya Mwenyezi Mungu siku ya Qiyama kwa kufuata nyayo za Bi. Khadija (ra) vile alivyofanya kwa Mtume (saw). Haya wenzangu uwanja uko wazi! 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 TAHARIRI 
Majeshi ya nje kupelekwa Lesotho: Je, ni sera za Nguvumali? 

Nyumba ya Wakfu yageuzwa  Baa Dar 
Na Mwandishi Wetu 

‘VAT’ yaingia Bakwata Same 
 Na Mwandishi Wetu 

Mchungaji asema hakuna mihadhara ya kashfa 
 Na Muhibu Saidi 

Maoni yetu: Masheikh tupeni Fatwa 

Safari yangu Ufini 
Ustaadh Ka-Batembo 

Unyanyasaji wa kidini mashuleni, vyuoni ukomeshwe 
Na Abuu Afahah 

Wanaume toeni haki za wanawake 
Na Zabibu Iddi Ng’onda Box 78, Mwadui 

MAONI: Yesu ni yule yule Isa 
Na Saleh Ngoi 

Hatuna uwezo wa kuwapinga manabii 
Na Elia Batendi, S.L.P. 538, DSM 

Ukoloni mwingine unaingizwa nchini? 
Sheikh Thabit H. Mbago,S.L.P. 21486,DSM 

Khatamy ni ‘Gorbacheiv’ mwingine? 
Na Athman Rajab 

Tufuate Uislamu kwa vitendo na siyo kwa maneno 
Mwandishi: Maalim Ali Bassaleh 

AN-NUUR  lina chuki na Wakristo 
Na Charles Kamuhabwa, DSA Mtwara 

Msiiparamie ovyo Biblia 
Na Sheikh Bernard P. Nyangasa 

Yaliyosemwa na viongozi wa dini juu ya idadi ya watu 1989 
Na Rajab Rajab 

Uislamu ulivyoingia Zanzibar -2 

Waislamu Moro watakiwa kutoyumba 
Na Rajab Rajab, Morogoro 

Wanawake Masasi wawataka Masheikh kutangaza sheria za Allah 
Na Muhibu Saidi, Masasi 

Ugaidi na Uislamu siyo kitu kimoja – Sheikh Jongo 
Na Bakari Musa 

Sheikh Abbas awataka wananchi Dodoma waepuke upuuzi 
Na Abu Zubair, Dodoma 

Vijana watakiwa kujiepusha na ‘vijiwe’ 
Na Badru Kimwaga 

Mafundisho ya Quran 
Kutoa katika njia ya Allah: Al-Baqarah aya   261-263 

Barua za wasomaji 

Mashairi 

Masomo ya dini ya Kiislam 

Chakula na Lishe 
Magonjwa yanayoathiri lishe 
  

 

 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita