NASAHA
Na. 053 Jumatano Juni 21 - 27, 2000
Ukurasa wa mwanzo
Islam Tanzania
Matoleo yaliyopita
RIWAYA

Dunia ndivyo ilivyo - 3

Mtunzi: Marcussy G. Mzee 

Kumbuka ulivyonifanyia umnyama wako, uliniwekea dawa za usingizi kwenye soda kisha "ukanibaka"na uliendelea na mchezo wako huku ukinilaghai kwa pesa, mimi sisemi zaidi kama leo unanikana Mungu yupo atanilipia na ipo siku utaona aibu juu ya hii dunia kwani malipo ya dhambi ni mauti bali kalama ya Mungu ni uzima wa milele".Alilalama Mariam huku akitoa machozi. 

Mzee Tandara na mkewe Bi. Fatuma walikuwa wakiendelea vizuri na biashara yao ya kuuza vitumbua katika baraza ndogo ya nyumba yao ya nyasi, hukuwakiendelea kuweka pesa katika Benki ya Maendeleo vijijini, wakamshukuru Mungu huku wakikubaliana na ule msemo usemao "Mungu hamtupi mja wake",lakini ya Mungu vile vile ni mengi msichana Mariam alikuwa katika Tafrani nzito huko mjini bila wazazi kujua kinachoendelea kati yaMariam na mwajiri wake. 

Mkewe Mzee Kidazu alikuja juu kama moto wa kifuu baada ya kusikia habari ile nzito toka kwa Mariam, ulizuku ugomvi mkubwa, huku mkewe akimimina matusi na kashfa nzito kwa Mzee Kidazu huku akidai apewe Talaka yake aondoke ili amwache aishi na "house-girl" wake. Juu ya Mzee Kidazu kujaribu kujitetea mbele ya mkewe bado hakumsaidia kitu. 

Mariam akawa anafungasha nguo zake katika mfuko wake wa Rambo uliochakaa tayari kwa safari ya kurejea kijijini, alisindikizwa hatua chache kwa macho, kisha akageuka, akamtazamaMzee Kidazu kwa jicho la kisasi, kwa sauti ya huzuni akatamka "Mjomba! Kama kwangu limetota, kwa uwezo wa Mungu kwako litazama". Kweli dunia ndivyo ilivyo! Mariam akavuta hatua kuelekea stendi ya "Bus" tayari kurejea kijijini kwa wazazi wake. Hukum nyuma akiacha mzozo mkubwa kati ya Mzee Kidazu na mkewe kutokana na kitendo cha kishenzi alichokifanya kwa "House-girl" wao, lakini mzozo huo ukamalizwa kifamilia, mambo yakaisha kwa usalama maisha yao ya ndoa yakaendelea kama zamani. 

Mariam alipokelewa kwa furaha na wazazi wake wawili, lakini Mariam hakuwa na furaha yoyote aliyoionesha kwa wazazi wake, alikuwa ni mnyonge aliyegubikwa na mawazo tele kichwani lakini hali hii haikuwapa mstuko wazazi wake, kwani walijua vile ni uchovu wa safari. Baada ya salamu na maamkizi ndipo ilipodhihirika kwanini Mariam kwa muda ule yupo pale kijijini, Baba na Mama yake Mariam walisikitika sana kufuatia habari ile iliyomuhusu Mariam. 

Pesa zilizokuwa zikiwekwa Benki zilimfanya Mariam asiyaone maisha ya pale kijijini magumu kama alivyo yaacha mwanzoni, akawa anashirikiana na mama yake kupika vitumbua, siku moja Mariam alikaa chini ya mti wa mpapai huku amejiinamia akifikiria juu ya ule ujauzito, "wewe! Vipi unaumwa"? Alistuliwa na sauti ya mama yake "Hapana mama nimepumzika tu", "usifikirie sana mwanangu dunia ndivyo ilivyo". 

Hivyo ndivyo ilivyojihili hali iliyopelekea Mariam kurudi tena katika himaya na maisha ya kijijini, kisichoridhiki hakiliki kutokana na mwendo mzuri wa biashara ya vitumbua wanakijiji wengi wakaanzisha biashara hiyo na kufanya kipato kwa upande wa kina Mariam kishuke sana. Hivyo hali ya maisha yao ikarudi tena katika taabu kwani hata ile akiba ya Benki nayo ilikuwa ikipungua siku hadi siku. 

Muda ukafikia, Mariam akajifungua mtoto wa kiume mwenye afya njema. Mh! Hapo ndipo ilipodhihirika kwamba kila panapo ukweli uongo hujitenga! Mariam alitoa machozi kila alipomwangalia mtoto wake mzuri wa kiume ambaye amefanana sana na Mzee Kidazu mwishowe akajisemea " Mungu yupo". 

Mzee Tandara akarudia tena biashara ya kuuza kuni. Alitembea kilometa kadhaa kutafuta kuni, maisha yakawaelemea tena, huku Mariam akiendelea kumhudumia mtoto wake kwa taabu na mashaka matupu, akampa jina la Masumbuko. Juu ya matunzo duni aliyokuwa anayapata lakini aliendelea kukua vizuri, Masumbuko akafikia umri wa kwenda shule, akaanza shule, juhudi zake katika masomo zilileta mafanikio katika matokeo ya mtihani wake wa mwisho kwa kufaulu vizuri. 

"Sawa mwanngu juu ya kufaulu kwako nasikitika sana tena nina uchungu mkubwa moyoni sina uwezo wa kugharamia masomo ya sekondari, wewe mwenyewe unaona hali ya maisha yetu ilivyo, nitafanya nini mwanangu?" Maneno haya yalimchoma sana Masumbuko na kumfanya ajiinamie, kisha akamtazama mama yake, akamuuliza "Mama! Hivi Baba yuko wapi?" Swali hili likampa huzuni sana mama yake, kwa macho yaliyojaa huruma akamjibu kwa kumpa mkasa wote uliomkuta mpaka kuzaliwa kwake na kuwepo katika hali ile.... 

Kutokana na mambo yaliyomkuta mama yake, Masumbuko roho ilimuuma na akapata uchungu mkubwa, kweli duniani kuna watu wenye tabia mbaya tena wengine ni watu wakubwa wenye umri wa kutosha kutofanya upuuzi kama aliofanyiwa Mariam, mama. Hivyo Masu akaamua kumuaga mama yake kwenda mjini kutafuta kazi lakini kabla hajaondoka akapewa wosia na mama yake... 

Nyumbani kwa Mzee Kidazu maisha yaliendelea huku mtoto wao Jamila akiendelea na masomo ya sekondari, Jamila alikuwa Jamila haswa ameumbika vizuri akamvutia kila mtu, lakini hakutaka kupotezewa muda na mtu yeyote hasa wale wenye tamaa za mapenzi, lakini Waswahili husema "Ndege mjanja..... Jamila hakutaka kabisa kupotezea mudawa wale wenye uchu wa mapenzi kwa watoto wa shule. Mzee Kidazu na mkewe wanaafikiana kutafuta tena mtu wa kufanya kazi ndogo ndogo pale nyumbani, lakini safari hii linatolewa sharti na mkewe, kwamba mfanyakazi wa sasa asiwe msichana bali mvulana, kwa ajili ya kazi ndogo ndono isipokuwa kupika. 

Masumbuko anatelemka toka ndani ya Bus la "Yo Transport" katika stendi ya Ma-Bus Msamvu ,akashika njia inayoelekea katikati ya Mji wa Morogoro, alipokuwa katika maeneo ya jirani na kiwanda cha kutengeneza sabuni cha KOMOA huku akishangaa shangaa baadhi ya majengo, anastuliwa na honi ya gari kwa nyuma, alipotaka kugeuka tayari dereva alishafunga breki jirani kabisa na miguu yake, alipoangalia ndani ya gari akakutana macho kwa macho na mzee wa Makamo kiasi, na macho yao yalipokutana yalizungumza kitu fulani. 

Mzee Kidazu akafungua mlango wa gari, akamwita Masumbuko kwa sauti ya utaratibu "Wee kijana hebu njoo"! Masumbuko hakukawia akatii wito akamsogelea, na ikamtoka salam iliyo jaa hofu "Shikamoo!" Naye Mzee Kidazu akaitikia"Marahaba mtoto mzuri, je unaitwa nani, unatoka wapi?" "Mimi naitwa Masumbuko, natokea Mikese nimekuja hapa kutafuta kazi" alijibu huku akimuangalia usoni, kwa kweli walifanana, lakini hawakujuwana kwamba pale ni mtu na Baba yake, mambo hayo, akamchukua kwenye gari mpaka nyumbani. 

Juhudi za kufanya kazi pasipo uvivu kulimfurahisha sana mama Idd. Kwani hakupoteza hata sekunde moja bila kujishughulisha na kazi. Wakawa na uelewano mzuri sana na Jamila. Kutokana na Jamila kupenda kumtania kila mara wakati mwingine kusaidia baadhi ya kazi, lakini panapofuka moshi.....,Masu alijitahidi sana kuvikwepa vishawishi vya Jamila,ambaye alikuwa akifanya vituko vya kila aina hasa wanapokuwa wapo wawili tu pale nyumbani. 

Jamila alivutiwa sana uzuri wa jambo aliokuwa nao Masu, hali ya upole, unyenyekevu na tabasam lake vilimfanya Jamila aingie kichwa kichwa, lakini Masu aliogopa asije fukuzwa kazi bure. Ilifikia siku ya siku Masu akiwa chumbani kwake akibadilisha nguo kwani alitoka kukoga, akastukia Jamila ameingia ghafla na upande mmoja wa khanga, akafunga mlango kwa ndani hali aliyokuwa nayo ilimfanya Masu atetemeke akafumba macho kwa viganja vya mikono yake, katika vuta nikuvute wote wakajikuta kitandani, puu! 

Jamila akatoka huku moyo wakeu meridhika lakini Masu akabaki kitandani amejiinamia akijutia tendo lile, akajiuliza maswali mengi iwapo Mzee Kidazu atagundua, Mh! Masikini bila kujijua kumbe ni mtu na dada yake, aibu! 

Tabia ikajengeka ikaota mizizi, Masumbuko naye Aah! Kamchezo kakaendelea, lakini lililo na mwanzo halikosi mwisho, tahamaki Jamila akanasa, ujauzito, Juhudi za kutaka kuitoa nzikashindikana, siku zilivyozidi kwenda na mimba nayo ikaanza kujitokeza,na kupewa barua ya kufukuzwa shule. 

Mzee Kidazu alipopata habari ya kufukuzwa shule nusra apoteze maisha kwa "Pressure" akamwita Masumbuko, kilichofuatia hapo nikipigo kikali. Huku akitoa matusi mazito mazito. Mh! Mkuki kwa nguruwe....., Masu akatimuliwa kwa kutupiwa vitunguo zake chache zilizokuwemo kwenye kifuko cha Rambo, akashika njia na kuondoka huku akiwa na mawazo tele kichwani "Nitaenda wapi?" Wakati huu mji siuelewi vizuri, iwapo nitaishi bila kazi matokeo yake hayatakuwa mazuri nifanye nini mie?" Mwishoe akakata shauri kurudi kijijini kujisghughulisha na kilimo. 

Majira ya mchana wa jua kali sana kijana Masu akawasili kijijini kwao, akapokelewa kwa furaha na mama yake pamoja na Babu na Bibi yake, Masumbuko hakuficha kile kilichomsibu mpaka kufikia kurudi tena katika maisha ambayo alishaanza kuyasahau mama yake machozi yakamtoka, kwani tukio lile lilifanana na lililomkuta yeye, kisha akajiinamia kwa sekunde kadhaa mwishowe Masu akamwita mama yake "Mama! Usilie ukilia utaniliza na mimi, dunia ndivyo ilivyo ina mambo mengi yaliyopangwa na Sub-hana Mungu yupo na atatusaidia kwa haya yaliyotokea", kauli ya Masu inamtoa mama yake katika majonzi. Wakaanza kilimo kilicholeta faraja kwao. 

Nyumbani kwa Mzee Kidazu hali ya masimango na kejeli vilimuandama Jamila, hali iliyopelekea akose Raha, hali ya afya yake ikadhoofika sana, akamkumbuka sana Masu, akajiinamia huku machozi yakimtiririka, kuondoka kwa Masu ilikuwa ni huzuni tupu kwake, akakaa, akawaza sana mwishowe akafikia uamuzi wa kunywa sumu ili aepukane na adha toka kwa Baba yake. 

Akajifungilia ndani akachukua glassi ya maji akamimina sumu kali ya panya, akainyanyua glassi. Lakini kabla hajainywa nafsi ikamsuta na ikamuonya "Ole wao wale wanaodhurumu nafsi za roho zao na kuua, hawa wote siku ya kiyama Mungu hatowauliza kitu atawatia moja kwa moja katika shimo la moto wa Jehanamu". Sauti hii ilimpomjia, akairudisha glassi juu uya meza, msichana Jamila akaona ni afadahali apande "Bus" amfuate kipenzi chake Masu huko kijijini, kwani alikuwa tayari kwenda kuishi maisha ya aina yoyote. 

Ilikuwa ni safari iliyoashiria huzuni, na kwenda kuishi maisha ya dhiki ambayo hajayazoea, lakini alijipa imani ya ushindi, akapanda "Bus laYob-Transport tayari kwa safari ya kijijini Mikese, safari pevu ilikuwa mbele yake - kuishi mbali na familia yake baba na mama, kitu alichohisi kitakuwa kigumu sana kwake, lakini mambo yameharibika: mawazo yalimsumbua katika muda wote wa safari ile. 

Masumbuko na mama yake, wakiwa wameshika majembe mkononi wamechoka jua kali sana wanatoka shamba, ghafla Masu alistuka "Aaah! Jamila" akamkimbilia kwa furaha, akampokea mizigo, mabegi mawili yaliyojaa nguo, wakaongozana mpaka nyumbani, wakala chakula kwa pamoja, ndipo Masu akamfahamisha mama yake kuhusu Jamila, wakafurahi wakamkaribisha sana pale kijijini. 

Baada ya mapumziko mafupi, Jamila akaelezea hali halisi iliyomkuta, Masu na mama yake walisikitika sana, lakini mama Masu ndio lilimchoma zaidi, maisha yakaendelea vizuri huku Jamila akiizoea hali ya maisha ya pale kijijini. 

Nyumbani kwa Mzee Kidazu amani ikatoweka kwani mkewe amekuja juu anataka ajue ni wapi alipokimbilia Jamila, lakini Mzee Kidazu akamtamkia mke wake "kama unamtaka mwanao nenda mfuate huko alipo." Kuanzia sasa sitaki kusikia upuuzi wako wa kumuuliza Jamila." 

Muda wa mavuna ulipofika, familia ya Mzee Tandara ilifanikiwa kupata mavuno mazuri sana walipata maguni karibu hamsini ya mahindi na hususan ya mpunga kutokana na kilimo cha heka kumi za mpunga, kumi za mahindi, wakatenga kiasi kwa ajili ya chakula na kiasi kilichobakia walipeleka Morogoro kwa mauzo, wakapata pesa nyingi za kutosha. Masumbuko akajenga nyumba nzuri sana pale kijijini akafungua duka kubwa. 

Mzee Tandala akamwita Masu ili amueleze jambo la busara lenye hekima "Mjukuu wangu nilichokuitia hapa ni kimoja, fanya mpango ili tupeleke barua ya posa ili ufunge ndoa na huyu bint, sababu si vizuri kidini kukaa katika hali hii",baada ya maelezo hayo Masu alipata furaha moyoni, ikaandikwa barua akatumwa mshenga, akapanda bus kuelekea Morogoro. Maelezo aliyopewa yalimfikisha nyumbani kwa Mzee Kidazu bila wasiwasi. 

Mzee Kidazu kwa kutotaka kuiona tena sura ya Jamila pale nyumbani akaipokea barua ile ya uchumba kisha akatoa majibu haraka sana ya kulikubali ombi lile. Mshenga akaipokea barua ya majibu akafunga safari kurudi kijijini. 

Mipango na michango ya harusi ikapangwa haraka haraka nyumbani kwa Mzee Tandara pia nyumbani kwa Mzee Kidazu. Jamila akapanda Bus kuelekea Morogoro, huku tumbo likiwa tayari limeshajitokeza zaidi, akapokelewa vizuri na mama yake, siku mbili baadaye akapelekwa saloon kuandaliwa zaidi..... 

Masumbuko na nduguze Bibi, babu na mama yake wakajumuika na baadhi ya jamaa kuelekea Morogoro kumfuata mchumba wake, tayari kwa kufunga ndoa. 

Watu walikuwa wengi kweli kweli, nyimbo za kila aina ziliimbwa,masheikh wakatayarishwa kukamilisha lile lililokuwa likisubiriwa, lakini kabla hakujatendeka lolote, Umati wote wa wale ulistushwa na sauti kali ya mwana mama aliyesimama kuipinga ndoa ile, "Ndugu waalikwa, nasikitika sana kwa kuivunja au kuisitisha ndoa hii, kwani hao wanaotaka kufunga ndoa ni mtu na dada yake wa kuzaliwa kwa baba mmoja, hivyo sipingani na sheria ya dini, kama sheria inaruhusu watu hao waoane sawa", alisema mama Masu huku akilia kwa sauti, umati wote ukapatwa na mshangao mkubwa. 

Mama Masu akaelezea mkasa mzima kuanzia yeye mwenyewe alivyopewa ujauzito na Mzee Kidazu kisha akatimuliwa ndipo akazaliwa Masu, ambapo Masu naye akapata kazi ya ndani kwa Kidazu ibilisi akawaingia akatembea na Jamila mtoto wa Mzee bila kujua kuwa ni dada yake. Kilifuata kilio kwa Masu na Jamila ambaye alibakiza muda mchache kujifungua:"Mh! Yaani nazaa na kaka yangu?" Alijiuliza. 

Sheikh Mkuu Yahaya Omari Bawazir akachukua kipaza sauti na kuwaasa watu kwa kifupi, "Ndugu waalikwa bila shaka mmesikia kisa kizito kilicho pelekea ndoa isifungwe, hivyo hili liwe fundisho kwa wazee wengine wenye tabia mbaya kama alivyofanya Mzee Kidazu, tamaa yake ya kutembea na "House-girl" wake leo imeleta aibu hapa, jamani angalieni msihadaike na mambo ya dunia, naomba hili lisirudiwe tena hii ni fedheha kubwa kwa mzee mwenzetu, tabia hii ilaaniwe kabisa. Iwe fundisho kwa wengine wenye tabia mbaya mimi naishia hapa na Mwenyezi Mungu ayafikishe katika nyoyo zetu na tuyafuate, tusikengeuke. 

MWISHO. 

Juu
 

YALIYOMO
 
 

Tahariri
Uhuru wa kuabudu utiwe katika matendo bila ya ubaguzi

Kauli ya Sumaye yawakera wananchi

Licha ya Katiba ya nchi kutambua uhuru na haki ya kuabudu: Qur’an kizimbani

CCM yapata kiwewe

Wapinzani Waishutumu sheria mpya ya uchaguzi

Mtoto wa Afrika yutaabani

CCM wanatumia pesa za serikali kwa kampeni - Chenyenge

USHAURI NASAHA
Dhuluma haiondoki bila kubadili mfumo

Habari za Mikoani

Kalamu ya Mwandishi
Kweli CUF ni ngangari!

MAKALA
Manabii wa kale na mageuzi

MAKALA
CCM na sera za maendeleo

MAKALA
Wajibu wa wananchi kwenye uchaguzi mkuu

Habari za Kimataifa

Lishe
Kuhifadhi matunda kwenye jokofu

RIWAYA
Dunia ndivyo ilivyo - 3

MASHAIRI

MICHEZO

  • Uingereza, Ujerumani nje
  • Washabiki wamshangaa Mkapa, wambeza Sumaye
  • BMT waipiga ngwara FAT

  • -

       Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:Bonyeza hapa
    Au
    Andika barua  kwa: nasaha1420@yahoo.com

    Ukurasa wa mwanzo
    Islam Tanzania
    Matoleo yaliyopita