AN-NUUR 
Na.173 Rajab 1419, Oktoba 30 - Novemba 6, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
 
Tanzania tuna sera gani kuhusu kanda 

Na Abu Abdullah, Tanga 

WIKI iliyopita nilifanya safari mbili za kwenda na kurudi Dar es Salaam. Kila mara nilijaribu kupanda gari ambayo haina historia ya mikosi ya njiani. Pengine matajiri wao ni miongoni mwa wenye kutoa katika njia ya Allah (s.w.). 

Kanda ya video tuliyoanza nayo safari siku ya mwanzo ilionyesha vita kati ya Waarabu waliovaa vilemba na Wamarekani kwenye miji ya viunga vya Algeria, kufuatia kutekwa nyara kwa ndege ya Kimarekani na magaidi hao wa kubuni. 

Pamoja na kutumia magari ya deraya na kuwa wengi lakini magaidi walishindwa vibaya na Wamarekani waliokuwa na silaha chache na pikipiki ya kurushia makombora, moja tu. 

Madhumuni ya igizo hilo ililenga kuwadhalilisha Waislamu (wenye siasa kali) wanaoitwa magaidi kwa upande mwingine kuitukuza Marekani. Kanda hii haikunikera sana kwa vile niliamini ni uongo uliokuwepo usingeweza kuleta ushawishi ulio kusudiwa. Zaidi nilihisi kujenga dhana ya mapambano kati ya miamba miwili ya kifikra ya ulimwengu wa leo, yaani Uislamu na Marekani. 

Kana kwamba gari haiwezi kuendelea bila kanda ya aina yoyote, baada ya kumalizika kwa video hiyo "kondakta" aliyumba yumba mpaka akafika kuweka kanda nyingine ya radio. Makelele yake yasiyoeleweka yalitukera wengi. 

Ndo-mboloo. Ndo-mbo-loo. Mama yee. Maa ooo! Makelele ya namna hiyo kwa wengi tulihiyari ukimya, lakini hatukuwa na uchaguzi. 

Safari ya pili: Gari ya pili na ya tatu, kurudi na kwenda tena, nilipanda gari za shirika hilo hilo na mambo yalikuwa yale yale ya vita vita na vita vya mara hizi ni vya kikatili kweli kweli, vile vinavyoigizwa na watu wenye asili ya Kichina, akina Bruce Lee. 

Watu hawa hupenda sana kutumia vifaa vya ncha kali vyenye kuwaka na makucha yao kama ya wanyama mwitu kutoa damu na kuuana kiholela. Teknolojia za kisasa za kutengeneza picha na kuhifadhi sauti zinafanya iwe vigumu kutokuamini unayoyaona na kuyasikia. Wasafiri ambao ni wagonjwa huwa na muda mgumu sana mpaka wafike waendako. 

Mzee mmoja ambaye alionekana kutokea moja ya vijiji vya ndani ndani Tanga, hakuweza kufaidi vyema safari yake, kwani alitazamana na video hiyo na spika moja ilikuwa juu tu ya kichwa chake. 

Nilimuona akiuma vidole vyake kwa masikitiko karibu muda wote wa kanda hiyo, ambayo ukatili wake hautoi muda wa mtangazaji kupumua. 

Msafiri mwingine alidumu na kusikitika kwa kubana ulimi wake na ufizi wake wa juu na kutoa sauti za"T-ch, t-ch, t-ch " huyu mambo yalivyozidi aliamua kujificha kabisa nyuma ya kiti cha mbele yake. 

Nikaendelea kusoma haiba ya wasafiri wengine wenzangu, niliwaona wasafiri wengine wawili ambao yaelekea walikuwa ni mtu na mkewe, kwenye viti vya wawili wawili. Wao walionekana kupendelea kufaidi safari yao kwa kuangalia mandhari nzuri ya nchi, na kujulishana majina ya vijiji gari lilimopita. Hata hivyo walipata matatizo ya kusikizana vyema na utulivu wa kumbukumbu. 

Binafsi niliamua mara ya nne kupanda gari isiyokuwa na video wala redio. Nilibahatika isiyokuwa na video lakini isiyokuwa na sauti ya kanda haikuwezekana. Sauti za nyimbo hizo nilidhani ndizo za wale vibwengo niliokuwa nikisimuliwa utotoni, ambao pamoja na kuona maganda ya samaki aina ya kamba waliokuwa wakiwala kwenye mito ya bahari, lakini sikuwahi kuwasikia. Sauti zenyewe ni "Kwech –kwech – kwech yoo !!" na mifano yake, zenye kutia wazimu kichwani. 

Katika kuzidi kutafakari nikawakumbuka Twaleban wa Afghanistan ambao ili kuhifadhi dini yao ya Kiislamu, wamepiga marufuku vituo vyote vya televisheni mpaka vitakaporekebisha aina ya matangazo na picha zao. Sambamba na hilo wanaendesha msako wa kuzinasa kanda zote zisizokubaliana na Uislamu. 

Na sisi Watanzania hata kama sera za wa Afghanistan hatunazo, lakini tuna sera za kudumisha na kuleta amani. Sera hii nina uhakika haitakuwa na matunda yoyote kwa kuangalia kanda za waigizaji wauaji na ni lazima tutafute sera maalum inayokubaliana na sera ya amani.  
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 

TAHARIRI 
Wakipewa fursa watainusuru nchi

Wasomi watetea haki ya wananchi kumiliki ardhi

Serikali izungumze na wananchi–Mzee Gonga

Akina mama watakiwa kushikamana na dini yao

Maoni
Serikali inaWhite Paper:  Wananchi mna nini?

Dondoo za Saikolojia: Hoja kengeza
Na Abu Halima Sa Changwa

Makala ya mtangazaji
Khatamy sio Gorbacheiv!!!

Makala
Malipo ya fadhila
Na Mohamed Saleh

Tanzania tuna sera gani kuhusu kanda
Na Abu Abdullah, Tanga

Mdahalo kati ya Waislamu na Wakristo- 2
Na Nandenga wa Mkomidachi

Teknologia
Jifunze Kuunganisha Kompyuta (3)
Na Hassan Omar

Makala na habari
'Usiiparamie ovyo Theolojia'
Na Charles Kamuhabwa, DSA Mtwara

Mwinyimkuu kufanya sensa ya waumini Magomeni
Na Jamillah Nassoro

Same tusilimu upya

Wazazi Mwanza wahimizwa kuwashonea watoto wao Hijab
Na Idd Katimba, Mwanza

Tuwaige Wangazija, 'tutafanikiwa'
Mwandishi: Maalim Bassalah

Serikali imeweka rekodi ya kutisha – Sheikh Salim
Na Mwandishi Wetu

Muhadhara waunguruma Geita
Na Hussein Abdallah, Geita

Fuateni Sharia ya Allah - Sheikh
Na Badru Kimwaga

Wanawake wa Kiislamu Mburahati wahimizwa kutafuta elimu

Mafunzo ya Qur'an
Vijana wa pangoni

Barua za wasomaji 

Masomo ya dini ya Kiislam 

Chakula na lishe
Chakula ni silaha ya kukabiliana na changamoto ya kansa
Na Mujahid Mwinyimvua
 
 

 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita