AN-NUUR
Na.158 Rabi' Awal 1419, Julai 17 - 23, 1998
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
.SUALA LA MWEMBECHAI
  • Wabunge wataka kujua nani aliamrisha kuua
  • Wasema yalikuwa mauaji ya makusudi
  • Ulikuwa uvunjaji wa haki za binadamu
Na Mwandishi Wetu 

WABUNGE wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania wameitaka serikali ieleze ni nani alitoa amri ya kuuliwa wananchi pale Mwembechai. Aidha wabunge hao wanahoji ni hatua gani zimeshachukuliwa dhidi ya Polisi walioua na ni kwa nini serikali inakuwa na tabia ya ubalakala katika utendaji wake. 

Pamoja na hoja hizo wabunge wametaka ufafanuzi juu ya suala la kashfa na kusisitiza umuhimu wa serikali kuunda Tume ya uchunguzi juu ya Mauaji ya Mwembechai kwani mpaka sasa serikali haina maelezo yenye kueleweka. 

Akizungumza bungeni juzi Mbunge wa Konde, Mhe. Salim Ahmed Said alisema kwamba kwa taratibu za jeshi la polisi, polisi hawezi kufanya jambo bila ya amri, hivyo akataka kujua ni nani alitoa amri ya kuua pale Mwembechai, ni OCD, RPC, Mkuu wa Wilaya Kinondoni, Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam, IGP au Waziri? 

Katika kuonyesha jinsi gani haki isivyotendeka na kuwepo kwa uonevu na ubalakala Mhe. Salim alihoji na kushangaa kwamba ni vipi mbwa aliyeuliwa kule Sumbawanga alitetewa mpaka na Jaji hili la mauaji ya Waislamu linyamaziwe. 

Mheshimiwa Hashul Nassor Ali ambaye ni Msemaji wa Upinzani Wizara ya Mambo ya Ndani akilizungumzia suala hili alisema kwamba limelitia doa jeshi la polisi na kwamba imejenga chuki baina ya polisi na wananchi. Alisema kila aliyeangalia televisheni alishuhudia Afisa wa polisi akiamrisha "Piga yule na yule". Aidha alisema watu walishuhudia kwamba kijana yule aliyeuliwa na polisi alipoanguka alikuwa na jiwe dogo mkononi. 

"Ile ilikuwa ni ‘Cold Blood Murder’ ilifanywa makusudi na polisi", alisema Mhe. Hashul. 

Kuonyesha ubalakala (double standard) wa serikali alioanisha na pengine chuki yake dhidi ya Waislamu Mhe. Hashul alioanisha tukio hili la Mwembechai ambapo serikali imeua kwa madai ya kuzuia ghasia na polisi kuzidiwa nguvu na lile la Arumeru ambapo wananchi wa huko wapatao 5000 wakiwa na sime na mikuki walikabiliana na polisi, na haikutolewa amri ya piga yule. 

Sambamba na hilo Mhe. Hashul Nassor Ali alihoji juu ya suala la kashfa za kidini. Alisema Muislamu kusema Yesu sio Mtoto wa Mungu ndivyo hasa Qur’an yake inavyosema. Lakini akasema wapo wale Morani wa Arumeru wao wanasema kwamba kwaya na mahubiri ya Kanisa ni kelele zinazowanyima usingizi, na ni laana kwa mujibu wa mila zao. Na wamechukua hatua ya kuchoma moto makanisa, ili kuthibitisha kukerwa kwao. "Pale Mwembechai piga yule kwa risasi ilitekelezwa", lakini Arumeru polisi waliwakimbia wananchi waliochoma makanisa. 

Katika kusisitiza umuhimu wa kuundwa kwa Tume ya uchunguzi Mhe. Hashul alisema kwamba kwa mara ya kwanza Mhe. Waziri wa Mambo ya Ndani alisema vyama vya upinzani vinahusika. Baadaye nchi fulani za kigeni na baadaye mujahidina. Kwanza Mhe. Hashul alitaka kujua hawa Mujahidina ndio nani. Lakini katika hotuba ya Waziri wa Mambo ya Ndani Bungeni Mhe. Hashul amesema kwamba sasa inasemwa kwamba ni vyama vya kidini vilivyoandikishwa kwa nia njema. 

Ni kutokana na kujikanganya huko Wabunge wamesema kwamba ni muhimu uchunguzi ufanyike. Mbunge wa Kigamboni Mhe. Kitwana Kondo, amemtaka Waziri wa Mambo ya Ndani akafanye uchunguzi aje na kauli thabiti. 

Pamoja na nukta hiyo Mhe. Kondo alitaka kujua wale askari walioua wamechukuliwa hatua gani. Aidha Mhe. Kitwana Kondo alimhoji Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi juu ya askari wanaolinda msikiti wa Mwembechai hivi sasa. Hali ambayo amesema imesababisha msikiti kutokuswaliwa na darasa mbali mbali zilizokuwa zikiendeshwa msikitini hapo kusita. 

Zaidi ya hayo Mhe. Kitwana Kondo alionyesha masikitiko yake dhidi ya hatua ya Polisi kuwakamata wazee watu wazima –Mzee Chata na Mzee Katambo na kusema kwamba wanaofanya matendo haya ndio wasioitakia nchi yetu mema na wala sio yeye anayeiambia kweli serikali yake na viongozi wake. Na katika kuisherehesha nukta hiyo Mhe. Kondo akamhoji Mhe. Waziri wa Mambo ya Ndani kwamba, je!, haioni hatari mbaya ingetokea au wazee wale wangefia jela? 

Kuhusu suala la "Parole" Mhe.Kitwana Kondo ameshangaa ni kwanini Mhe. Ali Ameir anachukua muda mrefu kuiunda (kupata watu wa upande mwingine). 

Katika hilo akamshauri aige mfano wa Mtume Mussa (a.s.). Kwamba alipopewa utume aliomba apewe msaidizi kutokana na kuwa na kigugumizi. Na Mwenyezi Mungu akampa Haruni (a.s.). Sasa na yeye kama hawaoni wasomi Waislamu arudi kwa Rais aombe msaada atapewa akina Harun wanao wajua. 

Akichangia hoja hiyo ya Wizara ya Mambo ya Ndani Mbunge wa Magu,Mhe. John Cheyo alisema kwamba kinachogomba katika suala la Mwembechai na mengine ni matumizi ya nguvu yaliyokithiri na kusema kwamba hakuna amani bali ni uvumilivu wa wananchi na zaidi kwamba watu wanaogopa. 

Wabunge wengi waliochangia hoja hiyo wametahadharisha juu ya matendo ya askari yanayokiuka sheria kama vile kufanya upekuzi usiku, kuwatesa na kuwaua raia. Walisema hali hiyo inajenga uhasama na uadui baina ya polisi na raia. 

Awali katika hotuba yake Mhe. Waziri wa Mambo ya Ndani alisema kwamba suala la Mwembechai limesababishwa na vikundi vya kidini ambavyo vingine vimesajiliwa kisheria lakini vimejihusisha na mahubiri ya kashfa na chuki baina ya dhehebu moja na jingine au baina ya dini moja na nyingine. Na katika kujibu hoja za Wabunge Mhe. Waziri akasema kwamba hakuna haja ya Tume kwani kila kitu kinajulikana; kwamba kulikuwa na vurugu. Hata hivyo kuhusu vifo akasema kwamba bado majalada yanafanyiwa uchunguzi na Wizara ya sheria. 

  

Juu 
 

YALIYOMO
 
TAHARIRI  

Maoni yetu: Wananchi kataeni kupotoshwa 

SUALA LA MWEMBECHAI: Wabunge wataka kujua nani aliamrisha kuua 
Na Mwandishi wetu  

Katiba ya nchi yapuuzwa: Waislamu wapigwa marufuku kuhubiri  

Mtihani darasa la saba 1998: Manispaa Moro yaagiza ipewe majina ya wanafunzi Wakatoliki 
Na Rajab Rajab, Morogoro 

 “Wushu”ya Waislamu wa China na jinsi ilivyowasaidia kupambana na dhulma dhidi yao 
Na MUSSA ALLY  

Yesu wa kwenye Mathayo siyo Yesu wa kwenye Luka 
Na. Masoud Mohammed 

Ni nani hawa Waislamu wa Siasa Kali ? 
Na USTADH  A.S. FUNDI  

Waislamu tuondokane na unyonge 
Na Abubakar Marwilo 

Maisha ya ndoa kwa Mwislamu 

Waislamu wana mwelekeo wao 
Na Sheikh Pandukizi Dilunga 

Ni mwaka gani Yesu alianza kuitwa Mungu 
Na MCHUNGAJI A.T. MANONI  

Wanawake wameamua kuwa wazi kweli kweli 
Na Bi. Fatma Musa 

Kimya kingi kina mshindo mkuu: Vipi Mhe. Rais wale walioua? 
Na Mussa Ally 

Mtazamo wa madhalimu wa Tanzania kwa Waislamu 
Na Rajab Isa 

Aliyoyasema KK bungeni 

Waislamu mkoa wa Morogoro wampinga Yahya 
Na. Abu Adli  

Polisi wachafua mazingira ya msikiti wa Mwembechai 
Na Badru Kimwaga 

Wanawake wa Kiislamu Ubungo darajani wamuunga mkono Sheikh Bafadhil 
Na Kassim Juma 

Barua za wasomaji  

Mashairi  

Mafundisho ya Qur'an: Kanuni za kumkumbuka Allah na kutumia katika njia yake 

Masomo  

Chakula na lishe: Lishe ya mtoto aliyekuwa mgonjwa 
Na Mujahiid Mwinyimvua 
 

 

 

 

 
 Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita