|
|
|
Na. Abu Adli KUFUATIA tamko la Bakwata Makao Makuu Dar es Salaam la kumtaka Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Alhaj Omar M. Bafadhil ajiuzulu, Waislamu mkoani humo wametoa tamko la kupinga hatua hiyo. Waislamu hao wamesema kutokana na katiba ya Bakwata, Sheikh Omar amechaguliwa kihalali na Waislamu wa mkoa huo hivyo ataendelea na wadhifa wake hadi mwisho wa uhai wake. "Sisi sote tunaungana naye kwa khutuba yake aliyoitoa katika mkesha wa Maulidi ya kuadhimisha kuzaliwa mtukufu huko Bagamoyo", wamesema Waislamu wa mkoa huo katika tamko lao. Aidha, wamemtaka Sheikh Yahya Hussein aende mkoani humo ili apeleke takwimu ni maendeleo gani Bakwata imewaletea Waislamu hadi sasa. "Tunakutaka uje hapa ueleze toka Bakwata liundwe 1968 hadi 1998 kuna maendeleo gani ndani ya Uislamu miaka thelathini?", wamehoji Waislamu hao na kuwaomba Waislamu kote nchini waunge mkono tamko la Sheikh Omar kuwa kuna udhaifu katika Bakwata na ikibidi wafanye maandamano ya amani kwa pamoja kuliunga mkono tamko hilo. Tamko hilo pia limedai kuwa Yahya Hussein siyo Bakwata na kwamba yeye ni Balukta na alikuwa mpinzani mkubwa wa Bakwata na sasa anaendeleza uadui wake akiwa ndani ya Baraza hilo. Wakati huo huo, Sheikh Omar Bafadhili amesema kwamba hana muda wa kujibizana na Yahya Hussein magazetini kwani kwa kufanya hivyo atakuwa amejivunjia hadhi yake kwa waumini. Sheikh Omar aliyasema hayo nyumbani kwake alipokuwa akiongea na mwandishi wa habari hizi mwishoni mwa wiki. "Siko tayari kujibizana na Yahya, yeye anafahamu Sheikh na mjumbe wa
Kamati ya Maulamaa Taifa wana hadhi na wajibu gani ndani ya Bakwata kulinganisha
na watendaji wa kawaida", alisema Sheikh Bafadhil bila kufafanua.
Na Badru Kimwaga POLISI wafanyao doria maeneo ya msikiti wa Mwembechai wamelalamikiwa kwa kuchafua majengo yaliyozunguka msikiti huo. Wakitoa malalamiko yao, wakazi wa maeneo ya jirani wamedai kuwa askari hao wanaolinda eneo hilo yapata miezi mitano, tangu kutokea vurugu, huwa wakijisaidia haja ndogo ndani ya majengo ya msikiti huo, yaliyo nyuma ya msikiti, pembezoni mwa banda la kuuza vinywaji liitwalo Uroja wa Kiunguja, na majengo mengine ambayo hayajamalizwa kujengwa. Wakiongea kwa kuficha majina yao, wakazi hao wamesema kuwa wamekuwa wakiwashuhudia askari hao wakiwa katika sare zao pamoja na silaha zao, wakigeuza majengo hayo kama. Wakazi hao wameongeza kusema kuwa imeonekana mipira ya kiume (kondom) nje ya chumba wanacholalalia kisicho na mlango hali ambayo wamedai kuwa inatia wasiwasi kwamba eneo hilo la ibada huenda limegeuzwa kuwa danguro. Lakini baada ya wenye msikiti kuhoji, juzi majira ya jioni, mkuu wa maskari hao, ambaye Mwandishi hakuweza kumtambua akiwa ndani ya Hyundai TZM 3445, aliwasili eneo hilo na tangu siku hiyo, askari hao wameacha kulala katika chumba hicho. Haieleweki kama mkuu huyu aliwasili eneo hilo kikazi au alikuwa katika jitihada ya kufuatilia malalamiko hayo. Askari hao ambao wako eneo hilo tangu wavamie msikiti wa Mwembechai na kuua watu wanne,wamedaiwa kuwa kero kwa wakazi wa hapo. Uvamizi wa polisi Msikiti wa Mwembechai umeathiri sana mipango ya Ibada
ikiwa ni pamoja na kupungua kwa idadi ya waumini.
Na Kassim Juma WANAWAKE Waislamu wa Msikiti wa Ubungo Darajani Jijini wameunga mkono hotuba ya Sheikh Bafadhil aliyoitoa mjini Bagamoyo hivi karibuni. Wakizungumza kwa niaba ya wenzao, wanawake sita ambao walifika katika ofisi ya gazeti hili Mtaa wa Mahiwa Kariakoo Jijini mwishoni wa wiki iliyopita, wamesema Sheikh Omar ni mfano wa kuigwa na masheikh wengine nchini. "Sisi wanawake wa Msikiti wa Ubungo tunamuunga mkono Sheikh Omar Bafadhil kwa sababu amezungumza mambo ya msingi kwa Waislamu", walisema kwa pamoja akina mama hao. Aidha walishutumu kauli ya Sheikh Yahya Hussein iliyomtaka Sheikh Bafadhil kujiuzulu kwa madai ya kuiumbua Bakwata hadharani. Hotuba ya Sheikh Omar katika mkesha wa Maulid mjini Bagamoyo, imeibua mijadala miongoni mwa Waislamu sehemu mbali mbali nchini. Katika hotuba yake hiyo pamoja na mengine aliyoyazungumza, Sheikh Omar
aliitaka Bakwata kubadili mwenendo ilionao sasa wa kuwa mbali na Waislamu
badala yake iwe mtetezi na msemaji wa haki za Waislamu nchini.
|
Maoni yetu: Wananchi kataeni kupotoshwa SUALA LA MWEMBECHAI: Wabunge
wataka kujua nani aliamrisha kuua
Katiba ya nchi yapuuzwa: Waislamu wapigwa marufuku kuhubiri Mtihani darasa la saba 1998: Manispaa
Moro yaagiza ipewe majina ya wanafunzi Wakatoliki
“Wushu”ya Waislamu wa China
na jinsi ilivyowasaidia kupambana na dhulma dhidi yao
Yesu wa kwenye Mathayo siyo Yesu wa
kwenye Luka
Ni nani hawa Waislamu wa Siasa Kali
?
Waislamu tuondokane na unyonge
Waislamu wana mwelekeo wao
Ni mwaka gani Yesu alianza kuitwa
Mungu
Wanawake wameamua kuwa wazi
kweli kweli
Kimya kingi kina mshindo mkuu:
Vipi Mhe. Rais wale walioua?
Mtazamo wa madhalimu wa Tanzania
kwa Waislamu
Waislamu mkoa wa Morogoro
wampinga Yahya
Polisi wachafua mazingira
ya msikiti wa Mwembechai
Wanawake wa Kiislamu Ubungo
darajani wamuunga mkono Sheikh Bafadhil
Mafundisho ya Qur'an: Kanuni za kumkumbuka Allah na kutumia katika njia yake Chakula na lishe: Lishe ya
mtoto aliyekuwa mgonjwa
|