AN-NUUR
Na.158 Rabi' Awal 1419, Julai 17 - 23, 1998
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
S.L.P. 55105, SIMU 181365, DSM
TAHARIRI
Mauaji ya Mwembechai , kimya cha Rais kina tafsiri gani?
Kama tulivyowahi kusema awali damu ya Muislamu haiwezi kumwagika bure bure tu na wala "kisasi" (5:45) hakiwezi kuondoshwa kwa kuifukia damu ya Muislamu kwa mchanga. 

Suluhisho hapa ni wahusika na mauaji yale kufikishwa mahakamani. Mahakama ndiyo itakayoamua kwamba walikuwa na hatia au la. 

Uhai wa mtu ni kitu kitakatifu ambacho hakiwezi kuchezewa ovyo ovyo na ndio maana hata Katiba ya nchi imeweka kifungu maalum kinacholinda uhai wa watu. Na kwa ajili hiyo basi, mtu akiua hata kama ni kwa bahati mbaya lazima atafikishwa mahakamani. 

Na ni kwa sababu hiyo hiyo, Askari haruhusiwi kuchukua sheria mkononi na kumuua jambazi au mhalifu yeyote. Na ndio sababu vile vile wale Askari kule Arusha waliowaua watuhumiwa wa ujambazi walikamatwa na kamati za uchunguzi zikaundwa. 

Waliomuua marehemu Imran Kombe ni polisi wa Serikali na walikuwa kazini. Hata hivyo kwa vile Katiba na Sheria za nchi zinaheshimu na kulinda uhai wa raia; askari polisi wale hawakuhamishwa kituo cha kazi wakapelekwa Musoma au Sumbawanga, Bukoba au Mbeya ili kuwaficha mbali na ndugu wa marehemu. Walikamatwa na wakafikishwa mahakamani. 

Kuna watu wameua pale Mwembechai. Tena kwa kuamriwa "piga yule"; "mwongeze" na "yule". Damu ikamwagika. Wananchi wakashuhudia damu ya Muislamu yule ikifukiwa kwa mchanga. Aliyesema piga yule alionekana na anajulikana na aliyeitikia amri ya piga yule anajulikana pia. 

Katiba ya nchi inalinda uhai wa Raia. Qur’an inasema kosa la kuua ni zito sana kiasi kwamba mtu akiua mtu mmoja huhesabiwa kana kwamba kaua watu wote. 

"Kwa sababu ya hayo tukawaandikia wana wa Israel ya kwamba atakayemuua mtu bila ya yeye kuua mtu, au bila ya kufanya fisadi katika nchi, basi ni kama ameua watu wote, na mwenye kumwacha mtu hai (kumsaidia kuishi) ni kama amewaacha hao watu wote. Bila shaka Mitume waliwafikia na hoja zilizo wazi; kisha wengi katika wao baada ya haya walikuwa waharibifu sana katika nchi (5:32)" 

Na ili kulinda uhai; watu waovu wasimwage damu ya wengine bila ya sheria, Qur’an ikasema: 

"Enyi mlioamini! Mmepewa ruhusa kulipa kisasi katika waliouawa – Muungwana kwa muungwana, na mtumwa kwa mtumwa, na mwanamke kwa mwanamke. Na anayesamehewa na ndugu yake chochote basi ashikwe kulipa kwa wema; na yeye alipe kwa ihsani. Hiyo ni tahafifu itokayo kwa Mola wenu na ni rehema.Na atakayeruka mipaka baada ya haya, basi yeye atapata adhabu iumizayo (2:178). 

Kwa hali hiyo basi; kwa kuzingatia Katiba ya nchi na mafundisho ya Uislamu suala la Damu ya Waislamu iliyomwagika pale Mwembechai haliwezi kuisha kwa damu yao kufukiwa mchanga na wahusika kuhamishwa vituo vya kazi. 

Kuwaficha katika miji inayodhaniwa hakuana vugu vugu la wafiwa si ufumbuzi. Wauaji hawa popote waendapo harufu ya damu waliyomwaga inawafuata. 

Tungependa tusisitize kwamba Damu ya mtu haiwezi kumwagwa bure bure na mambo yakaisha kwa kuifukia kwa mchanga. 

Watu wameua hapa; wafiwa tupo tunawaona. Hawa ni lazima wafikishwe mahakamani. Vinginevyo tunatafuta kusababisha balaa katika nchi. 

Pamoja na yote hayo lipo tatizo kubwa linawatatiza Waislamu. Kimya cha Mheshimiwa Rais tafsiri yake nini! 

Tumeelezwa kwamba alitoa maelekezo watu waachiwe na wengine wapewe dhamana. Tena basi maelekezo yenyewe hayakutekelezwa kwa wakati na hatuoni hatua zozote kuchukuliwa. Hili linatia wasiwasi kwani hatuelewi ni vipi agizo la Rais laweza kukiukwa. 

Katika kutatizika huko tunashindwa kuelewa endapo taarifa za kuuliwa Waislamu zilishafika kwa Rais na zenyewe kazitolea maelekezo gani. Kule Arumeru tumesikia Mhe. Rais kaamua kuwafidia wananchi ambao ng’ombe wao waliuzwa kwa amri ya mahakama. Kasikia kilio chao japo wananchi hao wako mbali sana na Ikulu. 

Hiki cha kuuliwa Waislamu Mwembechai Rais mbona kimya!! 

Juu 
 

YALIYOMO
 

TAHARIRI 

Maoni yetu: Wananchi kataeni kupotoshwa

SUALA LA MWEMBECHAI: Wabunge wataka kujua nani aliamrisha kuua
Na Mwandishi wetu 

Katiba ya nchi yapuuzwa: Waislamu wapigwa marufuku kuhubiri 

Mtihani darasa la saba 1998: Manispaa Moro yaagiza ipewe majina ya wanafunzi Wakatoliki
Na Rajab Rajab, Morogoro

 “Wushu”ya Waislamu wa China na jinsi ilivyowasaidia kupambana na dhulma dhidi yao
Na MUSSA ALLY 

Yesu wa kwenye Mathayo siyo Yesu wa kwenye Luka
Na. Masoud Mohammed

Ni nani hawa Waislamu wa Siasa Kali ?
Na USTADH  A.S. FUNDI 

Waislamu tuondokane na unyonge
Na Abubakar Marwilo

Maisha ya ndoa kwa Mwislamu

Waislamu wana mwelekeo wao
Na Sheikh Pandukizi Dilunga

Ni mwaka gani Yesu alianza kuitwa Mungu
Na MCHUNGAJI A.T. MANONI 

Wanawake wameamua kuwa wazi kweli kweli
Na Bi. Fatma Musa

Kimya kingi kina mshindo mkuu: Vipi Mhe. Rais wale walioua?
Na Mussa Ally

Mtazamo wa madhalimu wa Tanzania kwa Waislamu
Na Rajab Isa

Aliyoyasema KK bungeni

Waislamu mkoa wa Morogoro wampinga Yahya
Na. Abu Adli 

Polisi wachafua mazingira ya msikiti wa Mwembechai
Na Badru Kimwaga

Wanawake wa Kiislamu Ubungo darajani wamuunga mkono Sheikh Bafadhil
Na Kassim Juma

Barua za wasomaji 

Mashairi 

Mafundisho ya Qur'an: Kanuni za kumkumbuka Allah na kutumia katika njia yake

Masomo 

Chakula na lishe: Lishe ya mtoto aliyekuwa mgonjwa
Na Mujahiid Mwinyimvua

 

 

 

 
 Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita