Mashairi
Wababe wakitawala
Kinyume kamwe hawezi, dhalimu kitawalia,
Kufanya mambo azizi, yenye kuwafiki njia,
Mwendo wao tangu enzi, si "huyu" kajianzia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Hujivalisha murua, mbele wakawaijia,
Mpate kuwachagua, kwa kura kuwapigia,
"Thumma" utu hujivua, viti wakishakalia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Si wema wa kutawala, japo wametangulia,
Kutenda mambo jamala, hilo tawasingizia,
Walipo wakisha "kula", lengo limetimilia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Ndugu zetu mlo Nzasa, si peke mnaolia,
Ni sote yametugusa, pamoja twaugulia,
Halipo mlilokosa, hayo kuwaangukia,
Ndiyo shukuruani yao, "wababe" wakitawala.
Kuchomewa maskani, bila kuwahurumia,
Wana na wenu wandani, peupe mkabakia,
Mmefanyiwa uhuni, Mola atawalipia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Tadhani nyie si watu, tena si wao raia,
Hamna thamani katu, wala kitu kuchangia,
Yamewafika wenzetu, na sisi yanatujia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Haya hayatakuwako, macho kuyaangalia,
Watu kupeana heko, kwa kuwadhuru raia,
Kweli "wachamungu" wako, viongozi Tanzania!
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Tunapata taawili, maana inatimia,
Uliowazi ukweli, utawala wa sheria,
Hizi ndo zake dalili, cheche zinaturukia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Nchi mejaa amani, ndo wimbo twausikia,
Utulivu mesheheni, hawana khofu raia,
"Wakubwa" oneni soni, kuongopa si murua,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Nzasa wa kwenu mkasa, wahika umetwingia,
Twajua hiyo ni posa, harusi inafatia,
Baada ya ninyi hasa, wapi wataelekea!
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Chonde tusikanganyike, kuubaini udhia,
Ndiyo staili yake, serikali ya sheria,
"Ucha Mungu" dira yake, vile walivyotwambia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Mwinyi tunamkumbuka, kusema alipatia,
Si punde yameshafika, mboni zayashuhudia,
Yanatupata mashaka, kwa dhuluma kuzidia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Alikuwa wa huruma, utu alizingatia,
Kwa pupa "hakutarama", ni mwenda wa kurudia,
Kimya chake cha hekima, "ruhusa" akipimia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Thibitini msilie, nyoyo zisije kuvia,
Hadhari mshikilie, na Mola kumlilia,
Rais si wenu nyie, ndo shari kuwafikia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Muwe na subira njema, wa Nzasa twawausia,
Msijione yatima, Mola atawakidhia,
Wababe wana khatima, kufuzu si yao njia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe"wakitawala.
Wako wapi madhalimu, uungu walojitia,
Nao waliishi humu, wakawatesa raia,
Siku zao zilitimu, seuze hawa "mikia",
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Mola mpenda witiri, Muumba hii dunia,
Twakuomba ya Qahhari, waja kuwaangalia,
Pitisha yako qadari, yote umeshuhudia,
Ndiyo shukurani yao, "wababe" wakitawala.
Jihad R. Saballa, S.L.P.47, SHINYANGA.
Mauaji Mwembechai
Msalikheri salamu, nazituma gazetini
Ugweno Raa Simbomu, Shime yangu pokeeni
Imenisibu hatamu, AN-NUUR fikisheni
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Sio nakumbusha donda, bali damu yavuvia,
Wametwacha vidonda, damu tumezifukia,
Waliotaka kushinda, harufu wametwachia,
Waloua Mwembechai wahusika tokezeni.
Waumini twakumbusha, wajibu ukumbukeni
Duniani wanakesha, raha yetu vilioni,
Wanaua na kutisha, Mwembechai kumbukeni,
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni,
Ukasuku uacheni, waandishi wambieni,
Wahariri hakikini, maovu yafichueni,
AN-NUUR gazetini, jamii iambieni,
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Iogopeni shilingi, inapoteza amani,
Tutaviruka vigingi; Mwembechai unganeni,
Tumewapoteza wengi, kwa risasi motochini,
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Wawapi kina Malima; Af'stani na Sudani,
Kwa machungu mnasema, tunateswa dunaini,
Wamagharibi twasema, dawa yetu ijikoni,
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Bendera zenu za vuma, dunia shuhudieni,
Ya Marekani mwasema, ya nyumbani hamneni,
Kuimbe UKWELI wauma, "(unaumiza moyoni)",
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Piga huyu piga yule, sote tulishuhudia,
Ngumi zikiwa kelele, wakubwa chanzo mwajua,
Msiipishe simile, u-ngwana kujisemea,
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Mwembechai na Manyema, wazee tuwe pamoja,
Ubungo, Mwenge, Musoma, Mtambani Mtakuja,
Shinyanga Moshi twasema, wito wa Ponda twangoja,
Waloua Mwembechai, wahusika tokezeni.
Yasini S. Mussa,
UGWENO,
KILIMANJARO.
|
YALIYOMO
Maoni
Kuwa na mawazo ya kufugwa tunajidharaulisha
Sakata la
mabucha ya Nguruwe kuibuka upya
Na Mwandishi Wetu
Kondom sio
kinga ya Ukimwi
Bakwata
yairushia polisi makombora Ngaramtoni
MACHO YA
SHUTUMA
Na Abu Halima Sa Changwa
Serikali
yatakiwa iwachukulie hatua wauaji
Na Mwandishi Wetu
Historia
ya Msikiti wa Ngaramtoni
Silaha yetu
ni kura ya pamoja
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington
DC U.S.A
Anuani
ya fikra
Na Abu Halima Sa Changwa
Kuukaribisha
mwezi mtukufu
Tunahitaji
"UN' ya Waislamu!
Na Said Rajab
Kongamano
la wanawake wa Kiislamu Newala lafana
Umuhimu
wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo - 2
Na Ustaadh Kupa Pazi Said
Kesi
mojawapo ya mihadhara yafutwa
Wasaidieni
watoto wenye vipaji - Prof. Kilonzo
Mahafali
ya kidato cha nne Thaqafa: Wazazi wakumbushwa wajibu wao
Wanafunzi
Mwanza wadai haki za kuabudu mashuleni kwa usawa
Na Iddi M. Katiba, Mwanza
Saidianeni
katika shida - Sheikh Abdallah
Waislamu,
Wakristo Rufiji watakiwa kuunda umoja
Someni
muiokoe jamii kimaadili
Acheni
Shirki
Kesi
nyingine ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa
Na Muhibu Said
Kusilimu
kwa Wakristo kwaleta kero Mwanza
Nzasa
waomba msaada wa chakula, madawa
Katibu
wa Bakwata Moro ang'olewa Msikitini
Masomo
ya Dini ya Kiislamu
Barua
za Wasomaji
Mashairi
Chakula
na lishe
[Umuhimu wa chakula katika
shule za awali] |