AN-NUUR 
Na.176 Shaaban  1419, Novemba 20 - 26, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Umuhimu wa chakula katika shule za awali
 

Na Mujahid Mwinyimvua. 

KATIKA makala hii neno shule ya awali linamaanisha kituo cha kuwalelea/kuwasomesha watoto wadogo ambao hawajaanza elimu ya msingi (darasa la kwanza mpaka la saba kwa Tanzania). 

Katika vituo vya shule ya awali, mara nyingi watoto huwa na umri kati ya miaka 2 mpaka 6 au zaidi kidogo. Umri huo ni muhimu sana kwa maendeleo ya mtoto, kimwili na kiroho. 

Chakula kina nafasi kubwa ya kumjenga mtoto kimwili, na wengine wanasema hata kiroho. Kwa hiyo, umuhimu wa chakula katika vituo hivyo ni jambo lililowazi. 

Hata hivyo, kwa vile bado kuna baadhi ya shule za awali hasa madrasa na wazazi ambao wanaona kuwa swala la chakula katika vituo vyao si muhimu na litaongeza gharama, makala hii imelenga kuwazindua watu wa aina hiyo ( wanaosita kuwapa watoto chakula) na kuielimisha jamii kwa ujumla juu ya dhana ya chakula katika shule ya awali. 

Chakula tunacho kula kina faida kubwa moja, nayo ni kutupatia virutubisho (nutrients). Hivyo virutubisho vina kazi kubwa tatu. 

Kazi ya kwanza ni kujenga mwili. Kwa mfano, sote tuna jua kuwa binadamu kwa hali ya kawaida huzaliwa na baba na mama. Anapozaliwa huwa mdogo na hapo tunamwita mtoto mchanga. Baada ya miaka kadhaa huwa mkubwa na kuweza kufanya mambo yake mwenyewe. Mwanaadamu kama huyo anaweza kuongezeka umbo, kutoka mtoto na kuwa mkubwa kwa sababu ya virutubisho vinavyotokana na vyakula tunavyokula. 

Kazi ya pili ya virutubisho ni kuupa mwili nguvu na joto. Mambo au kazi mbalimbali zinazofanywa na binaadamu zinawezeshwa na nguvu (energy) inayotokana na virutubisho. Kutembea, kuongea, kulia, kubeba mizigo, kusoma, n.k. ni baadhi tu ya kazi hizo. 

Kazi ya tatu ya virutubisho ni kulinda mwili usipate magonjwa. 

Ulaji duni na magonjwa ni sababu kubwa zinazosababisha vifo vingi kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano katika nchi hasa za ulimwengu wa tatu ikiwemo Tanzania. 

Kwa mfano, taarifa ya shirika la Umoja wa Mataifa linalojishughulisha na mambo ya watoto (UNICEF) ya mwaka 1990 inaonyesha kuwa watoto 176 kati ya watoto 1000 wanaozaliwa Tanzania hufa kila mwaka kabla ya kutimiza umri wa miaka mitano. 

Ni muhimu watoto katika shule ya awali (madrasa, chekechea, n.k.) wapatiwe chakula cha kutosha, safi na salama na kilicho mlo kamili (balanced diet). Hii ni kwa sababu baadhi yao wanatoka nyumbani bila kula chakula chochote na wengine wanakaa mbali, wanapoteza muda mwingi njiani kabla ya kufika nyumbani. 

Katika kutayarisha chakula cha watoto wa shule ya awali, mwalimu au mlezi lazima azingatie mafungu makuu ya chakula yafuatayo: 

Chakula cha kujenga mwili 

Chakula cha aina hii ni muhimu sana kwa watoto wa shule ya awali. Hii ni kwa sababu mwili wake (pamoja na akili) unahitaji kujengeka na kukua. Mfano wa vyakula vinavyojenga mwili ni kama vile maziwa, nyama, samaki, mayai, senene, ndege, maharage, choroko, soya, njegere, karanga n.k. 

Chakula chenye kuupa mwili nguvu na joto 

Watoto hufanya shughuli mbalimbali kama vile kucheza, kusoma, kukimbia, n.k. ili mwili uweze kumudu kazi hizo na zile za kujenga mwili, lazima mwili upate vyakula vyenye kutoa nguvu, mfano wa vyakula hivyo ni mchele, viazi, mahindi, mtama, ndizi, karanga, alizeti, samli, siagi, asali, mihogo, kweme, n.k. 

Chakula cha kulinda mwili 

Chakula hiki husaidia kulinda mwili wa mtoto asipatwe na magonjwa mbalimbali. Mfano wa vyakula hivyo ni kama vile mbogaa mboga (mboga za majani, nyanya, karoti, n.k.) na matunda mbalimbali, embe, machungwa, mananasi, papai, ubuyu, ukwaju n.k.) 

Zaidi ya makundi hayo ya vyakula, watoto wa shule za awali lazima wapatiwe maji safi na salama kwa mfano yaliyochemshwa na kuchunjwa na kuhifadhiwa katika chombo safi. 

Ni matarajio yangu kuwa makala hii imekidhi haja iliyokusudiwa. Hivyo basi wenye shule za awali na wazazi na jamii kwa ujumla tuendelee kutoa chakula bora na maji safi na salama kwa watoto wetu na wale ambao bado hawajaanza kutoa huduma hiyo waanze sasa, la sivyo tuaathiri ukuaji na elimu ya watoto wetu 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
Maoni 
Kuwa na mawazo ya kufugwa tunajidharaulisha 

Sakata la mabucha  ya Nguruwe kuibuka upya 
Na Mwandishi Wetu  

Kondom sio kinga ya Ukimwi 

Bakwata yairushia polisi makombora Ngaramtoni 

MACHO YA SHUTUMA 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Serikali yatakiwa iwachukulie hatua wauaji 
Na Mwandishi Wetu 

Historia ya Msikiti wa Ngaramtoni 

Silaha yetu ni kura ya pamoja 
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC  U.S.A 

Anuani ya fikra 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Kuukaribisha mwezi mtukufu 

Tunahitaji "UN' ya Waislamu! 
Na Said  Rajab 

Kongamano la wanawake wa Kiislamu Newala lafana 

Umuhimu wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo - 2 
Na Ustaadh Kupa Pazi Said 

Kesi mojawapo ya mihadhara yafutwa 

Wasaidieni watoto wenye vipaji - Prof. Kilonzo 

Mahafali ya kidato cha nne Thaqafa: Wazazi wakumbushwa wajibu wao 

Wanafunzi Mwanza wadai haki za kuabudu mashuleni kwa usawa 
Na Iddi M. Katiba, Mwanza 

Saidianeni katika shida - Sheikh Abdallah 

Waislamu, Wakristo Rufiji watakiwa kuunda umoja 

Someni  muiokoe jamii kimaadili 

Acheni Shirki 

Kesi nyingine ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa 
Na Muhibu Said 

Kusilimu kwa Wakristo kwaleta kero Mwanza 

Nzasa waomba msaada wa chakula, madawa 

Katibu wa Bakwata Moro ang'olewa Msikitini 

Masomo ya Dini ya Kiislamu  

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Umuhimu wa chakula katika shule za awali]  

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita