AN-NUUR 
Na.176 Shaaban  1419, Novemba 20 - 26, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Kuukaribisha mwezi mtukufu
 

Mwenyezi Mungu (s.w.) anatufahamisha kwamba: "Enyi mlioamini mmelazimishwa kufunga (swaumu) kama walivyolazimishwa waliokuwa kabla yenu ili mpate kumcha Mungu". (Qur. 2:183). 

Maneno haya matukufu yana mafunzo makuu matatu. Kwanza, kufunga ni amri wala si jambo la hiari. Pili, kutokana na maslahi yanayopatikana katika funga, maslahi ambayo ni muafaka kwa maumbile ya binadamu, amri hii pia inawahusu wanadamu waliokuwepo kabla yetu. Tatu, tunafahamishwa kuwa, kwa kuitekeleza amri hii tutalifikia lengo la kuumbwa kwetu. Lengo ambalo tusingelifahamu bila ya kuelimishwa na Mwenyezi Mungu (s.w.) pale alipotuambia kuwa: 

"Sikuwaumba majini na wanaadamu ila wapate kuniabudu" ( Qur’an 51:56) 

Ni vipi Mwenyezi Mungu (s.w) anatutaka tumuabudu katika mwezi wa Ramadhani? Je, hii ina maana kuwa katika miezi mingine ya mwaka hatutakiwi kumuabudu/kumtii Mwenyezi Mungu (s.w.)? 

Jawabu la swali la kwanza tutalipata katika toleo namba 4 la mfululizo wa makala hizi kuhusu funga ya Ramadhani. Ama jawabu la swali la pili ni kuwa, tunatakiwa kumuabudu/kumacha Mwenyezi Mungu (s.w.) kwa masaa yote 24 ya kila siku na katika kila kipengele cha maisha yetu kwa mwaka mzima. Pili tunatakiwa kumcha Mwenyezi Mungu kwa juhudi zetu zote hata mauti yatukute tukiwa Waislamu wa kweli. 

"Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu kama ipasavyo kumcha; wala msife isipokuwa mmekwisha kuwa Waislamu kamili". (3:102) 

Na katika kumtii Mwenyezi Mungu tunatakiwa tusichague baadhi ya mambo na kuacha mengineyo, bali, ni kufuata amri zote au kwa maneno mengine ni kutii kila kipengele kilichopo katika maisha yetu. 

"Enyi mlioamini! Ingieni katika hukumu za Uislamu zote, wala msifuate nyayo za shetani; kwa hakika yeye kwenu ni adui dhahiri". (2:208) 

Kama utaratibu wa kumuabudu Mwenyezi Mungu (s.w.) ndio huu, inakuwaje Allah (s.w.) atuamrishe kufunga Ramadhani ili tupate kumuabudu? Kuna hekima gani katika mwezi wa Ramadhani tofauti na miezi mingine? 

Jawabu ni kuwa, katika mwezi wa Ramadhani tunapewa/kutunukiwa nafasi ya pekee. Nafasi ambayo kama tutaitumia ipasavyo itatusaidia kulifikia lengo la kuumbwa kwetu kwa urahisi zaidi. Kuhusu kheri zinazopatikana ndani ya mwezi wa Ramadhani, Nabii Muhammad (s.a.w.) anasema: 

"Mwezi wa Ramadhani ni mwezi wa Mwenyezi Mungu ambao ameujaza Rehma, Baraka na Msamaha". 

Na pia ni ukweli usio na shaka kuwa, kwa kutokuzingatia taratibu za mwezi wa Ramadhani tutakuwa ni wenye kuipoteza tunu hii, hivyo, kwa wenye hasara kubwa duniani na akhera. 

Mwezi wa Ramadhani unatupa nafasi ya kuanza maisha mapya na kujiwekea malengo bora zaidi kwa mwaka ujao. Endapo utakuwa umebahatika kuifahamu tunu hii na kuitekeleza ni kheri kwako. Endelea na ongeza juhudi. Na endapo utakuwa huifahamu tunu hii, basi hujachelewa bado, wakati ni huu; utumie na usiupoteze. 

Yanayofaa kujiandaa 

Tujipe mazoezi ya funga za sunnah kwa mfano: Jumatatu na Alhamisi, masiku meupe, masiku ya kiza na nyinginezo nyingi. 

"Aysha (r.a.) amesimulia kuwa Mtume wa Allah alikuwa akifunga (katika mwezi wa Shaabani) mfululizo mpaka tuseme hatafungua tena; na aliacha kufunga mfululizo mpaka tuseme hatafunga tena; na sikumuona Mtume wa Allah akifunga mwezi mzima, ila mwezi wa Ramadhani na sikumuona anafunga mwezi mwingine zaidi kuliko alivyokuwa akifunga mwezi wa Shaabani. (Muslim) 

Tujiandae kwa mahitaji muhimu katika mwezi wa Ramadhani kama vile; futari, daku, sadaka, zakatul-fitri na mengineyo muhimu. 

Tujiwekee malengo la kutekeleza ibada za ziada (sunnah) zilizotushinda mwaka uliopita, pia tujiwekee malengo ya kutekeleza majukumu muhimu maishani kwa mwaka unaofuata. 

Tahadhari: Tusijiwekee malengo mengi ambayo yatatushinda kutekeleza. Tujiwekee malengo makuu mawili au moja ili tutakapofanikisha tupate motisha ya kujiongezea mengine. 

Tujiwekee nia ya kutorudia tena kwenye maasi. Mtume wa Allah (s.w.) amesema: "Yeyote anayedhamiria kufanya jambo jema lakini hakufanikiwa kulifanya, anaandikiwa malipo (kama aliyefanya). (Bukhari na Muslim). 

Tujiweke vema na jamaa, ndugu au majirani ambao ilitokea hitilafu baina yetu. 

Tufuatilie mapema kalenda ya Kiislamu ili siku ya kuanza kufunga isitukute kwa mshtuko au kama ajali. 

Kwa kifupi tujiandae kwa kutekeleza yale yote yanayomfurahisha Mwenyezi Mungu; na tujiepushe kabisa na yote yasiyompendeza Allah (s.w.) 

Yasiyofaa katika kujiandaa 

Tuepukane na pumbao zote kama vile; kununua karata mpya ama kupangusa vumbi karata zilizosahaulika, kutafuta madrafti na kuyapaka rangi, kutafuta bao, kete, dhunna, kanda za mipasho (taarabu), manyanga na vigoma vya kula daku, na kadhalika. Michezo yote hii ni haramu; haifai, kwa sababu ni ya kupumbaza akili tu, na kumfanya binadamu asahau kushughulikia mambo yaliyo muhimu katika dunia na akhera yake. 

Tusijiandae kupandisha bei bidhaa muhimu zinazohitajika katika mwezi wa Ramadhani. Tupunguze bei kwa kukusudia kutoa sadaka nyingi. 

Tusijiandae kwa vunja jungu. Tunawezaje kukaribisha neema kwa kumkasirisha anayetuletea? Tukimkadhibisha anayetaka kutuzawadia ni vipi tunarajia zawadi kutufikia? Wenye tabia hii ya vunja jungu ni wale wanaokusudia kulifinyanga upya baada ya mwezi wa Ramadhani. Yaani wale wanaokusudia kurudia tena upotovu. 

Kwa maoni, maswali au mapendekezo, tafadhali tuandikie: 

Waandishi (Funga ya Ramadhani), 
S.L.P. 296, 
Arusha - Tanzania. 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
Maoni 
Kuwa na mawazo ya kufugwa tunajidharaulisha 

Sakata la mabucha  ya Nguruwe kuibuka upya 
Na Mwandishi Wetu  

Kondom sio kinga ya Ukimwi 

Bakwata yairushia polisi makombora Ngaramtoni 

MACHO YA SHUTUMA 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Serikali yatakiwa iwachukulie hatua wauaji 
Na Mwandishi Wetu 

Historia ya Msikiti wa Ngaramtoni 

Silaha yetu ni kura ya pamoja 
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC  U.S.A 

Anuani ya fikra 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Kuukaribisha mwezi mtukufu 

Tunahitaji "UN' ya Waislamu! 
Na Said  Rajab 

Kongamano la wanawake wa Kiislamu Newala lafana 

Umuhimu wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo - 2 
Na Ustaadh Kupa Pazi Said 

Kesi mojawapo ya mihadhara yafutwa 

Wasaidieni watoto wenye vipaji - Prof. Kilonzo 

Mahafali ya kidato cha nne Thaqafa: Wazazi wakumbushwa wajibu wao 

Wanafunzi Mwanza wadai haki za kuabudu mashuleni kwa usawa 
Na Iddi M. Katiba, Mwanza 

Saidianeni katika shida - Sheikh Abdallah 

Waislamu, Wakristo Rufiji watakiwa kuunda umoja 

Someni  muiokoe jamii kimaadili 

Acheni Shirki 

Kesi nyingine ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa 
Na Muhibu Said 

Kusilimu kwa Wakristo kwaleta kero Mwanza 

Nzasa waomba msaada wa chakula, madawa 

Katibu wa Bakwata Moro ang'olewa Msikitini 

Masomo ya Dini ya Kiislamu  

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Umuhimu wa chakula katika shule za awali]  

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita