AN-NUUR
Na.165 Jamadul Awwal 1419, Septembe 4 - 10, 1998
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Ugaidi ni ugaidi, hata wa Marekani ni ugaidi 

Na Maalim Ali Bassaleh 

KAMA tunakubali kuwa kuzipiga mabomu Balozi za Marekani, hapa Dar es Salaam na kule Nairobi, yaliyoua pamoja na kujeruhi watu wasio na hatia, ni kitendo cha ugaidi na kinachostahili kulaaniwa; basi hatuna budi kukiri pia kuwa kuzishambulia Sudan na Afghanistan, na kuua pamoja na kujeruhi raia wa nchi mbili hizo wasio na hatia, nacho ni kitendo cha kiharamia, kinachopasa kulaaniwa na kila yule anayejali utu na kuheshimu misingi ya haki za binadamu. 

Marekani inadai kuwa kikundi cha kigaidi kinachoongozwa na tajiri mmoja aitwaye Usama bin Laden, aliye mafichoni nchini Afghanistan, ndicho kinachohusika na ulipuaji wa balozi zake. Lakini inafaa tujiulize swali moja. Kuna tofauti gani baina ya kitendo hiki kilichofanywa na Marekani na kile kinachodaiwa kufanywa na bin Laden? Kama kuna tofauti yo yote ile, baina ya vitendo hivyo viwili, basi labda iwe ni kwamba ule ugaidi wa mwanzo ulifanywa na kikundi cha watu wasiokuwa na huruma na maisha ya wanadamu wenzao; na huu ugaidi wa pili umefanywa na serikali ya nchi isiyojali kabisa uhai wa binadamu wengine wasio Wamarekani. 

Inavyoonekana ni kuwa Marekani inajali zaidi uhuru wa watu wake. Katika kulinda maisha ya Wamarekani, Marekani ipo tayari kuhatarisha uhuru wa maisha ya watu wengine. Potelea mbali wengine wateketee lakini Wamarekani wapone. Huenda hii ikawa ndiyo sababu iliyowapelekea wananchi wa Kenya kulalamika kuwa wakati wa zoezi la kuokoa waliojeruhiwa na lile bomu lililolipuliwa kule Nairobi, vikosi mbalimbali vya uokoaji vilikuwa vimeshughulika kuokoa watu wa jinsi zote; lakini waokoaji wa Kimarekani waliwaokoa wenzao tu. Na wala hawakuwa tayari kutoa msaada kwa watu wa jinsi nyingine yo yote. 

Hakuna mwanadamu aliyemstaarabu, na anayethamini roho za wengine awezaye kufurahia ulipuaji mabomu unaoangamiza roho za watu wasio na hatia. Aidha, hakuna anayeshabikia kuuliwa Wamarekani, Wazungu, Waafrika au Waarabu; kwani wote hao ni wanadamu. Roho ya mwanadamu ni yenye thamani kubwa, inataka ithaminiwe na ilindwe kwa hali yoyote. Kitendo cha kuua binadamu, wasio na hatia, ovyo, kwa kisingizio cho chote, hakikubaliki. Qur’an Tukufu inasema: "…atakayemwua mtu bila ya yeye kuua mtu, au bila ya kufanya ufisadi katika nchi, basi ni kama amewaua watu wote …" (Al Maidah 5:32). 

Kwanini Qur’an Tukufu iseme hivyo? Naam, ni kwa sababu Uislamu unawaona wanadamu wote ni kama ndugu wa familia moja. Kwa hivyo kumfanyia ukatili mmoja wao ni sawa na kuwafanyia ukatili wote. 

Zilipolipuliwa balozi za Marekani na kusababisha vifo vya watu 257 na kujeruhi wengine zaidi ya 5000, sote, kwa umoja wetu, tulilaani vikali kitendo hicho cha kikatili. Serikali zetu za Tanzania na Kenya, zimekuwa zikitoa ushirikiano mkubwa kwa wapelelezi wa Kimarekani, wa FBI, katika jitihada za kuwasaka wale wote wanaohusika na uharamia huo. Tulidhani Marekani itaonyesha ustaarabu; itasubiri mpaka uchunguzi umalizike, iwajue waliohusika, iwatie mkononi, kisha iwakabidhi kwa vyombo vya sheria vinavyohusika; ili sheria ichukue mkondo wake. Lakini wapi! Wakati uchunguzi unaendelea, tayari Marekani inazishambulia Sudan na Afghanistan kwa makombora na kuua raia wasiohusika. Tendo hili ni la uonevu na ni la aibu kubwa sana; hasa linapofanywa na nchi kama Marekani. Tusijidanganye, ugaidi ni ugaidi, ufanywe na Ireland au ufanywe na Marekani! 

Marekani ni taifa kubwa, lenye nguvu nyingi. Ni taifa lenye kuogopewa na kuheshimiwa. Na serikali ya nchi hiyo ndiyo iliyo mstari wa mbele kuona demokrasia inatekelezwa duniani kote na kwamba haki za binadamu zinaheshimiwa. Iweje basi nchi kama hiyo ivuke mipaka ya nchi yake na itumie nguvu zake za ziada kwa kuzishambulia nchi nyonge na dhaifu, zisizoweza hata kujilinda wenyewe? Tuseme huku ndiko kuheshimu haki za binadamu? Au hii ndiyo demokrasia anayoisimamia Marekani ulimwenguni? Mwenye nguvu mpishe! Bila ya shaka hii ndiyo ile demokrasia ya wanyama mwitu; mkubwa kumrarua mdogo! 

Bwana Kofi Annan, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameipinga hatua hiyo iliyochukuliwa na Marekani. Kwa sababu imekwenda kinyume kabisa na sheria za kimataifa. Kama Marekani ilikuwa ina ushahidi wa madai yake ilikuwa iwasilishe swali hilo mbele ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, ambalo Marekani ni mjumbe wa kudumu na ina kura ya Veto humo, ili lijadiliwe na kutolewa maamuzi ya pamoja. Na hata kama itataka kuyapinga maamuzi yatayotolewa itaweza kufanya hivyo kwa kutumia ile kura yake ya turufu. Mbona Marekani ilipotaka kuiadhibu Iraq, kwa kuivamia Kuwait, ililipeleka swala hilo Umoja wa Mataifa na ikapata kibali cha kuitekeleza azma yake hiyo? Je! Leo imekwisha sahau kuwa kuna Umoja wa Mataifa, na hali Makao Makuu ya Umoja huo yapo katika ardhi yake nayo ndiyo inayogharimia fedha nyingi zaidi katika bajeti ya kuendesha taasisi hiyo? 

Senetor Don Coasts wa Indiana, kutoka chama cha Republican, amesema Rais Bill Clinton kwa wakati huu, aliokumbwa na kashfa za ufuska hakuwa na hadhi ya kuamrisha shambulio kama hilo alilolifanya. Maneno haya yanaonekana kutilia uzito madai ya nchi nyingi za Kiislamu kuwa Rais Clinton aliamrisha kushambuliwa Sudan na Afghanistan ili kujaribu kuzima ile kashfa inayomkabili nyumbani, ambayo ilikuwa imemwangushia hadhi yake. Kwa vyovyote vile hapakuwa na sababu sahihi ya kujichukulia sheria mkononi mwake wakati vyombo vya kisheria vya kimataifa vipo na vinaweza kushughulikia jambo hilo. Kwa nini kuamrisha wakombora yasiyo na macho kwenda kuua vikongwe, wanawake na watoto wadogo? Tunaambiwa kombora moja, bila ya kukusudiwa, limedondokea Pakistan, katika jimbo la Baluchistan na kuua wanavijji watano na kujeruhi wengine. 

Tunaiambia Marekani, kama kweli inapinga ugaidi wa mtu au kwa vikundi vya watu basi, pia, apinge na ugaidi unaosimamiwa na nguvu za dola (State terrorism)! Isije ikawa kama walivyosema Waswahili: "Mkuki kwa nguruwe, kwa binadamu unaua!" 
 

Juu 
 

YALIYOMO
 
 
TAHARIRI 
HAKI YA KUABUDU MASHULENI: Hoja ya uwingi isizuie haki ya wachache 

Aliyeandika Yesu si Mungu bado akabiliwa na kesi 
Na Mwandishi Wetu 

Wazazi walia na Mkuu wa shule Mkwawa 
Na Mwandishi Wetu, Iringa 

Serikali iache kudhulumu  Waislamu - Bakwata  
Na Mwandishi Wetu

KESI YA MIRATHI: Hukumu ya Jaji Agostino yatupwa 
Na Mwandishi Wetu 

Sumaye sasa atoa ‘waadhi’ Msikitini 
Na Mwandishi Wetu, Arusha 

Sekondari ya Kiislamu Sumbawanga, mtihani kwenu – Sheikh Akilimali 
Na Harun Rashid, Sumbawanga 

37 wasilimu  Mwanza 
Na Mwandishi Wetu, Mwanza 

Akamatwa kwa kusoma gazeti la ANNUUR ! 

MGOGORO WA CHWAKA NA MARUMBI: Serikali ya Dk. Salmin itafute ufumbuzi 
Na Mwandishi Wetu, Pemba 

MAPENDEKEZO YA KATIBA YA SHIRIKISHO LA TANZANIA - 4 

Kwa nini walengwa wa mabomu wawe ni Marekani? 
Na Maalim Ali Bassaleh 

Profesa amekosea kusema kwamba... 
Na A.M. Hamza 

Ugaidi ni ugaidi, hata wa Marekani ni ugaidi 
Na Maalim Ali Bassaleh 

Dhana ya Udugu wa kiislamu 

UGAIDI: Chanzo si magaidi, ni dhuluma ya Marekani 
Na HASSAN KIMANGALE 

Jengeni familia bora 
Na Abuu Said, Iringa 

Tuwasaidie Waislamu kielimu na kiuchumi - Bi Zuhura 
Na SAID RAMADHANI KISSIMBA 

Tumieni uhuru wenu vyema 
Na Abuu Zaina, Iringa 

Hoja za kutofautisha Yesu na Issa ni udhaifu,  ni uzushi mtupu! - 4  
Na Muhibu Said 

Mihadhara ya Wakristo yatawala Handeni 
Na Mwandishi Wetu, Handeni 

Ziara ya Kadinali Pengo Moro  
Na Mussa Ally, Morogoro 

Aonyesha ujuzi wa kutengeneza Trekta 
Na Mwandishi Wetu 

Waislamu wasizifanye sharia za dini kuwa nzito – Sheikh Mzonge 
Na Ashraf  Yusuf, Moshi 

Sengerema waomba msaada 
Na Idd Katimba, Mwanza 
 
Mafundisho ya Quran 

Barua za wasomaji 

Mashairi: 

Masomo ya dini ya Kiislam 

Chakula na Lishe 
Matunzo ya mtoto mwenye lishe duni 

Matangazo 
 
 

 

 

 

 
 Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita