|
|
Hatimaye Mzee
Katambo, Chata waachiwa
WAZEE wawili waliowekwa rumande kwa miezi kadhaa wameungana na familia zao baada ya AN-NUUR kufichua kupuuzwa agizo la Rais kulikofanywa na baadhi ya wahusika. Kwa takriban miezi mitano, Mzee Chata Abdallah na Mzee Katambo walisota mahabusu hatimaye wameachiliwa huru ikidaiwa kwamba hawana shitaka la kujibu. Mzee Chata Abdallah ambaye ni Imamu wa Msikiti wa Mtambani aliachiwa huru mchana wa Ijumaa, Julai 3, Mzee Mussa Katambo aliachiwa Julai 6. Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari, mwendesha mashitaka wa Polisi alidai mbele ya Hakimu Ligema kuwa washitakiwa hao wamefutiwa shitaka na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DPP) baada ya kuona hawana kesi ya kujibu. Kukamatwa kwa wazee hao kulifuatia hatua za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Luteni Makamba kuitikia kilio cha Paroko Lwambano wa Kanisa Katoliki Mburahati kuhusiana na suala la mihadhara. Wakiwa rumande pamoja na watuhumiwa wengine wa kadhia ya Mwembechai, taarifa zinafaamisha kwamba Rais alitoa agizo ambalo lilitaka wahusika wawaachie huru wazee wote, wanawake na wanafunzi. Hata hivyo pamoja na kuwepo kwa agizo la Rais, wazee hao waliendelea kusota rumande katika gereza la Segerea huku wakipata mateso na madhalilisho ya kila namna. Akiongea na mwandishi wa habari hizi nyumbani kwake Mwananyamala kwa Msisiri, Mzee Chata alisema kwamba, alikamatwa nyumbani kwake Februari 10, 1998 saa 5 asubuhi na askari watatu walivalia kiraia. Alipelekwa kituo cha polisi Oysterbay kisha kituo kikuu (Central) ambapo kote alidaiwa kufanya mhadhara bila kibali na kuwakaribisha watu wa mhadhara katika msikiti anaoungoza, walilala kituo cha polisi ambapo kesho yake walipelekwa mahakamani na kisha kurundikwa Keko. Huko amesema walikuwa wakivuliwa nguo bila kujali umri wao kwa madai ya kupelekuliwa. Pamoja na kuvuliwa nguo mara kwa mara amesema walikuwa wakipigwa sana virungu na kupewa adhabu mbalimbali. Akitoa mfano, alisema yeye pamoja na kuvimba na kuumwa miguu alikuwa akilazimishwa kuchuchumaa wakati hawezi. Alisema ilibidi akinge kifua awaambie askari hao bora wampige risasi. Alisema pamoja na watuhumiwa kuugua maradhi mbalimbali kama upele, vifua, tumbo na magonjwa mengine, lakini wote walikuwa wakipewa Panadol, Aspro na Asprin. Mzee Chata Abdallah alizaliwa mwaka 1922 huko Rutare, Ujiji mkoani Kigoma. Alisoma Madrasa (ya juu) mwaka 1929 hadi 1938 huko Tabora. Muda wote amekuwa ni mwanachama hai wa TANU na CCM. Amewahi kuwa mjumbe wa Halmashauri ya TANU ya Wilaya ya Igunga na mkoa wa Tabora. Amekuwa Diwani kati ya mwaka 1968 hadi 1976 akawa Katibu Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni. Hivi sasa ni Imamu Mkuu wa Msikiti wa Mtambani, wilayani Kinondoni. |
Maoni yetu: Prof. Juma Kapuya, vipi Muislamu usijue agenda za Waislamu? Hatimaye Mzee Katambo, Chata waachiwa
Sheikh Bafadhil aitaka Bakwata iwe
mtetezi wa Waislamu
Makala: Uinjilisti wa Mbuni haufai
Mussa Katambo: Mzee aliyewekwa rumande kwa kuandaa mihadhara Makala: Elimu ya ngono yapenyezwa
tena Zanzibar
Arusha wasema: Hongera Mhe. KK kwa
kuwa mfano mwema
Wanawake Songea kuandaa maonesho
Kesi ya mgogoro wa Ardhi
AN-NUUR marufuku
gerezani?
Waislamu Karagwe wadai kusalishwa
na imamu asiyejua kutawadha
Ofisi mpya za Rabita
|