AN-NUUR
Na.154 Safar 1419, Juni 19-25, 1998
 
Home 

Links 

Islam Tanzania 

Matoleo ya nyuma 
 
 

Sheikh wa Wilaya Same ahimiza Waislamu kushiriki tamasha

Na Mwandishi Wetu 

SHEIKH wa Wilaya ya Same Sheikh Mohamed Mustafa amewahimiza Waislamu wa Wilaya ya Same kushiriki tamasha la ujenzi wa Chuo cha Kiislamu huko Kirinjiko, Mwembe. Tamasha hilo ambalo litawahusisha Waislamu wa nchi nzima litaanza June 26, hadi Julai 3, 1998. 

Akizungumza katika swala ya Ijumaa Juni 12 mjini Same Sheikh Mohamed Mustafa alisema kwamba chuo hicho ni kwa manufaa ya Waislamu wote. 

Katika kutoa nasaha zake Sheikh Mustafa amesema kwamba kitu chochote kizuri ni kigumu upatikanaji wake. Ni cha kuhangaikia. Akasema hata Mtume (s.a.w.) alipata taabu katika kuueneza Uislamu kwahiyo akawasihi Waislamu wa Same wasikate tamaa kutokana na ugumu unaoambatana na ujenzi wa Kirinjiko 

Aliwaambia kwamba wanachotakiwa wao ni kufanya juhudi na kutoa michango yao na hata kama umri wao utakwisha kabla ya chuo kukamilika jaza yao wataipata kwa Mola wao na wengine wataendeleza kazi hiyo. 
 
 
 

Sheikh awataka wanawake wajistiri 

Na Badru Kimwaga 

IMAMU Mkuu Msaidizi wa Msikiti wa Manyema, uliopo Kariakoo, jijini, Sheikh Abdulrahman , amewataka Waislamu nchini kuwakemea mabinti na wake zao, kutembea bila kuzingatia sheria na maamrisho ya Mwenyezi Mungu. 

Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki, alipokuwa akihutubia waumini wa Msikiti wa Mwinyimkuu, uliopo Magomeni Mapipa, jijini Dar es Salaam kwa kusema kuwa wazazi wa Kiislamu, hasa wanaume wanatakiwa kuwaasa wake na mabinti zao, kujistiri miili yao ili kuweza kuepusha vishawishi vinavyopeleka wanaume kuwatamani na hatimaye kuwabaka. 

Sheikh Abdulrahman aliongeza kwa kusema kuwa, ni jambo la kawaida kwa siku za hivi karibuni, wake na mabinti wa waumini wa Kiislamu kutembea nusu uchi, huku wazazi wakiona jambo hilo ni sawa na la kawaida bila kujua wanamkosea Mwenyezi Mungu. 

"Mabinti zetu na wake zetu, siku hizi wanatembea uchi uchi... uchi... kabisa na sisi tunaona sawa ... mwanamke anavaa nguo nyepesi na kuonyesha ramani ya mwili wake.... hapo akibakwa atalaumu nani na hali mwenyewe anajitangaza kubakwa... tena ni mabinti na wake za waumini ambao safu ya kwanza ya swala hawakosi... tukemee na tukosane nao", alisema Sheikh huyo. 

Na kuongeza kuwa, hata ndani ya Qur'an, Mtume Muhammad (saw) aliambiwa na Mwenyezi Mungu (sw) kuwa awaambie wake zake na mabinti zake kujistiri na wake wa waumini, ili kuwafanya wasipate kero kutoka kwa wanaume, kuwataka, kwani wajitambulisha kuwa wacha Mungu. 

Aidha, Sheikh alilaumu chama cha waandishi wa habari wanawake nchini (TAMWA), kutokana na hoja waliyopeleka bungeni ambayo imepitishwa kuwa muswada tayari kuwa sheria juu ya kujamiiana bila kupeleka na hoja ya kukemea na kukataza uvaaji nguo fupi kwa wanawake. 

Alisema kuwa ni wanawake wenyewe wanaojirahisisha kwa kutojisitiri miili yao. 

"Iweje iwepo sheria ya kuwalaumu wabakaji, huku hakuna sheria kwa wenye kushawishi, ni uongo na utafutaji sifa kwa viongozi wa TAMWA, kwani nao pia huvaa nguo fupi maofisini mwa", alidai Sheikh Abdulrahman. 

Hivi karibuni TAMWA ilipeleka hoja bungeni kuhusiana na masuala ya kujamiiana na kuzuia kubaka. 

Sheria hiyo baada ya kupitishwa na Bunge inategemewa kuanza kutumika mwakani, iwapo itatiwa saini na Rais Benjamin Mkapa, kuidhinisha kuwa sheria. 
 
 
 

SHEIKH Mohamed Mustafa. 

Madrasat Al-Hujuun washerehekea mwaka mpya 

Na Mwandishi Wetu 

AKINA mama wa Madrasat Al-Hujuun Kitangiri, Mwanza walifanya hafla ya kusherehekea mwaka mpya wa Kiislamu hivi karibuni. 

Katika sherehe hiyo iliyotanguliwa na usomaji wa Qur'an, ulifuatiwa na risala ya akina mama kwa wageni waliohudhuria sherehe hiyo. 

Risala ya akina mama hao pamoja na mengine, kubwa mno lilikuwa kulaani mauaji ya Waislamu wa Mwembechai na kudhalilishwa kwa akina mama wa Kislamu. 

Aidha, risala hiyo ilikiita kitendo hicho ni cha ukiukwaji wa haki za binadamu na kitendo cha kinyama. 

Risala hiyo iliyosomwa na Mwenyekiti wa Madrasa hiyo, Bibi Ziyada Ramadhani uliilaumu serikali kwa kile walichokiita ubaguzi. Walisema serikali ya Tanzania inajidai kila siku kuwa haina dini, lakini kwa kitendo hicho imedhihirisha inayo dini yake. 

Akina mama hao waliendelea kueleza katika risala yao kuwa, akinamama wa Kiislamu na Waislamu wote katika nchi hii wanaonekana siyo binadamu wanaostahili kupewa haki kama akina mama wengine na raia wengine. Na hii ni kwa sababu ya dini yao ya Kiislamu. 

Kinachoshangaza walisema ni kuona serikali inapiga kelele kuhusu hazi za akina mama wa Kitanzania na kupambana na wale wanaowadhalilisha, lakini udhalilishaji unapofikia kwa akina mama wa Kiislamu inaonekana si tatizo. 

Wakati huo huo, Madrasa Sharifatur-Rahman iliyopo Tandale, Mtogole ilifanya hafla ya kuukaribisha mwaka mpya wa 1419 madrasani hapo hivi karibuni. 

Katika hafla hiyo, mgeni rasmi Alhaj Yusuf Zakaria alisisitiza umuhimu wa kuwaelimisha watoto na akina mama ili kujenga jamii yenye maadili mema. 

Alihimiza Waislamu wajenge na kuendesha vituo cha kulelea watoto, shule za awali za watoto (Nursery School) n.k. 

Awali Maalim Kitwana alitoa ufafanuzi juu ya dhana potofu iliyojengeka juu ya kutenganisha elimu - elimu ya dini na dunia. Alisema elimu zote ni lazima zisomwe na zote ni muhimu. Ili kuisaidia Madrasa hiyo, uliendeshwa mnada na michango ambapo fedha taslimu na ahadi zilitolewa. 

 
 

YALIYOMO
 

TAHARIRI  

Maoni yetu: 
Kama hodari wa kuhoji Tuhoji pia Tume ya Majeshi ya Vita 

Waraka wa Abu Aziz  

Unafiki si suala la wakati fulani  
  
Wakatoliki wawili wasilimu 

Ashitakiwa baada kusilimu 

Historia ya harakati za ukombozi wa Kashmir 

Sheikh wa Wilaya Same ahimiza Waislamu kushiriki tamasha 

Sheikh awataka wanawake wajistiri 

Madrasat Al-Hujuun washerehekea mwaka mpya 
 
Kutoa talaka ovyo ovyo ni kuchupa mipaka ya Allah - Ust. Khamis Salim 

Uislamu ni mfumo wa maisha - Mbukuzi 

Pole ya Mwinjilisti Kusupa ni kejeli 
 
 

 

 
 Maoni yoyote kuhusu ukarasa huu yapelekwe kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
An-nuur Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita