|
AN-NUUR
|
| HOJA BINAFSI
Maendeleo ya Tanzania ni ndoto Na Fatma Mussa MAENDELEO ni kitendo cha kupiga hatua, toka kwenye hali moja kuelekea kwenye hali nyingine. Yaani kutoka kwenye hali duni kwenda kwenye hali nzuri zaidi. Na kwa kawaida sehemu yoyote ile maendeleo hayawezi kuja hivi hivi, lazima yafanyiwe kazi ili yapatikane. Kazi hiyo haitegemewi kufanywa na mwingine yoyote isipokuwa watawala na watawaliwa (serikali na raia). Watawala wao ndio wenye jukumu la kupanga na kuratibu mipango na kutafuta njia za kusaidia utekelezaji wake ili watawaliwa waweze kufanya hayo ambayo yameshapangwa. Katika wakati huu wa sasa ambao ulimwengu mzima unaimba wimbo mmoja wa kuelekea katika karne ya 21, karne ya maendeleo ya sayansi na teknolojia. Nchi mbalimbali zinajitahidi kuchukua hatua mpya za kuyaendea maendeleo hayo ya sayansi na teknolojia. Miongoni mwa nchi hizo ni hii nchi yetu ya Tanzania. Katika nchi yetu ya Tanzania, jitihada za makusudi zinafanyika kuyaendea maendeleo kama vile, maendeleo ya viwanda, kuboresha elimu na hata kubinafsisha mashirika ya umma ili yaweze kufanyakazi kwa ufanisi zaidi. Kwa bahati mbaya katika nchi yetu viwanda vinavyotiliwa mkazo ni viwanda vya bia, viwanda vya sigara ambavyo badala ya kumuendeleza mwananchi vinamdumaza zaidi na hata kumuharibu afya yake kiasi cha kumfanya ashindwe hata kufanya kazi kwa bidii. Halikadhalika, hivi leo kila kona utakayokatiza lazima ukumbane na matangazo ya pombe na sigara n.k. Hii inathibitisha ni namna gani Watanzania walivyo walevi wa kupindukia. Mbaya zaidi ulevi umekuwa ukisifiwa na wananchi wakihamasishwa kwa lugha nzuri ili waone kuwa ulevi hauathiri kitu chochote, tunaambiwa imani "spirit" ya taifa letu ni pombe aina ya Konyagi. Hiyo haitoshi, urithi wetu pia ni Safari, baada ya kazi Tusker, asili yetu Serengeti . Na ukitaka upate nguvu Guiness. Hivi mtu anayejengewa mazingira ya kuwa muda wote awe anafikiria pombe tu, ni saa ngapi atafikiria maendeleo ya nchi yake. Halafu mtu kama huyo ndiye anayetarajiwa kuleta maendeleo ya nchi. Vilevile, sasa hivi kumekuwa na wimbi kubwa la mchafuko na muharibiko wa maadili ya jamii, na imekuwa ikipigiwa kelele kuwa ubakaji umezidi, heshima hakuna, watu wanaishi kama wanyama au zaidi ya wanyama. Na ikaonekana kuwa ili kurekebisha hali hiyo inabidi sheria kali ziwekwe kwa wahusika. Lakini serikali yetu inashindwa kutambua kuwa suala si sheria au adhabu kali, kinachotakiwa ni sheria au adhabu muafaka. Adhabu ambayo itamfanya mfanyaji asirudie na waliotaka kufanya wasijaribu. Ili kuwathibitishia kuwa sheria kali sio suluhisho la tatizo, ni pale ilipopitishwa sheria ya makosa ya kujamiiana. Siku sheria ile ilipotangazwa rasmi idadi ya kesi za ubakaji na kunajisi watoto ziliongezeka na vyombo vya habari vilikuwa vinaripoti kuwa, pamoja na kupitishwa sheria kali kuhusu ubakaji n.k. kiwango cha kesi hizo kimeongezeka kwa kasi, hii inathibitisha ni namna gani sheria kali hazisaidii. Halikadhalika, serikali yetu haiangalii nini chanzo cha tatizo, inaliangalia tatizo lenyewe, hivi unafikiri watu walizowea kulewa hovyo wataona kuwa kumbaka mtu ni jambo baya na ni kosa. Vile vile serikali yenyewe ndiyo inayochochea masuala ya ukahaba na uzinifu, makasino yanaongezeka kila kukipambazuka. Imefikia hatua watoto nao wanachochewa kufanya zinaa, hata na viongozi wa nchi, kwa kuwataka wazazi wasione aibu kuwapa watoto wao kondomu. Hivi serikali yetu inafikiria katika hali kama hii watu saa zote wanawaza zinaa na ulevi ni saa ngapi watafikiria kuleta maendeleo ya nchi yao. Hivi kweli katika nchi kama hii ambayo Grosari, baa na Makasino ni mengi kuliko shule za awali (Nursery school) na shule za msingi, maendeleo yanatarajiwa yatokee wapi. Kama hali hii haitarekebishwa, basi maendeleo katika Tanzania itakuwa ni ndoto tena ndoto ya mchana ambayo mtu unaota huku umesimama, unatembea au ukiwa jukwaani! |
YALIYOMO
TAHARIRI Iran ina agenda gani? Mauaji,udhalilishaji Mwembechai: Wanawake
Waislamu waandamana Tabora Na Mwandishi Wetu 'Serikali ieleze hatua iliyochukua
kuhusu mauaji Mwembechai' ‘Musiwasingizie wake zenu maovu’
Barua za wasomaji
|
Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua kwa: webmaster@islamtanzania.org