|
AN-NUUR
|
Mauaji,udhalilishaji
Mwembechai:
Na Mwandishi Wetu MAMIA ya wanawake Waislamu waliokuwa wakiandamana mjini Tabora walisimama kwa muda mbele ya Kanisa la Moravian na kutoa kilio chao kwa Mwenyezi Mungu dhidi ya wale walioshiriki kuwaua Waislamu Mwembechai na kuwadhalilisha wanawake Waislamu. Mbele kidogo ya Kanisa hilo kuna Msikiti, Masjid Aziz ambapo pia walisimama na kuwaombea dua mashahidi wa Mwembechai. Wamesema kwamba katika Kanisa la Moravian ndipo zilipotolewa kauli za kukomesha mihadhara Januari 3 mwaka huu, kauli ambazo zilikuja kuzaa kadhia ya Mwembechai kwa hiyo ni mahali munasibu kutolea kilio chao. Maandamano ya akina mama hao yalianzia katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa Mtaa wa Gongoni saa 2:30 asubuhi, kupitia barabara ya Kazima kisha barabara ya Mwanza. Baada ya kuomba dua mbele ya Kanisa la Moravian, waliendelea kupitia mtaa wa Rufita na kuvuka tena barabara ya Kazima na kuelekea eneo la Ng'ambo ambapo walipita mitaa ya Kitete, Kitunda, Itetemya na kupitia Kituo Kikuu cha Polisi Tabora mpaka Msikiti wa Shirika la Reli. Kutoka hapo waliingia tena barabara ya Kazima. Wanawake hao waliobeba mabango yaliyokuwa na ujumbe maalum kwa wahusika, walimalizia maandamano yao katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa saa 5:30 asubuhi ambapo lilifanyika kongamano. Mwisho wa kongamano hilo wito ulitolewa kwa Waislamu kote nchini kuutumia vizuri uhuru wao wa kupiga kura vinginevyo watakuwa wanajidhuru wenyewe kama mshumaa. Mshumaa unaowaangazia wengine huku wenyewe ukijiunguza na kujimaliza. Hayo yamesemwa na Sheikh maarufu mjini Tabora Sheikh Ali Salala wakati akifunga kongamano hilo Septemba 20, mwaka huu. Wito huo wa Sheikh Salala umekuja kufuatia mada mbalimbali na mjadala katika kongamano zilizoonyesha kwamba ipo dhulma inayofanywa dhidi ya Waislamu na viongozi wa kisiasa ambao wamepata madaraka kupitia kura za wananchi. Pamoja na wito huo, wanawake Waislamu waliokutana katika kongamano hili walikariri kilio cha Waislamu kwamba waliowaua Waislamu pale Mwembechai wafikishwe mahakamani. Aidha, waliazimia kuimarisha elimu kwao na watoto wao ikiwa ni pamoja na kudumisha maadili ya Uislamu. Walimtaka kila mwanamke Muislamu atambuliwe kwa kitambulisho chake cha Hijab na kuwalaani wale wote wanaokiuka maadili kwa kujichubua nyuso zao na kubadili nywele. Waliwaomba Masheikh wawe imara katika kusimamia maadili ya Kiislamu na kuwataka wasishiriki kufungisha ndoa zenye ngoma na mambo mengine yaliyo kinyume na Uislamu. |
YALIYOMO
TAHARIRI Iran ina agenda gani? Mauaji,udhalilishaji Mwembechai: Wanawake
Waislamu waandamana Tabora Na Mwandishi Wetu 'Serikali ieleze hatua iliyochukua
kuhusu mauaji Mwembechai' ‘Musiwasingizie wake zenu maovu’
Barua za wasomaji
|
Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua kwa: webmaster@islamtanzania.org